Barua ya Pili kwa Wakorintho 1:1-24

  • Salamu (1, 2)

  • Faraja kutoka kwa Mungu katika dhiki zote (3-11)

  • Mabadiliko katika mipango ya safari za Paulo (12-24)

1  Paulo, mtume wa Kristo Yesu kupitia mapenzi ya Mungu, na Timotheo+ ndugu yetu, kwa kutaniko la Mungu lililo huko Korintho, pamoja na watakatifu wote walio katika Akaya yote:+  Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.  Asifiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo,+ Baba wa rehema nyororo+ na Mungu wa faraja yote,+  ambaye hutufariji* katika majaribu*+ yetu yote, ili tuweze kuwafariji wengine+ walio katika majaribu* ya namna yoyote, kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.+  Kwa maana kama vile mateso kwa ajili ya Kristo yalivyo mengi ndani yetu,+ ndivyo pia faraja tunayopokea kupitia Kristo ilivyo nyingi.  Basi tukikabili majaribu,* ni kwa ajili ya faraja na wokovu wenu; na tukifarijiwa, ni kwa ajili ya faraja yenu inayotenda ili kuwasaidia mvumilie mateso yaleyale ambayo sisi pia tunateseka.  Na tumaini letu kwa ajili yenu haliyumbi-yumbi, kwa kuwa tunajua kwamba kama vile mnavyoshiriki katika mateso, ndivyo pia mtakavyoshiriki katika faraja.+  Kwa maana hatutaki mkose kujua, akina ndugu, kuhusu dhiki tuliyopata katika mkoa wa Asia.+ Tulikuwa na mkazo mkubwa sana unaozidi nguvu zetu wenyewe, hivi kwamba hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu.+  Kwa kweli, tulihisi kwamba tumepokea hukumu ya kifo. Ilikuwa hivyo ili tusijitegemee sisi wenyewe, bali tumtegemee Mungu+ ambaye huwafufua wafu. 10  Alituokoa kutoka katika hatari kubwa ya kifo na atatuokoa, nasi tumeweka tumaini letu kwake kwamba ataendelea kutuokoa.+ 11  Ninyi pia mnaweza kutusaidia kwa kutoa dua kwa ajili yetu,+ ili wengi watoe shukrani kwa ajili yetu kwa kibali tunachopokea kwa sababu ya majibu ya sala za wengi.*+ 12  Kwa maana hili ndilo jambo tunalojisifia, dhamiri yetu inatoa ushahidi kwamba tumejiendesha katika ulimwengu, na hasa kuwaelekea ninyi, kwa utakatifu na unyoofu unaotoka kwa Mungu, si kwa hekima ya kimwili,+ bali kwa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. 13  Kwa maana kwa kweli hatuwaandikii jambo lolote isipokuwa yale mnayoweza kusoma* na kuyaelewa, nami natumaini mtaendelea kuyaelewa mambo haya kikamili,* 14  kama vile ambavyo pia mmeelewa kwa kadiri fulani, kwamba sisi ni sababu yenu ya kujisifu, kama vile mtakavyokuwa kwetu pia katika siku ya Bwana wetu Yesu. 15  Basi nikiwa na uhakika huu, nilikusudia kuja kwenu kwanza, ili muwe na pindi ya pili ya kuwa na shangwe;* 16  kwa maana nilikusudia kuwatembelea nikiwa safarini kwenda Makedonia, nirudi kwenu baada ya kutoka Makedonia, kisha mnisindikize kwenda Yudea.+ 17  Basi, nilipokusudia hivyo, je, nilipuuza jambo hilo? Au je, mimi ninakusudia mambo kwa njia ya kimwili hivi kwamba ninasema “Ndiyo, ndiyo” na kisha “Siyo, siyo”? 18  Lakini Mungu anaweza kutegemewa ili kwamba yale tunayowaambia yasiwe “ndiyo” na wakati uleule “siyo.” 19  Kwa maana Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliyehubiriwa miongoni mwenu kupitia sisi, yaani, kupitia mimi na Silvano* na Timotheo,+ hakuwa “ndiyo” na wakati uleule “siyo,” bali kuhusiana naye “ndiyo” imekuwa “ndiyo.” 20  Kwa maana hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa “ndiyo” kupitia yeye.+ Kwa hiyo, kupitia yeye pia “Amina” husemwa kwa Mungu,+ nayo humletea utukufu kupitia sisi. 21  Lakini yule anayetoa uhakikisho kwamba ninyi na sisi ni wa Kristo na yule ambaye ametutia mafuta ni Mungu.+ 22  Yeye pia ametia muhuri wake juu yetu+ naye ametupatia rehani ya kile kitakachokuja,* yaani, roho,+ katika mioyo yetu. 23  Sasa ninamwita Mungu awe shahidi dhidi yangu,* kwamba sijaja Korintho kwa sababu ya kuwahurumia ninyi. 24  Si kwamba sisi ni mabwana wa imani yenu,+ bali sisi ni wafanyakazi wenzenu kwa ajili ya shangwe yenu, kwa maana mnasimama kwa imani yenu.

Maelezo ya Chini

Au “dhiki.”
Au “dhiki.”
Au “hututia moyo.”
Au “dhiki.”
Au “kwa sababu ya nyuso nyingi zinazosali.”
Au labda, “yale ambayo tayari mnayajua vizuri.”
Tnn., “mpaka mwisho.”
Au labda, “ili mnufaike mara mbili.”
Pia anaitwa Sila.
Au “malipo ya awali; uthibitisho (dhamana) wa kile kitakachokuja.”
Au “dhidi ya nafsi yangu.”