Kitabu cha Pili cha Wafalme 5:1-27

  • Elisha amponya Naamani ukoma (1-19)

  • Gehazi mwenye pupa apigwa na ukoma (20-27)

5  Sasa Naamani, mkuu wa jeshi la mfalme wa Siria, alikuwa mtu maarufu aliyeheshimiwa na bwana wake, kwa sababu Yehova alikuwa amewapa Wasiria ushindi* kupitia yeye. Alikuwa shujaa hodari, ingawa alikuwa na ukoma.*  Pindi moja Wasiria walipovamia Israeli, walimchukua mateka msichana mdogo kutoka katika nchi ya Israeli, akawa kijakazi wa mke wa Naamani.  Msichana huyo alimwambia hivi bimkubwa wake: “Laiti bwana wangu angemtembelea nabii+ aliye kule Samaria! Angemponya ukoma wake.”+  Basi akaenda* na kumwambia bwana wake mambo aliyosema msichana huyo kutoka Israeli.  Kisha mfalme wa Siria akasema: “Nenda sasa! Nami nitamtumia barua mfalme wa Israeli.” Basi akaenda, akaondoka akiwa amebeba talanta kumi* za fedha, vipande 6,000 vya dhahabu, na mavazi kumi.  Akampelekea mfalme wa Israeli barua hiyo ambayo ilisema hivi: “Pamoja na barua hii, ninamtuma mtumishi wangu Naamani ili umponye ukoma wake.”  Mara tu mfalme wa Israeli aliposoma barua hiyo, aliyararua mavazi yake na kusema: “Je, mimi ni Mungu, ninaweza kuua na kumfanya mtu aendelee kuwa hai?+ Kwa maana anamtuma mtu huyu kwangu na kuniambia nimponye ukoma wake! Mnaona wenyewe kwamba anatafuta ugomvi nami.”  Lakini Elisha mtu wa Mungu wa kweli aliposikia kwamba mfalme wa Israeli ameyararua mavazi yake, mara moja akamtumia mfalme ujumbe huu: “Kwa nini uliyararua mavazi yako? Tafadhali, mruhusu aje kwangu ili ajue kwamba kuna nabii katika Israeli.”+  Basi Naamani akaja na farasi wake na magari yake ya vita, akasimama katika mlango wa nyumba ya Elisha. 10  Hata hivyo, Elisha akamtuma mjumbe amwambie: “Nenda ukaoge mara saba+ katika Mto Yordani,+ na mwili wako utaponywa, nawe utakuwa safi.” 11  Ndipo Naamani akakasirika, akaanza kuondoka akisema: “Nilisema moyoni mwangu, ‘Atatoka na kunijia na kusimama hapa na kuliita jina la Yehova Mungu wake, akitikisa mkono wake kwenda mbele na nyuma juu ya ukoma ili auponye.’ 12  Je, Abana na Farpari, mito ya Damasko,+ si bora kuliko maji yote ya Israeli? Je, siwezi kuoga humo na kuwa safi?” Ndipo akageuka na kwenda zake kwa hasira kali. 13  Basi watumishi wake wakamkaribia na kumwambia: “Baba yangu, kama nabii huyo angekwambia ufanye jambo fulani lisilo la kawaida, je, hungefanya? Je, wakati huu hupaswi kufanya zaidi, kwa kuwa amekuambia tu, ‘Oga, uwe safi’?” 14  Ndipo akashuka mtoni na kujitumbukiza* mara saba katika Mto Yordani, kama alivyosema mtu wa Mungu wa kweli.+ Kisha mwili wake ukaponywa ukawa kama mwili wa mvulana mdogo,+ akawa safi.+ 15  Kisha akarudi kwa yule mtu wa Mungu wa kweli,+ yeye na msafara wake wote,* akasimama mbele yake na kusema: “Sasa najua kwamba hakuna Mungu mahali pengine popote duniani isipokuwa Israeli.