Barua ya Pili kwa Wakorintho 11:1-33

  • Paulo na mitume walio bora sana (1-15)

  • Hali ngumu alizokabili Paulo akiwa mtume (16-33)

11  Laiti mngenivumilia katika kukosa kidogo akili. Lakini kwa kweli, mnanivumilia!  Kwa maana nina wivu juu yenu, wivu wa kimungu,* kwa kuwa mimi binafsi niliwachumbia mume mmoja ili niwatoe mkiwa bikira safi* kwa Kristo.+  Lakini kwa njia fulani, ninaogopa kwamba kama nyoka alivyomshawishi Hawa kwa ujanja,+ huenda akili zenu zikapotoshwa kutoka kwenye unyoofu wa moyo na usafi* unaomfaa Kristo.+  Kwa maana, kama ilivyo, mtu akija na kuhubiri Yesu mwingine tofauti na yule tuliyemhubiri, au mkipokea roho nyingine tofauti na ile mliyopokea,+ au habari njema nyingine tofauti na ile mliyokubali, mnakubaliana naye.  Kwa maana ninaona kwamba katika jambo lolote sijawa mdogo kuliko mitume wenu walio bora sana.+  Lakini hata kama sina ustadi wa kusema,+ hakika nina ujuzi; kwa kweli tuliwafafanulia katika kila njia na katika mambo yote.  Au je, nilifanya dhambi kwa kujinyenyekeza ili ninyi mwinuliwe, kwa sababu niliwatangazia habari njema ya Mungu kwa furaha bila gharama?+  Niliyanyang’anya* makutaniko mengine kwa kupokea vitu* kutoka kwao ili niwahudumie ninyi.+  Na bado, nilipokuwa pamoja nanyi na nikapatwa na uhitaji, sikuwa mzigo kwa mtu yeyote, kwa maana ndugu waliotoka Makedonia walinipatia mahitaji yangu kwa wingi.+ Ndiyo, katika kila njia sikutaka kuwa mzigo kwenu nami nitaendelea kufanya hivyo.+ 10  Kwa hakika ikiwa kweli ya Kristo imo ndani yangu, sitaacha kujisifu+ katika maeneo ya Akaya. 11  Kwa sababu gani? Je, ni kwa sababu siwapendi? Mungu anajua ninawapenda. 12  Lakini nitaendelea kufanya kile ninachofanya,+ ili niondoe kisingizio cha wale wanaotafuta sababu ya kuonekana* kuwa sawa na sisi katika mambo ambayo* wanajisifia. 13  Kwa maana watu wa namna hiyo ni mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu, wanaojifanya kuwa mitume wa Kristo.+ 14  Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe huendelea kujifanya kuwa malaika wa nuru.+ 15  Kwa hiyo si ajabu kwamba wahudumu wake pia huendelea kujifanya kuwa wahudumu wa uadilifu. Lakini mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.+ 16  Ninasema tena: Mtu yeyote asifikiri kwamba mimi sina akili. Lakini hata mkifikiri hivyo, basi mnikubali kama mtu asiye na akili, ili mimi pia nijisifu kidogo. 17  Hili ndilo ninalosema sasa, si kwa kufuata kielelezo cha Bwana, bali kama mtu asiye na akili, kwa ujasiri wa kujisifu. 18  Kwa kuwa wengi wanajisifu kulingana na mwili,* mimi pia nitajisifu. 19  Kwa kuwa ninyi mna “akili” sana, mnakubaliana kwa furaha na watu wasio na akili. 20  Kwa kweli, mnakubaliana na yeyote anayewafanya kuwa watumwa, yeyote anayemeza mali yenu, yeyote anayenyakua kile mlicho nacho, yeyote anayejitukuza juu yenu, na yeyote anayewapiga usoni. 21  Ninasema hili kwa aibu yetu, kwa sababu huenda ikaonekana tumetenda kwa udhaifu. Lakini ikiwa wengine wanatenda kwa ujasiri—ninazungumza kama mtu asiye na akili—mimi pia ninatenda kwa ujasiri. 22  Je, wao ni Waebrania? Mimi pia.+ Je, wao ni Waisraeli? Mimi pia. Je, wao ni uzao wa* Abrahamu? Mimi pia.+ 23  Je, wao ni wahudumu wa Kristo? Ninajibu kama mwendawazimu, mimi ni mhudumu kwa njia kubwa hata zaidi: Nimefanya kazi nyingi zaidi,+ nimefungwa gerezani mara nyingi zaidi,+ nimepigwa mara nyingi sana, na kukaribia kufa mara nyingi.+ 24  Mara tano nilipigwa na Wayahudi viboko 40 kasoro kimoja,+ 25  mara tatu nilipigwa kwa fimbo,+ mara moja nilipigwa mawe,+ mara tatu nilivunjikiwa na meli,+ usiku mmoja na mchana mmoja nimekaa baharini; 26  mara nyingi katika safari, hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi, hatari za kutokana na watu wangu mwenyewe,+ hatari za kutokana na mataifa,+ hatari jijini,+ hatari nyikani, hatari baharini, hatari kati ya ndugu wa uwongo, 27  kwa kazi ngumu na yenye kutaabisha, mara nyingi kukosa usingizi usiku,+ njaa na kiu,+ kukosa chakula mara nyingi,+ na pia baridi na kukosa mavazi.* 28  Zaidi ya mambo hayo ya nje, pia kuna jambo linalonipata siku kwa siku:* kuhangaikia makutaniko yote.+ 29  Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu? Ni nani amekwazika, nami sina hasira? 30  Ikiwa ni lazima nijisifu, nitajisifu kuhusu mambo yanayoonyesha udhaifu wangu. 31  Mungu na Baba ya Bwana Yesu, Yule anayestahili kusifiwa milele, anajua sisemi uwongo. 32  Huko Damasko gavana aliye chini ya Areta mfalme alikuwa akilinda jiji la Wadamasko ili kunikamata, 33  lakini nilishushwa katika kapu kupitia dirisha kwenye ukuta wa jiji,+ nami nikaiponyoka mikono yake.

Maelezo ya Chini

Au “safi kiadili.”
Tnn., “bidii ya Mungu.”
Au “usafi wa kiadili.”
Au “msaada.”
Au “Niliyapora.”
Au “kisingizio cha.”
Au “cheo ambacho.”
Yaani, kwa maoni ya wanadamu.
Tnn., “mbegu ya.”
Tnn., “katika uchi.”
Au “kuna mambo yanayonikaza kila siku kuhusu.”