Kitabu cha Pili cha Samweli 3:1-39

  • Nyumba ya Daudi yazidi kupata nguvu (1)

  • Wana wa Daudi (2-5)

  • Abneri ajiunga na Daudi (6-21)

  • Yoabu amuua Abneri (22-30)

  • Daudi amwombolezea Abneri (31-39)

3  Vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi viliendelea kwa muda mrefu; Daudi akazidi kupata nguvu,+ lakini nyumba ya Sauli ikazidi kudhoofika hatua kwa hatua.+  Wakati huo, Daudi akazaa wana huko Hebroni.+ Mzaliwa wake wa kwanza aliitwa Amnoni+ na mama yake alikuwa Ahinoamu+ wa Yezreeli.  Mzaliwa wake wa pili alikuwa Kileabu na mama yake alikuwa Abigaili,+ mjane wa Nabali Mkarmeli; na wa tatu alikuwa Absalomu+ mwana wa Maaka, binti ya Talmai+ mfalme wa Geshuri.  Wa nne alikuwa Adoniya+ mwana wa Hagithi, na wa tano alikuwa Shefatia mwana wa Abitali.  Wa sita alikuwa Ithreamu mwana wa Egla, mke wa Daudi. Hao ndio wana ambao Daudi aliwazaa huko Hebroni.  Vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi vilipokuwa vikiendelea, Abneri+ aliendelea kuimarisha cheo chake katika nyumba ya Sauli.  Awali Sauli alikuwa na suria aliyeitwa Rispa,+ binti ya Aya. Baadaye Ish-boshethi+ akamuuliza Abneri: “Kwa nini ulifanya ngono na suria wa baba yangu?”+  Abneri akakasirika sana kwa sababu ya maneno ya Ish-boshethi na kusema: “Je, mimi ni kichwa cha mbwa kutoka Yuda? Mpaka leo, nimeitendea kwa upendo mshikamanifu nyumba ya Sauli baba yako, ndugu zake, na rafiki zake, nami sijakusaliti kwa kukutia mikononi mwa Daudi; lakini leo unanishutumu kwa sababu ya kosa linalohusu mwanamke.  Mungu na aniadhibu mimi Abneri, tena vikali, nisipomtendea Daudi kama Yehova alivyomwapia:+ 10  kwamba atauhamisha ufalme kutoka katika nyumba ya Sauli na kuimarisha kiti cha ufalme cha Daudi juu ya Israeli na juu ya Yuda, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba.”+ 11  Ish-boshethi hakuthubutu kumwambia Abneri hata neno moja zaidi, kwa sababu alimwogopa Abneri.+ 12  Papo hapo Abneri akawatuma wajumbe kwa Daudi, akisema: “Nchi hii ni ya nani?” Akaongezea: “Fanya agano pamoja nami, nami nitafanya lolote niwezalo* kuwageuza Waisraeli wote wawe upande wako.”+ 13  Daudi akamwambia: “Vema! Nitafanya agano pamoja nawe. Lakini nakuomba ufanye jambo moja tu, usithubutu kuja mbele yangu mpaka umlete kwanza Mikali,+ binti ya Sauli, utakapokuja kuniona.” 14  Kisha Daudi akawatuma wajumbe kwa Ish-boshethi,+ mwana wa Sauli, akisema: “Nipe mke wangu Mikali, niliyemchumbia kwa magovi 100 ya Wafilisti.”+ 15  Kwa hiyo Ish-boshethi akawatuma watu wamchukue Mikali kutoka kwa Paltieli+ mumewe, mwana wa Laishi. 16  Lakini mume wake akaenda pamoja naye, akamfuata akilia mpaka Bahurimu.+ Kisha Abneri akamwambia: “Nenda zako, rudi!” Kwa hiyo akarudi. 17  Basi Abneri akatuma ujumbe kwa wazee wa Israeli, akisema: “Kwa muda fulani mlitaka Daudi awe mfalme wenu. 18  Sasa chukueni hatua, kwa maana Yehova alimwambia hivi Daudi: ‘Kwa mkono wako wewe Daudi mtumishi wangu+ nitawaokoa watu wangu Waisraeli kutoka mikononi mwa Wafilisti na kutoka mikononi mwa maadui wao wote.’” 19  Ndipo Abneri akazungumza na watu wa Benjamini.+ Pia, Abneri akaenda kuzungumza na Daudi faraghani kule Hebroni ili kumwambia mambo ambayo Waisraeli na nyumba yote ya Benjamini walikuwa wamekubaliana. 20  Abneri alipofika kwa Daudi kule Hebroni akiwa na wanaume 20, Daudi alimwandalia karamu pamoja na wanaume waliokuwa naye. 21  Halafu Abneri akamwambia Daudi: “Acha niende nikawakusanye pamoja Waisraeli wote kwako bwana wangu mfalme, ili wafanye agano pamoja nawe, nawe utakuwa mfalme juu ya kila kitu upendacho.”