Kitabu cha Pili cha Wafalme 22:1-20

  • Yosia, mfalme wa Yuda (1, 2)

  • Maagizo ya kurekebisha hekalu (3-7)

  • Kitabu cha Sheria chapatikana (8-13)

  • Hulda atabiri msiba (14-20)

22  Yosia+ alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 31 huko Yerusalemu.+ Mama yake aliitwa Yedida binti ya Adaya kutoka Boskathi.+  Alitenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova na kutembea katika njia zote za Daudi babu yake,+ naye hakugeuka na kwenda kulia au kushoto.  Katika mwaka wa 18 wa Mfalme Yosia, mfalme huyo alimtuma mwandishi Shafani, mwana wa Azalia mwana wa Meshulamu, kwenye nyumba ya Yehova,+ akisema:  “Panda uende kwa kuhani mkuu Hilkia+ umwambie akusanye pesa zote zinazoletwa katika nyumba ya Yehova+ ambazo walinzi wa malango wanakusanya kutoka kwa watu.+  Waagize wawape wale waliowekwa kusimamia kazi katika nyumba ya Yehova, ili nao wawape wafanyakazi walio katika nyumba ya Yehova wanaopaswa kurekebisha sehemu zilizoharibika za* nyumba hiyo,+  yaani, wawape mafundi, wajenzi, na waashi, ambao watazitumia kununua mbao na mawe yaliyochongwa ili kurekebisha nyumba hiyo.+  Lakini hawapaswi kudaiwa hesabu yoyote ya matumizi ya pesa wanazopewa, kwa sababu ni waaminifu.”+  Baadaye kuhani mkuu Hilkia akamwambia mwandishi Shafani:+ “Nimepata kitabu cha Sheria+ katika nyumba ya Yehova.” Basi Hilkia akampa Shafani kitabu hicho, naye akaanza kukisoma.+  Kisha mwandishi Shafani akaenda kwa mfalme na kumwambia: “Watumishi wako wamekusanya* pesa zilizopatikana katika nyumba hiyo, nao wamewapa wale wanaosimamia kazi katika nyumba ya Yehova.”+ 10  Pia, mwandishi Shafani akamwambia mfalme: “Kuna kitabu+ ambacho kuhani Hilkia amenipa.” Kisha Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme. 11  Mara tu mfalme aliposikia maneno ya kitabu hicho cha Sheria, akayararua mavazi yake.+ 12  Halafu mfalme akamwagiza hivi kuhani Hilkia, Ahikamu+ mwana wa Shafani, Akbori mwana wa Mikaya, mwandishi Shafani, na Asaya mtumishi wa mfalme: 13  “Nendeni mkatafute ushauri wa Yehova kwa niaba yangu, kwa niaba ya watu, na kwa niaba ya watu wote wa Yuda kuhusu maneno ya kitabu hiki ambacho kimepatikana; kwa maana ghadhabu ya Yehova iliyowaka dhidi yetu ni kali,+ kwa sababu mababu zetu hawakutii maneno ya kitabu hiki kwa kuyashika mambo yote yaliyoandikwa kutuhusu.” 14  Basi kuhani Hilkia, Ahikamu, Akbori, Shafani, na Asaya wakaenda kwa nabii wa kike anayeitwa Hulda.+ Alikuwa mke wa Shalumu mwana wa Tikva mwana wa Harhasi, mtunzaji wa chumba cha mavazi, naye alikuwa akiishi katika Wilaya ya Pili ya Yerusalemu; wakazungumza naye huko.+ 15  Hulda akawaambia, “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mwambieni hivi mtu aliyewatuma kwangu: 16  “Yehova anasema, ‘Nitaleta msiba mahali hapa na kwa wakaaji wake, maneno yote ya kitabu ambacho mfalme wa Yuda amesoma.+ 17  Kwa sababu wameniacha na wanaifukizia miungu mingine+ moshi wa dhabihu ili kunikasirisha kwa kazi zote za mikono yao,+ ghadhabu yangu itawaka dhidi ya mahali hapa nayo haitazimwa.’”+ 18  Lakini mwambieni hivi mfalme wa Yuda aliyewatuma kutafuta ushauri wa Yehova: “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Kuhusu maneno ambayo umesikia, 19  kwa sababu moyo wako ulikuwa msikivu,* nawe ukajinyenyekeza+ mbele za Yehova uliposikia mambo niliyosema dhidi ya mahali hapa na wakaaji wake—kwamba watakuwa kitu cha kutisha na laana—nawe ukayararua mavazi yako+ na kulia mbele zangu, mimi pia nimekusikia, asema Yehova. 20  Ndiyo sababu nitakuzika pamoja na mababu zako,* nawe utalazwa kwa amani katika kaburi lako, na macho yako hayataona msiba wote nitakaoleta mahali hapa.’”’” Kisha wakampelekea mfalme jibu hilo.

Maelezo ya Chini

Au “kurekebisha nyufa zilizo katika.”
Tnn., “wamemimina.”
Tnn., “laini.”
Tnn., “nitakukusanya kwa watu wako.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.