Ayubu 2:1-13

  • Shetani atilia shaka tena nia ya Ayubu (1-5)

  • Shetani aruhusiwa kugusa mwili wa Ayubu (6-8)

  • Mke wa Ayubu: “Mtukane Mungu, ufe!” (9, 10)

  • Ayubu atembelewa na marafiki watatu (11-13)

2  Baadaye siku ilifika ambayo wana wa Mungu wa kweli*+ waliingia na kusimama mbele za Yehova,+ na Shetani pia akaingia kati yao na kusimama mbele za Yehova.+  Ndipo Yehova akamuuliza Shetani: “Umetoka wapi?” Shetani akamjibu Yehova: “Nimetoka kuzururazurura na kutembeatembea duniani.”+  Yehova akamwambia Shetani: “Je, umemwona* mtumishi wangu Ayubu? Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani. Yeye ni mtu mnyoofu na mtimilifu,*+ anayemwogopa Mungu na kuepuka uovu. Bado anashika kabisa utimilifu+ wake, hata ingawa unajaribu kunichochea dhidi yake+ ili nimwangamize* bila sababu.”  Lakini Shetani akamjibu Yehova: “Ngozi kwa ngozi. Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.*  Lakini, ili mambo yabadilike, nyoosha mkono wako upige mfupa na nyama yake, na kwa hakika atakutukana mbele za uso wako mwenyewe.”+  Ndipo Yehova akamwambia Shetani: “Tazama! Yumo mikononi mwako! Ila tu usiondoe uhai wake!”*  Kwa hiyo Shetani akaondoka mbele za* Yehova, akampiga Ayubu kwa majipu yenye maumivu makali*+ kuanzia wayo wa mguu mpaka utosini.  Na Ayubu akachukua kigae na kukitumia kujikuna, naye aliketi kwenye majivu.+  Hatimaye mke wake akamwambia: “Je, bado unashika kabisa utimilifu wako? Mtukane Mungu, ufe!” 10  Lakini akamwambia: “Unazungumza kama mmojawapo wa wanawake wapumbavu. Je, tukubali tu mambo mema kutoka kwa Mungu wa kweli, tusikubali pia mambo mabaya?”+ Licha ya hayo yote, Ayubu hakutenda dhambi kwa midomo yake.+ 11  Marafiki watatu wa Ayubu wakasikia kuhusu misiba yote iliyompata Ayubu, kila mmoja wao akaja kutoka nyumbani kwake—Elifazi+ Mtemani, Bildadi+ Mshua,+ na Sofari+ Mnaamathi. Basi wakakubaliana kukutana ili waende kumpa pole na kumfariji Ayubu. 12  Walipomwona kwa mbali, hawakumtambua. Wakaanza kulia kwa sauti kubwa na kurarua mavazi yao, wakarusha mavumbi hewani na juu ya vichwa vyao.+ 13  Kisha wakaketi ardhini pamoja naye kwa siku saba, mchana na usiku. Hakuna yeyote kati yao aliyemwambia neno lolote kwa sababu waliona kwamba alikuwa na maumivu makali sana.+

Maelezo ya Chini

Msemo wa Kiebrania unaorejelea malaika, wana wa Mungu.
Tnn., “umeuweka moyo wako juu ya.”
Au “mtu asiye na lawama na mnyoofu.”
Tnn., “nimmeze.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Tnn., “mbele za uso wa.”
Au “vidonda vibaya sana.”