Barua ya Pili kwa Wakorintho 12:1-21

  • Maono ya Paulo (1-7a)

  • “Mwiba katika mwili” wa Paulo (7b-10)

  • Hajapungukiwa kuliko mitume walio bora sana (11-13)

  • Paulo awahangaikia Wakorintho (14-21)

12  Lazima nijisifu. Hakuna faida, lakini nitaenda kwenye maono+ ya miujiza na ufunuo wa Bwana.+  Ninamjua mtu fulani katika muungano na Kristo, ambaye miaka 14 iliyopita—kama ni katika mwili au nje ya mwili, sijui; Mungu anajua—alinyakuliwa mpaka kwenye mbingu ya tatu.  Ndiyo, ninamjua mtu kama huyo—iwe ni katika mwili au bila mwili, mimi sijui; Mungu anajua—  ambaye alinyakuliwa kuingia katika paradiso na kusikia maneno yasiyoweza kutamkwa na ambayo si halali kwa mtu kuyasema.  Nitajisifu kuhusu mtu wa namna hiyo, lakini sitajisifu kuhusu mimi mwenyewe isipokuwa kuhusu udhaifu wangu.  Kwa maana hata nikitaka kujisifu, sitakuwa mtu asiye na akili, kwa kuwa nitasema ukweli. Lakini sitaki kufanya hivyo, ili yeyote asinisifu zaidi ya yale anayoona kwangu au kusikia kutoka kwangu,  kwa sababu tu ya kupokea maono hayo ya ajabu. Ili nisijiinue mno, nilipewa mwiba katika mwili,+ malaika wa Shetani, aendelee kunipiga kofi,* ili nisijiinue kupita kiasi.  Mara tatu nilimwomba Bwana kuhusu jambo hili, kwamba aniondolee.  Lakini akaniambia: “Fadhili zangu zisizostahiliwa zinakutosha, kwa kuwa nguvu zangu zinakamilika katika udhaifu.”+ Kwa furaha zaidi, basi, nitajisifu kuhusu udhaifu wangu, ili nguvu za Kristo zibaki juu yangu kama hema. 10  Basi ninapendezwa na udhaifu, na matusi, na nyakati za uhitaji, na mateso na shida, kwa ajili ya Kristo. Kwa maana ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa na nguvu.+ 11  Nimekuwa mtu asiye na akili. Mlinilazimisha kuwa hivyo, kwa sababu ninyi mlipaswa kunipendekeza. Kwa maana hata katika jambo moja sikuwa mdogo kuliko mitume wenu walio bora sana, hata kama mimi si kitu.+ 12  Kwa kweli, ishara za mtume zilitokezwa kati yenu kwa uvumilivu mkubwa,+ na kwa ishara na mambo ya ajabu* na matendo yenye nguvu.+ 13  Ni kwa njia gani mlikosa kupendelewa kuliko makutaniko mengine, isipokuwa kwamba mimi mwenyewe sikuwa mzigo kwenu?+ Mnisamehe kosa hili kwa fadhili. 14  Tazama! Hii ni mara ya tatu niliyo tayari kuja kwenu, nami sitakuwa mzigo. Kwa kuwa ninawatafuta ninyi, si mali zenu;+ kwa maana watoto+ hawatarajiwi kuweka akiba kwa ajili ya wazazi wao, bali wazazi kwa ajili ya watoto wao. 15  Kwa upande wangu, nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili yenu.*+ Kama nikiwapenda ninyi sana, je, mimi nipendwe kidogo? 16  Lakini hata iweje, mimi sikuwa mzigo kwenu.+ Hata hivyo mnasema, nilikuwa “mjanja” na niliwashika “kwa ujanja.” 17  Sikujifaidi kutoka kwenu kupitia yeyote kati ya wale niliowatuma kwenu, sivyo? 18  Nilimhimiza Tito na nikamtuma yule ndugu pamoja naye. Je, kweli Tito alijifaidi kutoka kwenu?+ Tulitembea katika roho ileile, sivyo? Katika hatua zilezile, sivyo? 19  Je, mnafikiri kwamba muda huu wote tumekuwa tukijitetea kwenu? Tunazungumza mbele za Mungu katika muungano na Kristo. Lakini wapendwa, yote tunayofanya ni kwa ajili ya kuwajenga. 20  Kwa maana ninaogopa kwamba huenda nitakapofika, sitawakuta mkiwa kama ninavyotaka nami sitakuwa kama mnavyotaka, badala yake, huenda kuna mizozo, wivu, milipuko ya hasira, migawanyiko, masengenyo, minong’ono,* kujivuna kwa kiburi, na machafuko. 21  Labda nitakapokuja tena, huenda Mungu wangu akaninyenyekeza mbele yenu, nami niwaombolezee wengi kati ya wale ambao mwanzoni walitenda dhambi lakini hawajatubu unajisi wao na uasherati* na mwenendo mpotovu* ambao wametenda.

Maelezo ya Chini

Au “kunipiga.”
Au “miujiza.”
Au “nafsi zenu.”
Au “umbeya.”
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “ufidhuli; matendo ya kuchukiza yanayofanywa bila aibu.” Kigiriki, a·selʹgei·a. Angalia Kamusi.