Kitabu cha Pili cha Wafalme 18:1-37

  • Hezekia, mfalme wa Yuda (1-8)

  • Maelezo kuhusu kuanguka kwa Israeli (9-12)

  • Senakeribu avamia Yuda (13-18)

  • Rabshake amdhihaki Yehova (19-37)

18  Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Hoshea+ mwana wa Ela mfalme wa Israeli, Hezekia+ mwana wa Mfalme Ahazi+ wa Yuda akawa mfalme.  Alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Abi* binti ya Zekaria.+  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova,+ kama alivyofanya Daudi babu yake.+  Yeye ndiye aliyeondoa mahali pa juu,+ akazivunjavunja nguzo takatifu, na kuukata ule mti mtakatifu.*+ Pia alimpondaponda yule nyoka wa shaba aliyetengenezwa na Musa;+ kwa maana mpaka wakati huo Waisraeli walikuwa wakimfukizia moshi wa dhabihu, na nyoka huyo alikuwa akiitwa sanamu ya nyoka wa shaba.*  Alimtumaini Yehova+ Mungu wa Israeli; na hakuna mfalme yeyote kati ya wafalme wote wa Yuda aliyekuwa kama yeye, kabla yake wala baada yake.  Alishikamana kabisa na Yehova.+ Hakugeuka na kuacha kumfuata; aliendelea kushika amri ambazo Yehova alimpa Musa.  Na Yehova alikuwa pamoja naye. Popote alipoenda, alitenda kwa hekima. Alimwasi mfalme wa Ashuru na kukataa kumtumikia.+  Aliwashinda pia Wafilisti+ mpaka Gaza na maeneo yake, kuanzia mnara wa walinzi mpaka jiji lenye ngome.*  Katika mwaka wa nne wa utawala wa Mfalme Hezekia, yaani, mwaka wa saba wa Hoshea+ mwana wa Ela mfalme wa Israeli, Mfalme Shalmanesa wa Ashuru alikuja kushambulia Samaria, akaanza kulizingira.+ 10  Nao wakaliteka+ baada ya miaka mitatu; Samaria lilitekwa katika mwaka wa sita wa utawala wa Hezekia, ambao ulikuwa mwaka wa tisa wa utawala wa Mfalme Hoshea wa Israeli. 11  Kisha mfalme wa Ashuru akawapeleka Waisraeli uhamishoni+ kule Ashuru na kuwaweka katika eneo la Hala na Habori kando ya mto Gozani na katika majiji ya Wamedi ili waishi humo.+ 12  Walipelekwa huko kwa sababu hawakuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wao, badala yake waliendelea kuvunja agano lake, mambo yote ambayo Musa mtumishi wa Yehova aliamuru.+ Hawakusikiliza wala kutii. 13  Katika mwaka wa 14 wa utawala wa Mfalme Hezekia, Senakeribu mfalme wa Ashuru+ alipanda kuja kuyashambulia majiji yote yenye ngome ya Yuda na kuyateka.+ 14  Kwa hiyo Mfalme Hezekia wa Yuda akatuma ujumbe huu kwa mfalme wa Ashuru kule Lakishi: “Nimekosea. Ondokeni, msinishambulie, nami nitalipa chochote mtakachonitoza.” Mfalme wa Ashuru akamtoza Mfalme Hezekia wa Yuda faini ya talanta 300 za fedha* na talanta 30 za dhahabu. 15  Basi Hezekia akawapa fedha yote iliyokuwa katika nyumba ya Yehova na katika hazina za nyumba ya mfalme.*+ 16  Wakati huo Hezekia aling’oa* milango ya hekalu+ la Yehova na miimo ambayo yeye mwenyewe, Mfalme Hezekia wa Yuda, alikuwa ameifunika kwa dhahabu,+ naye akampa mfalme wa Ashuru. 17  Kisha mfalme wa Ashuru akamtuma Tartani,* Rabsarisi,* na Rabshake* pamoja na jeshi kubwa kutoka Lakishi+ kwenda kwa Mfalme Hezekia kule Yerusalemu.+ Wakapanda kwenda Yerusalemu na kujipanga karibu na mfereji wa kidimbwi cha juu, kwenye barabara kuu ya uwanja wa mfuaji wa nguo.+ 18  Walipomwita mfalme atoke nje, Eliakimu+ mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba,* Shebna+ aliyekuwa mwandishi, na Yoa mwana wa Asafu aliyefanya kazi ya kuweka kumbukumbu, wakaenda nje kukutana nao. 19  Basi Rabshake akawaambia: “Tafadhali, mwambieni hivi Hezekia: ‘Mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru, anauliza, “Ujasiri wako unategemea msingi gani?+ 20  Unasema, ‘Nina mbinu na nguvu za kupigana vita,’ lakini hayo ni maneno matupu. Unamtumaini nani, hivi kwamba unathubutu kuniasi mimi?