Kitabu cha Pili cha Samweli 6:1-23

  • Sanduku la agano laletwa Yerusalemu (1-23)

    • Uza alikamata sanduku la agano na kuuawa (6-8)

    • Mikali amdharau Daudi (16, 20-23)

6  Daudi akawakusanya tena wanajeshi wote walio bora wa Israeli, wanaume 30,000.  Kisha Daudi na wanaume wote waliokuwa pamoja naye wakaondoka kwenda Baale-yuda ili kuleta Sanduku la Mungu wa kweli+ kutoka huko, ambalo mbele yake watu hulisifu jina la Yehova wa majeshi,+ anayeketi kwenye kiti cha ufalme juu ya* makerubi.+  Hata hivyo, wakaweka Sanduku la Mungu wa kweli juu ya gari jipya la kukokotwa+ ili walisafirishe kutoka katika nyumba ya Abinadabu,+ iliyokuwa kwenye kilima; na Uza na Ahio, wana wa Abinadabu, walikuwa wakiliongoza gari hilo jipya.  Basi wakalisafirisha Sanduku la Mungu wa kweli kutoka katika nyumba ya Abinadabu iliyokuwa kwenye kilima, na Ahio alikuwa akitembea mbele ya Sanduku hilo.  Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakisherehekea mbele za Yehova kwa ala za kila aina zilizotengenezwa kwa mbao za mberoshi, vinubi, vinanda vinginevyo,+ matari,+ matasa, na matoazi.+  Lakini walipofika kwenye uwanja wa kupuria wa Nakoni, Uza akaunyoosha mkono wake haraka na kulikamata Sanduku la Mungu wa kweli,+ kwa sababu ng’ombe walikuwa karibu kuliangusha.  Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Uza, na Mungu wa kweli akamuua+ papo hapo kwa sababu ya tendo lake lisilo la heshima,+ akafa hapo karibu na Sanduku la Mungu wa kweli.  Lakini Daudi akakasirika kwa sababu hasira kali ya Yehova iliwaka dhidi ya Uza; na tangu siku hiyo mahali hapo panaitwa Peres-uza.*  Basi Daudi akamwogopa Yehova+ siku hiyo na kusema: “Sanduku la Yehova linawezaje kuja kwangu?”+ 10  Daudi hakutaka kuleta Sanduku la Yehova mahali alipokuwa katika Jiji la Daudi.+ Badala yake, Daudi aliagiza lipelekwe katika nyumba ya Obed-edomu,+ Mgathi. 11  Sanduku la Yehova likaendelea kukaa katika nyumba ya Obed-edomu Mgathi kwa miezi mitatu, na Yehova akazidi kumbariki Obed-edomu na nyumba yake yote.+ 12  Mfalme Daudi akaambiwa hivi: “Yehova ameibariki nyumba ya Obed-edomu na vitu vyake vyote kwa sababu ya Sanduku la Mungu wa kweli.” Basi Daudi akaenda kulichukua Sanduku la Mungu wa kweli kutoka katika nyumba ya Obed-edomu na kulipandisha kwa shangwe katika Jiji la Daudi.+ 13  Wale waliobeba+ Sanduku la Yehova walipokuwa wamepiga hatua sita, Daudi alitoa dhabihu ya ng’ombe dume na mnyama aliyenoneshwa. 14  Daudi alikuwa akicheza dansi huku na huku mbele za Yehova kwa nguvu zake zote; na wakati wote huo Daudi alikuwa amevaa* efodi ya kitani.+ 15  Daudi na nyumba yote ya Israeli walikuwa wakilipandisha Sanduku+ la Yehova kwa kelele za shangwe+ na sauti ya pembe.+ 16  Lakini Sanduku la Yehova lilipoingia katika Jiji la Daudi, Mikali,+ binti ya Sauli, akaangalia chini kupitia dirishani, akamwona Mfalme Daudi akirukaruka na kucheza dansi huku na huku mbele za Yehova; naye akaanza kumdharau moyoni mwake.+ 17  Basi wakaliingiza ndani Sanduku la Yehova na kuliweka mahali pake ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amepiga ili aliweke humo.+ Kisha Daudi akatoa dhabihu za kuteketezwa+ na dhabihu za ushirika+ mbele za Yehova.+ 18  Daudi alipomaliza kutoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika, akawabariki watu katika jina la Yehova wa majeshi.⁠ 19  Pia, akawagawia watu wote, umati wote wa Waisraeli, kila mwanamume na mwanamke mkate wa mviringo, keki ya tende, na keki ya zabibu kavu, halafu watu wote wakaenda zao, kila mmoja nyumbani kwake mwenyewe. 20  Daudi aliporudi ili kuwabariki watu wa nyumba yake mwenyewe, Mikali, binti ya Sauli+ akatoka nje kumpokea Daudi. Mikali akasema: “Mfalme wa Israeli amejitukuza kwelikweli leo kwa kujifunua leo mbele ya macho ya vijakazi wa watumishi wake, kama tu mtu asiye na akili anavyojifunua waziwazi!”+ 21  Ndipo Daudi akamwambia Mikali: “Nilikuwa nikisherehekea mbele za Yehova, aliyenichagua mimi badala ya baba yako na nyumba yake yote na ambaye aliniweka mimi kuwa kiongozi wa watu wa Yehova, Waisraeli.+ Kwa hiyo, nitasherehekea mbele za Yehova, 22  nami nitajinyenyekeza zaidi hata kuliko nilivyofanya na kuwa mdogo hata machoni pangu mwenyewe. Lakini nitatukuzwa na hao vijakazi uliowataja.” 23  Basi Mikali,+ binti ya Sauli, hakuwa na watoto mpaka siku alipokufa.

Maelezo ya Chini

Au labda, “katikati ya.”
Maana yake “Ghadhabu Dhidi ya Uza.”
Tnn., “amejifunga.”