Kitabu cha Pili cha Wafalme 3:1-27

  • Yehoramu, mfalme wa Israeli (1-3)

  • Wamoabu wawaasi Waisraeli (4-25)

  • Wamoabu washindwa (26, 27)

3  Yehoramu+ mwana wa Ahabu akawa mfalme wa Israeli kule Samaria katika mwaka wa 18 wa utawala wa Mfalme Yehoshafati wa Yuda, naye alitawala kwa miaka 12.  Akaendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, lakini si kwa kadiri aliyotenda baba yake au mama yake, kwa maana aliondoa nguzo takatifu ya Baali ambayo baba yake alikuwa ametengeneza.+  Hata hivyo, alishikamana na dhambi ambazo Yeroboamu mwana wa Nebati alikuwa amesababisha Waisraeli watende.+ Hakuziacha.  Mesha mfalme wa Moabu alikuwa mfugaji wa kondoo, naye alikuwa akilipa wanakondoo 100,000 na kondoo dume 100,000 ambao hawajakatwa manyoya kama ushuru kwa mfalme wa Israeli.  Mara tu Ahabu alipokufa,+ mfalme wa Moabu akamwasi mfalme wa Israeli.+  Basi Mfalme Yehoramu akaondoka Samaria siku hiyo na kuwakusanya Waisraeli wote.  Akamtumia pia ujumbe Mfalme Yehoshafati wa Yuda, akisema: “Mfalme wa Moabu ameniasi. Je, utaenda pamoja nami kupigana vita dhidi ya Moabu?” Akasema: “Nitaenda.+ Mimi ni kama wewe. Watu wangu ni kama watu wako. Farasi wangu ni kama farasi wako.”+  Kisha akamuuliza: “Tupande kupitia njia gani?” Akajibu: “Kupitia njia ya nyika ya Edomu.”  Basi mfalme wa Israeli akaondoka pamoja na mfalme wa Yuda na mfalme wa Edomu.+ Baada ya kuzunguka kwa siku saba, jeshi na wanyama wa kufugwa waliokuwa wakiwafuata hawakuwa na maji. 10  Mfalme wa Israeli akasema: “Inasikitisha sana! Yehova ametuita sisi wafalme watatu ili tu atutie mikononi mwa Moabu!” 11  Ndipo Yehoshafati akauliza: “Je, hakuna nabii wa Yehova mahali hapa ambaye tunaweza kumwomba ushauri kutoka kwa Yehova?+ Basi mmoja wa watumishi wa mfalme wa Israeli akajibu: “Yupo Elisha+ mwana wa Shafati, aliyekuwa akimmiminia Eliya maji mikononi.”*+ 12  Kisha Yehoshafati akasema: “Neno la Yehova liko pamoja naye.” Basi mfalme wa Israeli na pia Yehoshafati na mfalme wa Edomu wakashuka kwenda kumwona. 13  Elisha akamwambia mfalme wa Israeli: “Kwa nini umekuja kuniona?*+ Nenda kwa manabii wa baba yako na kwa manabii wa mama yako.”+ Lakini mfalme wa Israeli akamwambia: “Sitaenda, kwa maana ni Yehova aliyetuita sisi wafalme watatu ili atutie mikononi mwa Moabu.” 14  Elisha akamwambia: “Kwa hakika kama anavyoishi Yehova wa majeshi ambaye ninamtumikia,* kama singekuwa ninamheshimu Mfalme Yehoshafati+ wa Yuda, singekutazama wala kukutilia maanani.+ 15  Sasa niletee mpiga kinubi.”*+ Mara tu mpiga kinubi huyo alipoanza kupiga kinubi, mkono wa Yehova ukaja juu ya Elisha.+ 16  Akasema, “Yehova anasema hivi: ‘Chimbeni mitaro katika bonde* hili, 17  kwa maana Yehova anasema hivi: “Hamtaona upepo, wala hamtaona mvua; hata hivyo bonde* hili litajaa maji,+ nanyi mtakunywa maji yake, ninyi, ng’ombe wenu, na wanyama wenu wengine.”’ 18  Lakini hili ni jambo dogo sana machoni pa Yehova,+ kwa maana ataitia pia Moabu mikononi mwenu.+ 19  Mnapaswa kuangamiza kila jiji lenye ngome+ na kila jiji bora, mnapaswa kuukata kila mti mzuri, mnapaswa kuziba chemchemi zote za maji, nanyi mnapaswa kuharibu kila shamba zuri kwa kutupa mawe humo.”+ 20  Na asubuhi, wakati ambapo toleo la nafaka la asubuhi hutolewa,+ maji yakaanza kuja kwa ghafla kutoka upande wa Edomu, na nchi ikajaa maji. 21  Wamoabu wote wakasikia kwamba wafalme hao walikuwa wamekuja kupigana nao, basi wakawakusanya pamoja wanaume wote walioweza kubeba silaha,* nao wakasimama mpakani. 22  Walipoamka asubuhi na mapema, jua lilikuwa likiangaza juu ya maji, na Wamoabu waliokuwa upande wa pili waliona maji yakiwa mekundu kama damu. 23  Wakasema: “Hii ni damu! Hakika wafalme wamechinjana wenyewe kwa upanga. Haya basi, enyi Wamoabu, twendeni tukachukue nyara!”+ 24  Walipoingia katika kambi ya Israeli, Waisraeli wakatoka na kuanza kuwaua Wamoabu, nao wakawakimbia.+ Waisraeli wakazidi kuingia Moabu, wakawaua Wamoabu kadiri walivyosonga. 25  Wakabomoa majiji, na kila mtu akatupa jiwe katika kila shamba zuri, na kulijaza mawe; wakaziba kila chemchemi ya maji+ na kuukata kila mti mzuri.+ Mwishowe ni kuta za mawe za jiji la Kir-haresethi+ pekee zilizobaki, na watu wenye makombeo wakalizunguka na kuliangamiza. 26  Mfalme wa Moabu alipoona kwamba ameshindwa vitani, akachukua wanaume 700 waliojihami kwa mapanga ili wapenye na kuingia kwa mfalme wa Edomu;+ lakini hawakuweza. 27  Basi akamchukua mwana wake mzaliwa wa kwanza ambaye angetawala baada yake akamtoa kuwa dhabihu ya kuteketezwa+ juu ya ukuta. Wamoabu wakawa na ghadhabu kali dhidi ya Waisraeli, kwa hiyo Waisraeli wakaacha kumshambulia mfalme huyo na kurudi katika nchi yao.

Maelezo ya Chini

Au “aliyekuwa mtumishi wa Eliya.”
Tnn., “Kuna nini kati yangu nawe?”
Tnn., “ambaye ninasimama mbele zake.”
Au “mwanamuziki.”
Au “korongo.”
Au “korongo.”
Au “wote waliojifunga mshipi.”