Kitabu cha Pili cha Wafalme 9:1-37

  • Yehu atiwa mafuta kuwa mfalme wa Israeli (1-13)

  • Yehu amuua Yehoramu na Ahazia (14-29)

  • Yezebeli auawa; mbwa wala maiti yake (30-37)

9  Kisha nabii Elisha akamwita mmoja wa wana wa manabii na kumwambia: “Jifunge mavazi yako kiunoni, na uchukue haraka chupa hii ya mafuta uende Ramothi-gileadi.+  Utakapofika huko, mtafute Yehu+ mwana wa Yehoshafati mwana wa Nimshi; ingia ndani, umchukue kutoka miongoni mwa ndugu zake, na kumpeleka katika chumba cha ndani zaidi.  Kisha chukua chupa ya mafuta, uyamimine juu ya kichwa chake na kusema, ‘Yehova anasema hivi: “Ninakutia mafuta uwe mfalme wa Israeli.”’+ Halafu ufungue mlango na kukimbia bila kukawia.”  Basi yule mtumishi wa nabii akaenda Ramothi-gileadi.  Alipofika, aliwakuta wakuu wa majeshi wakiwa wameketi pamoja. Akasema: “Nina ujumbe wako, ewe mkuu.” Yehu akamuuliza: “Ni ujumbe wa nani kati yetu?” Akasema: “Ujumbe wako, ewe mkuu.”  Basi Yehu akainuka na kuingia ndani ya nyumba; mtumishi huyo akammiminia yale mafuta juu ya kichwa na kumwambia, “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Ninakutia mafuta uwe mfalme wa watu wa Yehova, uwe mfalme wa Israeli.+  Unapaswa kuiangamiza nyumba ya Ahabu bwana wako, nami nitailipizia kisasi damu ya watumishi wangu manabii na watumishi wote wa Yehova ambao Yezebeli aliwaua.*+  Na nyumba yote ya Ahabu itaangamia; nami nitamwangamiza kila mwanamume* wa Ahabu, kutia ndani wasio na uwezo na walio dhaifu katika Israeli.+  Nami nitaifanya nyumba ya Ahabu kuwa kama nyumba ya Yeroboamu+ mwana wa Nebati na kama nyumba ya Baasha+ mwana wa Ahiya. 10  Kuhusu Yezebeli, mbwa watamla katika shamba kule Yezreeli,+ na hakuna yeyote atakayemzika.’” Kisha mtumishi huyo akafungua mlango na kukimbia.+ 11  Yehu aliporudi kwa watumishi wa bwana wake, wakamuuliza: “Je, mambo yote yako sawa? Kwa nini mwendawazimu huyu alikuja kwako?” Akawajibu: “Ninyi mnajua huyu ni mtu wa aina gani na mambo anayosema.” 12  Lakini wakasema: “Hilo si kweli! Tafadhali tuambie.” Ndipo akasema: “Aliniambia hivi, halafu akasema, ‘Yehova anasema hivi: “Ninakutia mafuta uwe mfalme wa Israeli.”’”+ 13  Ndipo kila mmoja wao akavua vazi lake haraka na kulitandika chini ya Yehu kwenye ngazi zilizo wazi,+ nao wakapiga pembe na kusema: “Yehu amekuwa mfalme!”+ 14  Kisha Yehu+ mwana wa Yehoshafati mwana wa Nimshi akapanga njama dhidi ya Yehoramu. Yehoramu alikuwa akilinda huko Ramothi-gileadi,+ yeye na Waisraeli wote, kwa sababu ya Mfalme Hazaeli+ wa Siria. 15  Baadaye Mfalme Yehoramu akarudi Yezreeli+ ili kuuguza majeraha aliyokuwa amepata kutoka kwa Wasiria alipopigana na Mfalme Hazaeli wa Siria.+ Sasa Yehu akasema: “Mkikubaliana nami, msimwache yeyote atoroke kutoka jijini na kupeleka habari hii Yezreeli.” 16  Kisha Yehu akapanda gari lake na kwenda Yezreeli, kwa maana Yehoramu alikuwa amelala huko akiwa amejeruhiwa, na Mfalme Ahazia wa Yuda alikuwa ameshuka kwenda kumwona Yehoramu. 17  Mlinzi aliyekuwa amesimama juu ya mnara huko Yezreeli aliona kundi kubwa la wanaume wa Yehu likija. Mara moja akasema: “Ninaona kundi kubwa la wanaume.” Yehoramu akasema: “Chukua mpanda farasi mmoja umtume akutane nao, awaulize, ‘Je, mmekuja kwa amani?’” 18  Basi mpanda farasi akaenda kukutana naye, akasema: “Mfalme anauliza, ‘Je, mmekuja kwa amani?’” Lakini Yehu akasema: “Kwa nini unauliza kuhusu ‘amani’? Nifuate!” Basi yule mlinzi akasema: “Mjumbe aliwafikia, lakini hajarudi.” 