* Basi Daudi akamruhusu Abneri aende, akaenda zake kwa amani. 22  Wakati huohuo, watumishi wa Daudi na pia Yoabu walirudi baada ya kufanya uvamizi, walileta nyara nyingi sana. Abneri hakuwa tena pamoja na Daudi huko Hebroni, kwa maana alikuwa amemruhusu aende zake kwa amani. 23  Yoabu+ alipowasili na jeshi lote lililokuwa pamoja naye, aliambiwa hivi: “Abneri+ mwana wa Neri+ alikuja kwa mfalme, naye akamruhusu aende zake, na Abneri akaenda zake kwa amani.” 24  Basi Yoabu akaingia kwa mfalme na kumwambia: “Umefanya nini? Abneri alikuja kwako. Kwa nini ulimruhusu aende zake, akafanikiwa kutoroka? 25  Unamjua Abneri mwana wa Neri! Alikuja hapa kukupumbaza, kuchunguza shughuli zako zote, na kujua kila jambo unalofanya.” 26  Basi Yoabu akaondoka mbele ya Daudi, akawatuma wajumbe wamfuatie Abneri, wakamkuta kwenye tangi la maji la Sira na kumrudisha; lakini Daudi hakujua lolote kuhusu jambo hilo. 27  Abneri aliporudi Hebroni,+ Yoabu akampeleka pembeni ndani ya lango ili azungumze naye faraghani. Hata hivyo, Yoabu akamchoma kwa upanga tumboni, naye akafa;+ kwa sababu alimuua* Asaheli ndugu yake.+ 28  Daudi aliposikia habari hizo baadaye, alisema: “Mimi na ufalme wangu hatuna hatia milele mbele za Yehova kwa sababu ya damu+ ya Abneri mwana wa Neri. 29  Na irudi juu ya kichwa cha Yoabu+ na juu ya nyumba yote ya baba yake. Nyumba ya Yoabu isikose kamwe mwanamume anayetokwa na umajimaji+ au mtu mwenye ukoma+ au mwanamume anayetumikia kwenye gurudumu la mfumaji* au anayeuawa kwa upanga au asiye na chakula!”+ 30  Basi Yoabu na Abishai+ ndugu yake walimuua Abneri+ kwa sababu alimuua Asaheli ndugu yao vitani+ kule Gibeoni. 31  Kisha Daudi akamwambia Yoabu na watu wote waliokuwa pamoja naye: “Rarueni mavazi yenu na mvae nguo za magunia, mwombolezeeni Abneri kwa sauti.” Mfalme Daudi mwenyewe alikuwa akitembea nyuma ya machela ya kubebea maiti. 32  Walimzika Abneri huko Hebroni; na mfalme akalia kwa sauti kubwa kwenye kaburi la Abneri, na watu wote wakalia. 33  Mfalme akamwimbia Abneri wimbo wa maombolezo akisema: “Je, Abneri alipaswa kufa kama anavyokufa mtu mpumbavu? 34  Mikono yako haikuwa imefungwa,Na miguu yako haikuwa imefungwa pingu.* Ulianguka kama mtu anayeangushwa na wahalifu.”*+ Ndipo watu wote wakamlilia tena. 35  Baadaye watu wote wakaja kumpa Daudi mkate wa faraja* kungali mchana, lakini Daudi akaapa hivi: “Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa nitaonja mkate au kitu kingine chochote kabla ya jua kutua!”+ 36  Watu wote wakaona jambo hilo, nalo likawapendeza. Watu wote walipendezwa na jambo hilo kama walivyopendezwa na mambo yote yaliyofanywa na mfalme. 37  Basi watu wote* na Waisraeli wote wakajua siku hiyo kwamba si mfalme aliyeagiza Abneri mwana wa Neri auawe.+ 38  Kisha mfalme akawaambia hivi watumishi wake: “Je, hamjui kwamba mkuu na mtu mashuhuri ameanguka leo katika Israeli?+ 39  Niko dhaifu leo, ingawa nimetiwa mafuta kuwa mfalme,+ na wanaume hawa, wana wa Seruya,+ ni wakatili sana kwangu.+ Yehova na amlipe mtenda maovu kulingana na uovu wake mwenyewe.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “na tazama! mkono wangu uko pamoja nawe ili.”
Au “ambacho nafsi yako inatamani.”
Tnn., “kwa sababu ya damu ya.”
Huenda maneno hayo yanarejelea mwanamume mlemavu aliyelazimika kufanya kazi ya wanawake.
Tnn., “kwa shaba.”
Tnn., “wana wa ukosefu wa uadilifu.”
Au “mkate wa maombolezo.”
Yaani, watu wote wa Daudi.