+ 21  Tazama! Unautumaini msaada wa utete huu uliopondeka, Misri,+ ambao mtu yeyote akiuegemea utamchoma kiganja na kukitoboa. Hivyo ndivyo Farao mfalme wa Misri alivyo kwa wote wanaomtumaini. 22  Nawe ukiniambia, ‘Tunamtumaini Yehova Mungu wetu,’+ je, si yeye ndiye ambaye mahali pake pa juu na madhabahu zake zimeondolewa na Hezekia,+ huku akiwaambia watu wa Yuda na Yerusalemu, ‘Mnapaswa kuinama mbele ya madhabahu hii hapa Yerusalemu’?”’+ 23  Basi sasa, tafadhali, fanya mkataba huu pamoja na bwana wangu mfalme wa Ashuru: nitakupa farasi 2,000 ikiwa unaweza kupata wapanda farasi wa kutosha idadi hiyo.+ 24  Basi, unawezaje kumzuia hata gavana mmoja aliye mdogo zaidi kati ya watumishi wa bwana wangu, huku ukiitumaini nchi ya Misri ili upate magari ya vita na wapanda farasi? 25  Sasa je, nimepanda kuja kushambulia mahali hapa ili kupaharibu bila kupewa idhini na Yehova? Yehova mwenyewe aliniambia, ‘Panda uende kuishambulia nchi hii na kuiharibu.’” 26  Ndipo Eliakimu mwana wa Hilkia, na Shebna+ na Yoa wakamwambia Rabshake:+ “Tafadhali, zungumza nasi watumishi wako kwa lugha ya Kiaramu,*+ kwa maana tunaweza kuielewa; usizungumze nasi kwa lugha ya Wayahudi huku watu walio ukutani wakisikia.”+ 27  Lakini Rabshake akawaambia: “Je, bwana wangu amenituma niwaambie ninyi na bwana wenu tu maneno haya? Je, sipaswi kuwaambia pia wanaume wanaoketi ukutani, wale watakaokula kinyesi chao wenyewe na kunywa mkojo wao wenyewe pamoja nanyi?” 28  Kisha Rabshake akasimama na kusema hivi kwa sauti kubwa kwa lugha ya Wayahudi: “Sikieni neno la mfalme mkuu, mfalme wa Ashuru.+ 29  Mfalme anasema hivi: ‘Msikubali Hezekia awadanganye, kwa maana hawezi kuwaokoa kutoka mikononi mwangu.+ 30  Na msikubali Hezekia awafanye mumtumaini Yehova mkisema: “Kwa hakika Yehova atatuokoa, na jiji hili halitatiwa mikononi mwa mfalme wa Ashuru.”+ 31  Msimsikilize Hezekia, kwa maana mfalme wa Ashuru anasema hivi: “Fanyeni amani pamoja nami na mjisalimishe,* na kila mmoja wenu atakula matunda ya mzabibu wake mwenyewe na matunda ya mtini wake mwenyewe na kunywa maji kutoka katika tangi lake mwenyewe, 32  mpaka nitakapokuja na kuwapeleka katika nchi iliyo kama nchi yenu wenyewe,+ nchi yenye nafaka na divai mpya, nchi yenye mikate na mashamba ya mizabibu, nchi yenye mizeituni na asali. Ndipo mtakapoishi, nanyi hamtakufa. Msimsikilize Hezekia, kwa maana anawapotosha kwa kusema, ‘Yehova atatuokoa.’ 33  Je, kuna mungu yeyote kati ya miungu ya mataifa ambaye amewahi kuiokoa nchi yake kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru? 34  Iko wapi miungu ya Hamathi+ na Arpadi? Iko wapi miungu ya Sefarvaimu,+ Hena, na Iva? Je, imeokoa Samaria kutoka mikononi mwangu?+ 35  Ni mungu yupi kati ya miungu yote ya nchi mbalimbali ambaye ameokoa nchi yake kutoka mikononi mwangu, hivi kwamba Yehova aokoe Yerusalemu kutoka mikononi mwangu?”’”+ 36  Lakini watu walikaa kimya, hawakumjibu neno lolote, kwa maana mfalme alikuwa amewaagiza hivi: “Msimjibu.”+ 37  Lakini Eliakimu mwana wa Hilkia, aliyekuwa msimamizi wa nyumba,* Shebna aliyekuwa mwandishi, na Yoa mwana wa Asafu aliyekuwa akifanya kazi ya kuweka kumbukumbu wakaja kwa Hezekia mavazi yao yakiwa yameraruliwa, wakamwambia maneno ya Rabshake.

Maelezo ya Chini

Ufupisho wa jina Abiya.
Angalia Kamusi.
Au “akiitwa Nehushtani.”
Yaani, kila mahali, penye watu wengi au wachache.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “jumba la.”
Tnn., “alikata na kuondoa.”
Au “msimamizi mkuu wa vinywaji vya mfalme.”
Au “ofisa mkuu wa makao ya mfalme.”
Au “kamanda.”
Au “jumba la mfalme.”
Au “Kisiria.”
Tnn., “Fanyeni baraka pamoja nami na mtoke nje na kuja kwangu.”
Au “jumba la mfalme.”