Kitabu cha Pili cha Wafalme 23:1-37

  • Yosia afanya mabadiliko (1-20)

  • Pasaka yasherehekewa (21-23)

  • Yosia afanya mabadiliko zaidi (24-27)

  • Kifo cha Yosia (28-30)

  • Yehoahazi, mfalme wa Yuda (31-33)

  • Yehoyakimu, mfalme wa Yuda (34-37)

23  Basi mfalme akatuma ujumbe, na wazee wote wa Yuda na Yerusalemu wakakusanywa.+  Baada ya hayo mfalme akapanda kwenda katika nyumba ya Yehova pamoja na wanaume wote wa Yuda, wakaaji wote wa Yerusalemu, makuhani, na manabii—watu wote, kuanzia mdogo mpaka mkubwa. Akasoma, watu wote wakisikia, maneno yote ya kitabu+ cha agano+ kilichokuwa kimepatikana katika nyumba ya Yehova.+  Mfalme akasimama karibu na nguzo na kufanya agano* mbele za Yehova,+ kwamba atamfuata Yehova na kushika amri zake, vikumbusho vyake, na sheria zake kwa moyo wake wote na kwa nafsi* yake yote kwa kutekeleza maneno ya agano hilo yaliyoandikwa katika kitabu hicho. Watu wote wakakubali agano hilo.+  Halafu mfalme akamwagiza kuhani mkuu Hilkia,+ makuhani wa daraja la pili, na walinzi wa milango waondoe kutoka katika hekalu la Yehova vyombo vyote vilivyotengenezwa kwa ajili ya Baali, kwa ajili ya mti mtakatifu,*+ na kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni. Kisha akaviteketeza nje ya Yerusalemu kwenye matuta ya Kidroni, akapeleka majivu yake Betheli.+  Basi akawaondoa kabisa makuhani wa miungu ya kigeni, waliochaguliwa na wafalme wa Yuda kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu katika majiji ya Yuda na maeneo yanayozunguka Yerusalemu, na pia wale waliofukiza moshi wa dhabihu kwa Baali, kwa jua, kwa mwezi, kwa makundi ya nyota za unajimu, na kwa jeshi lote la mbinguni.+  Akauondoa mti mtakatifu*+ katika nyumba ya Yehova na kuupeleka nje ya Yerusalemu, katika Bonde la Kidroni, akauteketeza+ katika Bonde la Kidroni, akausaga mpaka ukawa mavumbi na kuyatawanya mavumbi hayo juu ya makaburi ya watu wa kawaida.+  Akabomoa pia nyumba za wanaume makahaba wa hekaluni+ zilizokuwa katika nyumba ya Yehova, mahali ambapo wanawake walikuwa wakifuma mahema ya ibada ya mti mtakatifu.*  Kisha akawaondoa makuhani wote katika majiji ya Yuda, naye akafanya mahali pa juu ambapo makuhani walifukizia moshi wa dhabihu pasifae kwa ibada, kuanzia Geba+ mpaka Beer-sheba.+ Alibomoa pia mahali pa juu palipokuwa kwenye malango yaliyokuwa katika njia ya kuingia kwenye lango la Yoshua mkuu wa jiji, malango yaliyokuwa upande wa kushoto mtu anapoingia katika lango la jiji.  Makuhani wa mahali pa juu hawakuhudumu kwenye madhabahu ya Yehova kule Yerusalemu,+ lakini walikula mikate isiyo na chachu pamoja na ndugu zao. 10  Pia alipafanya Tofethi,+ palipokuwa katika Bonde la Wana wa Hinomu*+ pasifae kwa ibada, ili mtu yeyote asimteketeze* motoni mwana wake au binti yake kwa ajili ya Moleki.+ 11  Pia farasi ambao wafalme wa Yuda walikuwa wamewaweka wakfu* kwa jua aliwazuia wasiingie katika nyumba ya Yehova kupitia chumba* cha Nathan-meleki ofisa wa makao ya mfalme, chumba kilichokuwa barazani; naye akayateketeza motoni magari yaliyowekwa wakfu kwa jua.+ 12  Mfalme alibomoa pia madhabahu ambazo wafalme wa Yuda walijenga kwenye paa+ la chumba cha juu cha Ahazi, na pia madhabahu ambazo Manase alijenga katika nyua mbili za nyumba ya Yehova.+ Alizivunjavunja na kutawanya mavumbi yake katika Bonde la Kidroni. 13  Na mahali pa juu palipokuwa mbele ya Yerusalemu upande wa kusini* wa Mlima wa Uharibifu,* mahali ambapo Sulemani mfalme wa Israeli alijenga kwa ajili ya Ashtorethi mungu wa kike mwenye kuchukiza wa Wasidoni; kwa ajili ya Kemoshi mungu mwenye kuchukiza wa Moabu; na kwa ajili ya Milkomu+ mungu mwenye kuchukiza wa Waamoni,+ mfalme alipafanya pasifae kwa ibada. 14  Naye akavunjavunja nguzo takatifu, akaikata miti mitakatifu*+ na kujaza mahali pake mifupa ya binadamu. 15  Alibomoa pia madhabahu iliyokuwa Betheli, mahali pa juu ambapo Yeroboamu mwana wa Nebati alijenga na ambapo palisababisha Waisraeli watende dhambi.+ Baada ya kuibomoa madhabahu hiyo na mahali pa juu, aliteketeza mahali hapo pa juu, akapasagasaga pakawa mavumbi, na kuuteketeza mti mtakatifu.*+ 16  Yosia alipogeuka na kuona makaburi yaliyokuwa mlimani, aliagiza mifupa itolewe katika makaburi hayo na kuteketezwa kwenye madhabahu, akaifanya madhabahu hiyo isifae kwa ibada, kulingana na neno la Yehova lililokuwa limesemwa na mtu wa Mungu wa kweli aliyetabiri kwamba mambo hayo yangetukia.