19  Kwa hiyo akatuma mpanda farasi wa pili, akawaambia hivi alipowafikia: “Mfalme anauliza hivi: ‘Je, mmekuja kwa amani?’” Lakini Yehu akasema: “Kwa nini unauliza kuhusu ‘amani’? Nifuate!” 20  Basi yule mlinzi akasema: “Aliwafikia, lakini hajarudi, na uendeshaji wa gari ni kama wa Yehu mjukuu* wa Nimshi, kwa maana yeye huendesha gari kama mwendawazimu.” 21  Yehoramu akasema: “Fungeni farasi kwenye gari!” Basi farasi wakafungwa kwenye gari lake la vita, na Yehoramu mfalme wa Israeli na Ahazia+ mfalme wa Yuda wakaondoka kila mmoja kwenye gari lake la vita ili kukutana na Yehu. Wakakutana naye katika shamba la Nabothi,+ Myezreeli. 22  Mara tu Yehoramu alipomwona Yehu, akamuuliza: “Yehu, umekuja kwa amani?” Lakini akamjibu: “Kunawezaje kuwa na amani wakati kuna ukahaba wa Yezebeli+ mama yako na ulozi wake mwingi?”+ 23  Mara moja Yehoramu akageuza gari lake ili akimbie, akamwambia Ahazia: “Tumedanganywa, Ahazia!” 24  Yehu akachukua upinde wake na kumpiga mshale Yehoramu katikati ya mabega, na mshale huo ukatokea moyoni mwake, naye akaanguka ndani ya gari lake la vita. 25  Kisha akamwambia Bidkari kamanda wake msaidizi: “Mwinue na umtupe katika shamba la Nabothi, Myezreeli.+ Kumbuka kwamba mimi na wewe tulipokuwa tukiendesha magari ya farasi* tukimfuata Ahabu baba yake, Yehova mwenyewe alitangaza hivi dhidi yake:+ 26  ‘“Kwa hakika kama nilivyoona damu ya Nabothi+ na damu ya wanawe jana,” asema Yehova, “nitakulipa+ wewe katika shamba hilihili,” asema Yehova.’ Basi sasa mwinue na umtupe katika shamba hili, kulingana na neno la Yehova.”+ 27  Mfalme Ahazia wa Yuda+ alipoona hayo, alikimbia kupitia njia ya nyumba ya bustani. (Baadaye Yehu akamfuatia na kusema: “Muueni yeye pia!” Kwa hiyo wakampiga ndani ya gari akipanda kuelekea Guri, karibu na mji wa Ibleamu.+ Lakini akaendelea kukimbia mpaka Megido, akafia huko. 28  Kisha watumishi wake wakambeba ndani ya gari mpaka Yerusalemu, wakamzika katika kaburi lake pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ 29  Mfalme Ahazia alianza kutawala Yuda katika mwaka wa 11 wa utawala wa Yehoramu mwana wa Ahabu.)+ 30  Yehu alipofika Yezreeli,+ Yezebeli+ akasikia habari hizo. Basi akapaka macho yake wanja na kupamba nywele zake, akatazama chini kupitia dirishani. 31  Yehu alipokuwa akiingia langoni, Yezebeli akasema: “Je, mambo yalimwendea sawa Zimri, aliyemuua bwana wake?”+ 32  Yehu akatazama juu dirishani na kuuliza: “Ni nani aliye upande wangu? Ni nani?”+ Mara moja maofisa wawili au watatu wa makao ya mfalme wakamtazama wakiwa dirishani. 33  Yehu akasema: “Mtupeni chini mwanamke huyo!” Kwa hiyo wakamtupa chini, na kiasi fulani cha damu yake kikatapakaa kwenye ukuta na farasi, kisha Yehu akamkanyaga-kanyaga. 34  Baada ya hayo akaingia ndani, akala na kunywa. Halafu akasema: “Tafadhali, mchukueni mwanamke huyu aliyelaaniwa mkamzike. Kwa maana yeye ni binti ya mfalme.”+ 35  Lakini walipoenda kumzika, hawakupata chochote isipokuwa fuvu la kichwa na miguu na viganja vya mikono.+ 36  Waliporudi na kumwambia Yehu, akasema: “Jambo hilo linatimiza neno hili la Yehova+ alilosema kupitia mtumishi wake Eliya, Mtishbi: ‘Katika shamba la Yezreeli, mbwa wataula mwili wa Yezebeli.+ 37  Na maiti ya Yezebeli itakuwa kama mbolea katika shamba la Yezreeli, ili watu wasiseme: “Huyu ni Yezebeli.”’”

Maelezo ya Chini

Tnn., “waliofia mikononi mwa Yezebeli.”
Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.
Tnn., “mwana.”
Tnn., “makundi ya magari ya farasi.”