Barua ya Pili kwa Wakorintho 2:1-17

  • Paulo akusudia kuleta shangwe (1-4)

  • Mtenda dhambi asamehewa na kurudishwa (5-11)

  • Paulo huko Troa na Makedonia (12, 13)

  • Huduma, maandamano ya ushindi (14-17)

    • Si wachuuzi wa neno la Mungu (17)

2  Kwa maana nimeamua kwamba sitakuja kwenu tena kwa huzuni.  Kwa maana nikiwahuzunisha ninyi, ni nani atakayekuwapo ili kunichangamsha isipokuwa yule ambaye nilimhuzunisha?  Niliandika mambo hayo, ili, nitakapokuja, nisihuzunishwe na wale ambao ninapaswa kushangilia juu yao, kwa sababu nina uhakika kwamba kile kinachonipa shangwe kinawapa ninyi nyote shangwe hiyohiyo.  Kwa maana kutokana na dhiki nyingi na maumivu ya moyo niliwaandikia kwa machozi mengi, si ili niwahuzunishe,+ bali niwajulishe kina cha upendo wangu kwenu.  Basi ikiwa yeyote amesababisha huzuni,+ hajanihuzunisha mimi, bali amewahuzunisha ninyi nyote kwa kadiri fulani—nisiwe mkali mno kwa yale ninayosema.  Karipio hili linalotolewa na wengi linamtosha mtu huyo;  badala yake, sasa mnapaswa kumsamehe kwa fadhili na kumfariji,+ ili asilemewe* na huzuni inayopita kiasi.+  Kwa hiyo ninawahimiza ninyi kumthibitishia upendo wenu.+  Ndiyo sababu niliwaandikia pia: ili kujua kama mngeonyesha uthibitisho wa utii wenu katika mambo yote. 10  Mkimsamehe mtu yeyote jambo lolote, mimi pia ninamsamehe. Kwa kweli, lolote ambalo nimesamehe (ikiwa nimesamehe jambo lolote) ni kwa ajili yenu machoni pa Kristo, 11  ili Shetani asitushinde akili,*+ kwa maana hatukosi kuzijua mbinu* zake.+ 12  Basi nilipofika Troa+ kutangaza habari njema kuhusu Kristo nami nikafunguliwa mlango katika Bwana, 13  roho yangu haikupata kitulizo kwa sababu sikumkuta Tito+ ndugu yangu. Basi, nikawaaga kisha nikaondoka kwenda Makedonia.+ 14  Lakini shukrani kwa Mungu, ambaye sikuzote hutuongoza katika maandamano ya ushindi kwa kushirikiana na Kristo, na kupitia sisi huieneza* harufu nzuri ya ujuzi kumhusu kila mahali! 15  Kwa maana kwa Mungu sisi ni harufu tamu ya Kristo kati ya wale wanaookolewa na kati ya wale wanaoangamia; 16  kwa hawa wa mwisho ni harufu ya kifo inayoleta kifo,+ kwa wale wa kwanza ni harufu ya uzima inayoleta uzima. Na ni nani anayestahili kabisa mambo haya? 17  Ni sisi, kwa maana sisi si wachuuzi wa* neno la Mungu+ kama watu wengi walivyo, bali tunasema kwa unyoofu wote, tukiwa tumetumwa na Mungu, ndiyo, machoni pa Mungu na kwa kushirikiana na Kristo.

Maelezo ya Chini

Au “asimezwe.”
Au “asitudanganye.”
Au “nia; njama.”
Au “huitambulisha.”
Au “hatufanyi biashara; hatupati faida kutokana na.”