+ 17  Kisha akauliza: “Lile jiwe la kaburi ninaloona pale ni la nani?” Ndipo watu wa jiji hilo wakamjibu: “Ni kaburi la mtu wa Mungu wa kweli kutoka Yuda+ aliyetabiri mambo haya uliyoitendea madhabahu ya Betheli.” 18  Kwa hiyo akasema: “Acheni apumzike. Mtu yeyote asiiguse mifupa yake.” Basi wakaiacha mifupa yake pamoja na mifupa ya yule nabii aliyetoka Samaria.+ 19  Yosia pia aliondoa nyumba zote za ibada zilizokuwa mahali pa juu katika majiji ya Samaria,+ ambazo wafalme wa Israeli walijenga na kumkasirisha Mungu, akazitendea kama alivyozitendea zile zilizokuwa Betheli.+ 20  Basi makuhani wote wa mahali pa juu waliokuwa mahali hapo akawatoa dhabihu juu ya madhabahu hizo, naye akateketeza mifupa ya wanadamu juu yake.+ Kisha akarudi Yerusalemu. 21  Kisha mfalme akawaamuru hivi watu wote: “Fanyeni Pasaka+ ya Yehova Mungu wenu kama ilivyoandikwa katika kitabu hiki cha agano.”+ 22  Pasaka kama hiyo haikuwa imewahi kufanywa tangu siku ambazo waamuzi walikuwa wakiongoza Israeli wala sikuzote za wafalme wa Israeli na wafalme wa Yuda.+ 23  Lakini katika mwaka wa 18 wa utawala wa Mfalme Yosia, Pasaka hiyo ya Yehova ilifanywa Yerusalemu. 24  Yosia pia aliwaondoa kabisa watu wote waliowasiliana na roho, wabashiri,+ sanamu za terafimu,*+ sanamu zenye kuchukiza,* na vitu vyote vyenye kuchukiza vilivyokuwa katika nchi ya Yuda na Yerusalemu, ili atekeleze maneno ya Sheria+ yaliyoandikwa katika kitabu ambacho kuhani Hilkia alipata katika nyumba ya Yehova.+ 25  Kabla ya Yosia hakukuwa na mfalme yeyote aliyekuwa kama yeye, ambaye alimrudia Yehova kwa moyo wake wote na kwa nafsi yake yote+ na kwa nguvu zake zote, kulingana na Sheria yote ya Musa, na baada yake hakutokea yeyote aliyekuwa kama yeye. 26  Hata hivyo, Yehova hakuacha hasira yake kali iliyowaka dhidi ya Yuda kwa sababu ya mambo yote yenye kuchukiza ambayo Manase alifanya na kumkasirisha Mungu.+ 27  Yehova akasema: “Nitaliondoa Yuda pia mbele za macho yangu,+ kama nilivyoliondoa Israeli;+ nami nitalikataa jiji hili nililochagua, Yerusalemu, na nyumba ambayo nilisema hivi kuihusu: ‘Jina langu litaendelea kukaa humo.’”+ 28  Na mambo mengine katika historia ya Yosia, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 29  Katika siku zake Farao Neko mfalme wa Misri alikuja kukutana na mfalme wa Ashuru karibu na Mto Efrati, kisha Mfalme Yosia akaenda kukabiliana naye; lakini Neko alipomwona, alimuua huko Megido.+ 30  Basi watumishi wake wakasafirisha maiti yake katika gari la vita kutoka Megido, wakamleta Yerusalemu na kumzika katika kaburi lake. Kisha watu nchini wakamchukua Yehoahazi mwana wa Yosia wakamtia mafuta na kumweka kuwa mfalme baada ya baba yake.+ 31  Yehoahazi+ alikuwa na umri wa miaka 23 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miezi mitatu huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Hamutali+ binti ya Yeremia kutoka Libna. 32  Yehoahazi alianza kutenda maovu machoni pa Yehova, alitenda mambo yote ambayo mababu zake walitenda.+ 33  Farao Neko+ alimtia gerezani kule Ribla+ katika nchi ya Hamathi, ili kumzuia asitawale Yerusalemu, kisha akaitoza nchi faini ya talanta 100 za fedha* na talanta moja ya dhahabu.+ 34  Isitoshe, Farao Neko alimweka Eliakimu mwana wa Yosia kuwa mfalme baada ya Yosia baba yake na kubadili jina lake kuwa Yehoyakimu; lakini akamchukua Yehoahazi na kumpeleka Misri,+ ambako alifia hatimaye.+ 35  Yehoyakimu alimpa Farao fedha na dhahabu, lakini alilazimika kuitoza nchi kodi ili ampe Farao fedha alizodai. Alimtoza kila mtu nchini kiasi kilichokadiriwa cha fedha na dhahabu cha kumpa Farao Neko. 36  Yehoyakimu+ alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 11 huko Yerusalemu.+ Mama yake aliitwa Zebida binti ya Pedaya kutoka Ruma. 37  Yehoyakimu aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova,+ alitenda mambo yote ambayo mababu zake walitenda.+

Maelezo ya Chini

Au “kufanya upya lile agano.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi, “Gehena.”
Tnn., “asimpitishe.”
Tnn., “wamewatoa.”
Au “chumba cha kulia chakula.”
Tnn., “kulia.” Yaani, kusini, mtu anapotazama mashariki.
Yaani, Mlima wa Mizeituni, hasa upande wa kusini ulio mbali zaidi unaojulikana pia kama Mlima wa Kosa.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “miungu ya familia; sanamu.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.