Barua ya Pili kwa Timotheo 4:1-22

  • “Timiza kikamili huduma yako” (1-5)

    • Hubiri neno kwa uharaka (2)

  • “Nimepigana pigano zuri” (6-8)

  • Maelezo ya binafsi (9-18)

  • Salamu za mwisho (19-22)

4  Ninakuagiza kwa uzito mbele za Mungu na Kristo Yesu, ambaye atawahukumu+ walio hai na wafu,+ na kwa ufunuo+ wake na Ufalme wake:+  Lihubiri neno;+ fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia,+ kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha.+  Kwa maana kutakuwa na wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye manufaa,*+ bali, kulingana na tamaa zao, watajikusanyia walimu ili masikio yao yafurahishwe.*+  Wataacha kuisikiliza ile kweli, nao watageukia hadithi za uwongo.  Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote, vumilia hali ngumu,+ fanya kazi ya mweneza-injili,* timiza kikamili huduma yako.+  Kwa maana mimi tayari ninamiminwa kama toleo la kinywaji,+ na wakati wangu wa kufunguliwa+ umekaribia sana.  Nimepigana pigano zuri,+ nimekimbia mbio mpaka mwisho,+ nimeishika imani.  Tangu sasa na kuendelea nimewekewa akiba ya taji la uadilifu,+ ambalo Bwana, aliye mwamuzi mwadilifu,+ atanipa kuwa thawabu katika siku ile,+ lakini si mimi tu, bali pia wote ambao wamependa kufunuliwa kwake.  Jitahidi kabisa ili uje kwangu upesi. 10  Kwa maana Dema+ ameniacha kwa sababu aliupenda mfumo wa mambo* wa sasa, naye ameenda Thesalonike, Kresensi ameenda Galatia, Tito ameenda Dalmatia. 11  Luka tu ndiye aliye pamoja nami. Mchukue Marko uje pamoja naye, kwa maana ni mwenye faida kwangu katika huduma. 12  Lakini nimemtuma Tikiko+ aende Efeso. 13  Utakapokuja, ilete ile kanzu niliyomwachia Karpo kule Troa, na vile vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi. 14  Aleksanda yule fundi wa shaba alinisababishia madhara mengi. Yehova* atamlipa kulingana na matendo yake.+ 15  Nawe pia jihadhari naye, kwa maana aliupinga ujumbe wetu kwa kadiri kubwa sana. 16  Katika kujitetea kwangu mara ya kwanza hakuna yeyote aliyekuja upande wangu, bali wote waliniacha—wasihukumiwe kwa jambo hilo. 17  Lakini Bwana alisimama karibu nami na kunitia nguvu, ili kupitia kwangu kazi ya kuhubiri itimizwe kikamili na mataifa yote yaisikie;+ nami niliokolewa kutoka katika kinywa cha simba.+ 18  Bwana atanikomboa kutoka katika kila tendo la uovu naye ataniokoa kwa ajili ya Ufalme wake wa mbinguni.+ Utukufu na uwe kwake milele na milele. Amina. 19  Uwape salamu zangu Priska na Akila+ na nyumba ya Onesiforo.+ 20  Erasto+ alibaki Korintho, lakini nilimwacha Trofimo+ akiwa mgonjwa huko Mileto. 21  Jitahidi kabisa ili ufike kabla ya majira ya baridi kali. Eubulo anakutumia salamu zake, na pia Pudensi na Lino na Klaudia na ndugu wote. 22  Bwana na awe pamoja na roho unayoonyesha. Fadhili zake zisizostahiliwa na ziwe pamoja nawe.

Maelezo ya Chini

Au “lenye afya; lenye faida.”
Au “waambiwe mambo wanayotaka kusikia.”
Au “endelea kuhubiri habari njema.”
Angalia Kamusi.