+ Sasa, tafadhali, pokea zawadi* kutoka kwangu mimi mtumishi wako.” 16  Hata hivyo, Elisha akasema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi ambaye ninamtumikia,* sitaipokea.”+ Akamsihi sana aipokee, lakini akazidi kukataa. 17  Hatimaye Naamani akasema: “Ikiwa hutaipokea, tafadhali, mimi mtumishi wako ninaomba udongo wa nchi hii, kiasi kinachoweza kubebwa na nyumbu wawili, kwa sababu mimi mtumishi wako sitaendelea kutoa dhabihu ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine yoyote isipokuwa kwa Yehova. 18  Lakini Yehova anisamehe mimi mtumishi wako kwa jambo hili moja: Bwana wangu anapoingia katika nyumba ya* Rimoni ili kusujudu humo, yeye huegemea mkono wangu, kwa hiyo ninalazimika kusujudu katika nyumba ya Rimoni. Nitakapokuwa nikisujudu katika nyumba ya Rimoni, tafadhali, naomba Yehova anisamehe mimi mtumishi wako kwa kufanya jambo hilo.” 19  Basi Elisha akamwambia: “Nenda kwa amani.” Baada ya kuondoka na kusafiri umbali fulani, 20  Gehazi+ mtumishi wa Elisha mtu wa Mungu wa kweli+ akasema moyoni mwake: ‘Tazama, Bwana wangu amemwacha huyu Naamani Msiria+ aende zake kwa kukataa kupokea vitu alivyoleta. Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, nitakimbia na kumfuata, nichukue kitu fulani kutoka kwake.’ 21  Kwa hiyo Gehazi akamfuata mbio Naamani. Naamani alipoona mtu fulani akimfuata mbio, akashuka kutoka kwenye gari lake na kwenda kumpokea, akamuuliza: “Je, mambo yote yako sawa?” 22  Akasema: “Mambo yote yako sawa. Bwana wangu amenituma nikwambie, ‘Tazama! Sasa hivi vijana wawili kutoka kwa wana wa manabii wamekuja kwangu kutoka katika eneo lenye milima la Efraimu. Tafadhali, wape talanta moja ya fedha na mavazi mawili.’”+ 23  Naamani akasema: “Haya, chukua talanta mbili.” Naye akamsihi sana azipokee,+ akafunga talanta mbili za fedha katika mifuko miwili, pamoja na mavazi mawili, akawapa watumishi wake wawili, wakambebea vitu hivyo. 24  Alipofika Ofeli,* akavichukua kutoka mikononi mwao, akaviweka nyumbani, na kuwaruhusu watu hao waende zao. Walipoondoka, 25  akaingia na kusimama karibu na bwana wake. Sasa Elisha akamuuliza: “Umetoka wapi, Gehazi?” Lakini akajibu: “Mimi mtumishi wako sikwenda mahali popote.”+ 26  Ndipo akamwambia: “Je, moyo wangu haukuwa pamoja nawe wakati yule mtu aliposhuka kutoka kwenye gari lake ili kukupokea? Je, huu ni wakati wa kupokea fedha au kupokea mavazi au mashamba ya mizeituni au mashamba ya mizabibu au kondoo au ng’ombe au watumishi wa kiume au watumishi wa kike?+ 27  Sasa ukoma wa Naamani+ utashikamana nawe pamoja na wazao wako milele.” Mara moja akaondoka mbele yake akiwa na ukoma, mweupe kama theluji.+

Maelezo ya Chini

Au “wokovu.”
Au “alikuwa na ugonjwa wa ngozi.”
Inawezekana ni Naamani.
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “kujizamisha.”
Tnn., “baraka.”
Tnn., “kambi yake yote.”
Tnn., “ninasimama mbele zake.”
Au “hekalu la.”
Eneo fulani kule Samaria, inawezekana ni kilima au ngome.