Kitabu cha Pili cha Wafalme 2:1-25

  • Eliya apelekwa juu katika dhoruba ya upepo (1-18)

    • Elisha apata vazi rasmi la Eliya (13, 14)

  • Elisha ayaponya maji ya Yeriko (19-22)

  • Dubu wawaua wavulana kutoka Betheli (23-25)

2  Yehova alipokuwa karibu kumchukua Eliya+ kuelekea mbinguni* katika dhoruba ya upepo,+ Eliya na Elisha+ wakaondoka Gilgali.+  Eliya akamwambia Elisha: “Kaa hapa, tafadhali, kwa sababu Yehova amenituma Betheli.” Lakini Elisha akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama unavyoishi,* sitakuacha.” Basi wakashuka kwenda Betheli.+  Kisha wana wa manabii* huko Betheli wakaja kwa Elisha na kumuuliza: “Je, unajua kwamba leo Yehova anamchukua bwana wako asiwe kiongozi wako?”+ Ndipo akajibu: “Tayari najua. Nyamazeni.”  Sasa Eliya akamwambia: “Elisha, tafadhali kaa hapa, kwa sababu Yehova amenituma Yeriko.”+ Lakini Elisha akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama unavyoishi,* sitakuacha.” Basi wakaenda Yeriko.  Kisha wana wa manabii waliokuwa Yeriko wakaenda kwa Elisha na kumuuliza: “Je, unajua kwamba leo Yehova anamchukua bwana wako asiwe kiongozi juu yako?” Ndipo akajibu: “Tayari najua. Nyamazeni.”  Sasa Eliya akamwambia: “Kaa hapa, tafadhali, kwa sababu Yehova amenituma Yordani.” Lakini Elisha akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi na kama unavyoishi,* sitakuacha.” Basi wote wawili wakaendelea na safari.  Na wana 50 wa manabii wakaenda pia, wakasimama na kuwatazama kwa mbali wote wawili wakiwa wamesimama kando ya Mto Yordani.  Kisha Eliya akachukua vazi lake rasmi,+ akaliviringa na kuyapiga maji, nayo yakagawanyika kushoto na kulia, basi wote wawili wakavuka ng’ambo kupitia nchi kavu.+  Mara tu walipovuka, Eliya akamwambia Elisha: “Omba jambo unalotaka nikutendee kabla sijachukuliwa na kukuacha.” Basi Elisha akamuuliza: “Tafadhali, naweza kupata mafungu mawili+ ya* roho yako?”+ 10  Eliya akajibu: “Umeomba jambo gumu. Ikiwa utaniona nitakapochukuliwa na kukuacha, itakuwa hivyo kwako; lakini usiponiona, jambo hilo halitatokea.” 11  Walipokuwa wakitembea, huku wakizungumza, kwa ghafla gari la moto na farasi wa moto+ wakawatenganisha, na Eliya akapanda kuelekea mbinguni* katika dhoruba ya upepo.+ 12  Elisha alitazama huku akipaza sauti, “Baba yangu, baba yangu! Gari la Israeli na wapanda farasi wake!”+ Alipotoweka kabisa machoni pake, akashika mavazi yake mwenyewe na kuyararua vipande viwili.+ 13  Ndipo akaliokota vazi rasmi+ la Eliya lililokuwa limeanguka kutoka kwa Eliya, akarudi na kusimama kwenye ukingo wa Yordani. 14  Kisha akachukua vazi rasmi la Eliya lililokuwa limeanguka kutoka kwake, akayapiga maji na kuuliza: “Yuko wapi Yehova, Mungu wa Eliya?” Alipoyapiga maji, yaligawanyika kushoto na kulia, Elisha akavuka ng’ambo.+ 15  Wana wa manabii waliokuwa Yeriko walipomwona kwa mbali, wakasema: “Roho ya Eliya imetua juu ya Elisha.”+ Basi wakaenda kukutana naye na kumwinamia mpaka ardhini. 16  Wakamwambia: “Hapa sisi watumishi wako tuna wanaume mashujaa 50. Tafadhali, waruhusu waende kumtafuta bwana wako. Labda roho ya* Yehova imemwinua juu na kumtupa juu ya mojawapo ya milima au katika mojawapo ya mabonde.”+ Lakini akawaambia: “Msiwatume.” 17  Hata hivyo, waliendelea kumsihi mpaka akaona aibu, kwa hiyo akasema: “Watumeni.” Wakawatuma wanaume 50, nao wakaendelea kumtafuta kwa siku tatu, lakini hawakumpata. 18  Waliporudi kwake, alikuwa anakaa Yeriko.+ Kisha akawauliza: “Je, sikuwaambia msiende?” 19  Baada ya muda watu wa jiji hilo wakamwambia Elisha: “Bwana wetu, unaona kwamba jiji hili liko mahali pazuri;+ lakini maji ni mabaya, na wakaaji wa nchi ni tasa.”* 20  Akawaambia: “Nileteeni bakuli dogo jipya, mweke chumvi ndani yake.” Basi wakamletea. 21  Kisha akatoka na kwenda kwenye chemchemi ya maji hayo, akatupa chumvi ndani yake+ na kusema: “Yehova anasema hivi: ‘Nimeyaponya maji haya. Hayatasababisha tena kifo wala utasa.’”* 22  Na maji hayo yameponywa mpaka leo hii, kulingana na neno alilosema Elisha. 23  Akapanda kutoka huko na kwenda Betheli. Alipokuwa akitembea njiani, wavulana fulani walitoka jijini na kuanza kumdhihaki,+ wakaendelea kumwambia: “Panda juu, wewe mwenye upara! Panda juu, wewe mwenye upara!” 24  Hatimaye akageuka na kuwatazama, akawalaani katika jina la Yehova. Ndipo dubu jike wawili+ wakatoka msituni na kuwararua vipandevipande watoto 42.+ 25  Kutoka huko, akaendelea na safari mpaka Mlima Karmeli,+ na kutoka huko akarudi Samaria.

Maelezo ya Chini

Au “angani.”
Au “nafsi yako inavyoishi.”
Inaonekana maneno “wana wa manabii” yanarejelea shule ya kuwafundisha manabii au chama cha manabii.
Au “nafsi yako inavyoishi.”
Au “nafsi yako inavyoishi.”
Au “sehemu mbili za.”
Au “angani.”
Au “upepo wa.”
Au labda, “yanaharibu mimba.”
Au labda, “kuharibu mimba.”