Kitabu cha Pili cha Wafalme 21:1-26

  • Manase, mfalme wa Yuda; jinsi alivyomwaga damu (1-18)

    • Jiji la Yerusalemu kuharibiwa (12-15)

  • Amoni, mfalme wa Yuda (19-26)

21  Manase+ alikuwa na umri wa miaka 12 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 55 huko Yerusalemu.+ Mama yake aliitwa Hefziba.  Manase alitenda maovu machoni pa Yehova, akafuata mazoea yenye kuchukiza ya mataifa+ ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.+  Alijenga upya mahali pa juu ambapo Hezekia baba yake alikuwa amebomoa,+ akajenga madhabahu kwa ajili ya Baali na kutengeneza mti mtakatifu,*+ kama alivyofanya Ahabu mfalme wa Israeli.+ Naye akaliinamia jeshi lote la mbinguni na kuliabudu.+  Alijenga pia madhabahu katika nyumba ya Yehova,+ ambayo Yehova alikuwa amesema hivi kuihusu: “Nitaweka jina langu Yerusalemu.”+  Naye alijenga madhabahu kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni+ katika nyua mbili za nyumba ya Yehova.+  Naye alimteketeza* motoni mwana wake mwenyewe; alifanya uchawi, alitafuta ishara za ubashiri,+ na kuwaweka rasmi watu wanaowasiliana na roho na wabashiri.+ Alitenda kwa kiwango kikubwa sana mambo maovu machoni pa Yehova, na kumkasirisha.  Akachukua sanamu ya kuchongwa ya mti mtakatifu*+ aliyokuwa ametengeneza na kuiweka ndani ya nyumba ambayo Yehova alikuwa amemwambia hivi Daudi na Sulemani mwanawe kuihusu: “Nitaweka jina langu milele katika nyumba hii na katika jiji la Yerusalemu, ambalo nimelichagua kati ya makabila yote ya Israeli.+  Nami sitaifanya tena miguu ya Waisraeli itangetange kutoka katika nchi niliyowapa mababu zao+ ikiwa watashika kwa uangalifu mambo yote niliyowaamuru,+ Sheria yote ambayo Musa mtumishi wangu aliwaagiza wafuate.”  Lakini hawakutii, na Manase aliendelea kuwapotosha, akasababisha watende uovu mkubwa zaidi kuliko uliofanywa na mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyaangamiza kutoka mbele ya Waisraeli.+ 10  Yehova aliendelea kusema hivi kupitia watumishi wake manabii:+ 11  “Manase mfalme wa Yuda amefanya mambo haya yote yenye kuchukiza; ametenda mambo maovu zaidi kuliko Waamori wote+ waliomtangulia,+ naye amesababisha watu wa Yuda watende dhambi kwa sanamu zake zenye kuchukiza.* 12  Kwa hiyo Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Tazama, ninaleta msiba mkubwa sana Yerusalemu+ na Yuda hivi kwamba masikio yote mawili ya yeyote atakayesikia habari zake yatawasha.+ 13  Nami nitanyoosha kamba ya kupimia juu ya Yerusalemu,+ kamba iliyotumika kupima Samaria+ na kutumia timazi iliyotumiwa kupima nyumba ya Ahabu,+ nami nitalifuta kabisa Yerusalemu liwe safi kama mtu anavyofuta bakuli liwe safi, akilifuta na kulipindua.+ 14  Nitawaacha watu waliobaki wa urithi wangu+ na kuwatia mikononi mwa maadui wao, nao wataporwa na kuchukuliwa nyara na maadui wao wote,+ 15  kwa sababu walitenda maovu machoni pangu nao waliendelea kunikasirisha tangu siku ambayo mababu zao walitoka Misri mpaka leo hii.’”+ 16  Manase pia alimwaga damu nyingi sana isiyo na hatia mpaka alipojaza Yerusalemu damu hiyo kutoka mwisho mmoja hadi mwingine,+ mbali na dhambi yake aliyosababisha Yuda kutenda kwa kufanya maovu machoni pa Yehova. 17  Na mambo mengine katika historia ya Manase na yote aliyofanya na dhambi alizotenda, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 18  Kisha Manase akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika bustani ya nyumba yake, katika bustani ya Uza;+ na Amoni mwanawe akawa mfalme baada yake. 19  Amoni+ alikuwa na umri wa miaka 22 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka miwili huko Yerusalemu.+ Mama yake aliitwa Meshulemethi binti ya Haruzi kutoka Yotba. 20  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, kama alivyofanya Manase baba yake.+ 21  Aliendelea kutembea katika njia zote ambazo baba yake alitembea, akaendelea kuziabudu na kuziinamia sanamu zenye kuchukiza ambazo baba yake aliabudu.+ 22  Kwa hiyo akamwacha Yehova Mungu wa mababu zake, naye hakutembea katika njia ya Yehova.+ 23  Hatimaye watumishi wa Amoni wakapanga njama dhidi yake na kumuua mfalme Amoni ndani ya nyumba yake mwenyewe. 24  Lakini watu wa nchi hiyo wakawaua wale wote waliopanga njama dhidi ya Mfalme Amoni, nao wakamweka Yosia mwanawe kuwa mfalme baada yake.+ 25  Na mambo mengine katika historia ya Amoni, mambo aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 26  Kwa hiyo wakamzika katika kaburi lake katika bustani ya Uza,+ na Yosia mwanawe+ akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Tnn., “alimpitisha.”
Angalia Kamusi.
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.