Kitabu cha Pili cha Samweli 5:1-25

  • Daudi awekwa kuwa mfalme wa nchi yote ya Israeli (1-5)

  • Yerusalemu latekwa (6-16)

    • Sayuni, Jiji la Daudi (7)

  • Daudi awashinda Wafilisti (17-25)

5  Baada ya muda makabila yote ya Israeli yakaja kwa Daudi huko Hebroni+ na kusema: “Tazama! Sisi ni mfupa wako na nyama yako.*+  Zamani, Sauli alipokuwa mfalme wetu, ni wewe uliyewaongoza Waisraeli vitani.*+ Na Yehova alikuambia hivi: ‘Utawachunga watu wangu Waisraeli, nawe utakuwa kiongozi wa Israeli.’”+  Basi wazee wote wa Israeli wakaja kwa mfalme huko Hebroni, na Mfalme Daudi akafanya agano nao+ huko Hebroni mbele za Yehova. Kisha wakamtia mafuta Daudi awe mfalme wa Israeli.+  Daudi alikuwa na umri wa miaka 30 alipowekwa kuwa mfalme, naye alitawala kwa miaka 40.+  Huko Hebroni alitawala Yuda kwa miaka 7 na miezi 6, na huko Yerusalemu+ alitawala Israeli yote na Yuda kwa miaka 33.  Mfalme na wanaume wake wakaenda Yerusalemu kuwashambulia Wayebusi+ waliokuwa wakiishi nchini. Walimdhihaki Daudi wakisema: “Hutaingia humu kamwe! Hata vipofu na vilema watakufukuza.” Hivi ndivyo walivyofikiri: ‘Daudi hataingia humu kamwe.’+  Hata hivyo, Daudi akaiteka ngome ya Sayuni, ambayo sasa ni Jiji la Daudi.+  Basi siku hiyo Daudi akasema: “Wale wanaowashambulia Wayebusi wanapaswa kupitia kwenye mfereji wa maji ili wawaue ‘vilema na vipofu,’ wanaomchukia Daudi!”* Ndiyo sababu watu wanasema: “Vipofu na vilema hawataingia nyumbani.”  Kisha Daudi akaanza kukaa katika ngome hiyo, nayo ikaitwa* Jiji la Daudi; na Daudi akaanza kujenga pande zote kuanzia kwenye Kilima*+ kuja ndani.+ 10  Kwa hiyo Daudi akawa mkuu zaidi na zaidi,+ na Yehova Mungu wa majeshi alikuwa pamoja naye.+ 11  Mfalme Hiramu+ wa Tiro akawatuma wajumbe kwa Daudi, na kupeleka mbao za mierezi,+ maseremala, na waashi wa kujenga kuta, nao wakaanza kumjengea Daudi nyumba.*+ 12  Na Daudi akajua kwamba Yehova alikuwa amemwimarisha kabisa kuwa mfalme wa Israeli+ na kwamba alikuwa ameukweza ufalme wake+ kwa ajili ya watu Wake Waisraeli.+ 13  Baada ya kutoka Hebroni, Daudi alichukua masuria+ na wake zaidi huko Yerusalemu, nao wakamzalia Daudi wana na mabinti zaidi.+ 14  Haya ndiyo majina ya watoto wake waliozaliwa Yerusalemu: Shamua, Shobabu, Nathani,+ Sulemani,+ 15  Ibhari, Elishua, Nefegi, Yafia, 16  Elishama, Eliada, na Elifeleti. 17  Wafilisti waliposikia kwamba Daudi alikuwa ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Waisraeli wote,+ Wafilisti wote wakapanda kuja kumtafuta Daudi.+ Daudi aliposikia jambo hilo, akashuka kuingia ndani ya ngome.+ 18  Kisha Wafilisti wakaja na kuenea katika Bonde la* Refaimu.+ 19  Daudi akamuuliza Yehova:+ “Je, nipande kwenda kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Ndipo Yehova akamwambia Daudi: “Panda uende, nami hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”+ 20  Basi Daudi akaenda Baal-perasimu na kuwaua huko. Ndipo akasema: “Yehova amewapasua na kuwapita+ maadui wangu mbele yangu, kama ufa uliopasuliwa na maji.” Ndiyo sababu alipaita mahali hapo Baal-perasimu.*+ 21  Wafilisti wakaacha sanamu zao hapo, na Daudi na wanaume wake wakazichukua na kwenda nazo. 22  Baadaye Wafilisti wakaja tena na kuenea katika Bonde la* Refaimu.+ 23  Daudi akamwomba Yehova ushauri, lakini Akasema: “Usipande moja kwa moja. Badala yake, zunguka nyuma yao, uwashambulie mbele ya vichaka vya mibaka. 24  Na utakaposikia sauti ya watu wakipiga mwendo juu ya vichaka vya mibaka, tenda bila kusita, kwa sababu mimi Yehova nitakuwa nimetangulia mbele yako kuliua jeshi la Wafilisti.” 25  Basi Daudi akafanya kama Yehova alivyomwamuru, akawaua Wafilisti+ kuanzia Geba+ mpaka Gezeri.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Tuna uhusiano wa damu nawe.”
Tnn., “uliyekuwa ukiwatoa nje na kuwaingiza ndani Waisraeli.”
Au “wanaoichukia nafsi ya Daudi.”
Au labda, “naye akaiita.”
Au “Milo.” Neno la Kiebrania linalomaanisha “jaza.”
Au “jumba la mfalme.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Maana yake “Bwana Anayepasua na Kupita.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”