Kitabu cha Pili cha Wafalme 25:1-30

  • Nebukadneza azingira Yerusalemu (1-7)

  • Jiji la Yerusalemu laharibiwa pamoja na hekalu lake; uhamisho wa pili (8-21)

  • Gedalia awekwa kuwa gavana (22-24)

  • Gedalia auawa; watu wakimbilia Misri (25, 26)

  • Yehoyakini aachiliwa huru Babiloni (27-30)

25  Katika mwaka wa tisa wa utawala wa Sedekia, katika mwezi wa kumi, siku ya kumi ya mwezi huo, Mfalme Nebukadneza+ wa Babiloni alikuja na jeshi lake lote kushambulia Yerusalemu.+ Akapiga kambi na kujenga ukuta kulizingira jiji hilo pande zote,+  naye akalizingira jiji hilo mpaka mwaka wa 11 wa utawala wa Mfalme Sedekia.  Katika siku ya tisa ya mwezi wa nne njaa ilikuwa kali sana+ jijini, na watu waliokuwemo hawakuwa na chakula.+  Sehemu ya ukuta wa jiji ilibomolewa,+ na wanajeshi wote wakakimbia wakati wa usiku kupitia lango lililokuwa kati ya kuta mbili karibu na bustani ya mfalme, wakati Wakaldayo walipokuwa wakilizingira jiji; naye mfalme akafuata njia inayoelekea Araba.+  Lakini jeshi la Wakaldayo likamfuatia mfalme, nalo likamfikia katika jangwa tambarare la Yeriko, na wanajeshi wake wote wakatawanyika na kumwacha.  Kisha wakamkamata mfalme+ na kumpeleka mpaka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla, nao wakamhukumu.  Wakawachinja wana wa Sedekia huku akitazama; kisha Nebukadneza akampofusha macho Sedekia, akamfunga kwa pingu za shaba, na kumpeleka Babiloni.+  Katika mwezi wa tano, siku ya saba ya mwezi huo, yaani, mwaka wa 19 wa utawala wa Mfalme Nebukadneza wa Babiloni, Nebuzaradani+ mkuu wa walinzi, mtumishi wa mfalme wa Babiloni, alikuja Yerusalemu.+  Akateketeza kabisa nyumba ya Yehova,+ nyumba ya mfalme,*+ na nyumba zote Yerusalemu;+ aliteketeza pia nyumba ya kila mtu maarufu.+ 10  Na jeshi lote la Wakaldayo lililokuwa pamoja na mkuu wa walinzi lilibomoa kuta zilizozunguka Yerusalemu.+ 11  Nebuzaradani mkuu wa walinzi aliwapeleka uhamishoni watu wote waliobaki jijini, watu waliojisalimisha kwa mfalme wa Babiloni, na watu wengine.+ 12  Lakini mkuu wa walinzi aliwaacha baadhi ya watu maskini kabisa nchini ili watunze mashamba ya mizabibu na kufanya kazi za kulazimishwa.+ 13  Pia Wakaldayo walivunja vipandevipande nguzo za shaba+ za nyumba ya Yehova na magari+ na Bahari ya shaba,+ vitu vilivyokuwa katika nyumba ya Yehova, nao wakaipeleka shaba hiyo Babiloni.+ 14  Walichukua pia ndoo za kuondolea majivu, sepetu, mikasi ya kukatia tambi za taa, vikombe, na vyombo vyote vya shaba vilivyotumiwa katika utumishi wa hekaluni. 15  Mkuu wa walinzi alichukua vyetezo na mabakuli yaliyotengenezwa kwa dhahabu+ na fedha halisi.+ 16  Shaba yote iliyotumiwa kutengeneza zile nguzo mbili, ile Bahari, na yale magari ambayo Sulemani alitengeneza kwa ajili ya nyumba ya Yehova, haingeweza kupimwa uzito.+ 17  Kila nguzo ilikuwa na urefu wa mikono 18,*+ na kifuniko chake kilikuwa cha shaba; na urefu wa kifuniko hicho ulikuwa mikono mitatu, na wavu pamoja na makomamanga yote yaliyozunguka kifuniko yalitengenezwa kwa shaba.+ Nguzo ya pili pamoja na wavu wake ilifanana na ya kwanza. 18  Mkuu wa walinzi alimchukua pia kuhani mkuu Seraya,+ Sefania+ kuhani wa pili, na walinzi watatu wa milango.+ 19  Pia alimchukua kutoka jijini ofisa mmoja wa makao ya mfalme aliyekuwa msimamizi wa wanajeshi, watu watano waliopatikana jijini walioshirikiana kwa ukaribu na mfalme, na pia mwandishi wa mkuu wa jeshi, aliyewaandikisha watu jeshini, na wanaume 60 kutoka miongoni mwa watu wa kawaida waliokuwa bado jijini. 20  Nebuzaradani+ mkuu wa walinzi aliwachukua na kuwapeleka kwa mfalme wa Babiloni kule Ribla.+ 21  Mfalme wa Babiloni aliwaua na kuwaangamiza huko Ribla katika nchi ya Hamathi.+ Hivyo watu wa Yuda wakaenda uhamishoni kutoka katika nchi yao.+ 22  Mfalme Nebukadneza wa Babiloni akamchagua Gedalia+ mwana wa Ahikamu+ mwana wa Shafani+ awasimamie watu aliowaacha katika nchi ya Yuda.+ 23  Wakuu wote wa jeshi na wanajeshi wao waliposikia kwamba mfalme wa Babiloni amemchagua Gedalia, mara moja wakaenda kwa Gedalia huko Mispa. Wakuu hao ni Ishmaeli mwana wa Nethania, Yohanani mwana wa Karea, Seraya mwana wa Tanhumethi Mnetofa, na Yaazania mwana wa Mmaakathi, pamoja na wanajeshi wao.+ 24  Gedalia akawaapia hivi pamoja na wanajeshi wao: “Msiogope kuwa watumishi wa Wakaldayo. Kaeni katika nchi hii na kumtumikia mfalme wa Babiloni, na mambo yatawaendea vyema.”+ 25  Na katika mwezi wa saba, Ishmaeli+ mwana wa Nethania mwana wa Elishama, aliyekuwa wa uzao wa kifalme,* akaja na wanaume wengine kumi, nao wakampiga na kumuua Gedalia pamoja na Wayahudi na Wakaldayo waliokuwa pamoja naye huko Mispa.+ 26  Kisha watu wote, kuanzia mdogo mpaka mkubwa, pamoja na wakuu wa jeshi, wakaondoka na kwenda Misri,+ kwa sababu waliwaogopa Wakaldayo.+ 27  Na katika mwaka wa 37 tangu Mfalme Yehoyakini+ wa Yuda alipopelekwa uhamishoni, katika mwezi wa 12, siku ya 27 ya mwezi huo, Mfalme Evil-merodaki wa Babiloni, katika mwaka alioanza kutawala, alimwachilia huru Mfalme Yehoyakini wa Yuda kutoka gerezani.+ 28  Alizungumza naye kwa fadhili na kukikweza kiti chake cha ufalme juu zaidi kuliko viti vya wafalme wengine waliokuwa pamoja naye Babiloni. 29  Basi Yehoyakini akavua mavazi yake ya gerezani, na sikuzote za maisha yake alikuwa akila kwenye meza ya mfalme. 30  Naye alipewa chakula kwa ukawaida kutoka kwa mfalme, siku baada ya siku, siku zote za maisha yake.

Maelezo ya Chini

Au “jumba la mfalme.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “mbegu ya ufalme.”