Danieli 1:1-21

  • Yerusalemu lazingirwa na Wababiloni (1, 2)

  • Mafunzo maalumu ya mfalme kwa vijana waliohamishwa (3-5)

  • Uaminifu wa vijana wanne Waebrania wajaribiwa (6-21)

1  Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Mfalme Yehoyakimu+ wa Yuda, Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alikuja na kuzingira Yerusalemu.+  Baada ya muda Yehova akamtia Mfalme Yehoyakimu wa Yuda mikononi mwake,+ pamoja na baadhi ya vyombo vya nyumba ya* Mungu wa kweli, akavileta katika nchi ya Shinari*+ katika nyumba ya* mungu wake. Akaviweka katika hazina ya mungu wake.+  Kisha Mfalme Nebukadneza akamwagiza Ashpenazi ofisa mkuu wa makao yake ya kifalme awalete baadhi ya Waisraeli,* kutia ndani wale wanaotoka katika uzao wa kifalme na wa watu mashuhuri.+  Walipaswa kuwa vijana* wasio na kasoro yoyote, wazuri kwa umbo, waliobarikiwa kuwa na hekima, ujuzi, na utambuzi,+ na wanaoweza kutumikia katika jumba la mfalme. Alipaswa kuwafundisha maandishi na lugha ya Wakaldayo.  Pia, mfalme aliagiza wapewe kila siku vyakula bora ambavyo yeye mwenyewe alikula na divai ambayo alikunywa. Walipaswa kuzoezwa* kwa miaka mitatu, na baada ya muda huo wangeanza kumtumikia mfalme.  Sasa baadhi ya vijana hao walikuwa wa kabila la* Yuda: Danieli,*+ Hanania,* Mishaeli,* na Azaria.*+  Na ofisa mkuu wa makao ya mfalme akawapa majina;* alimpa Danieli jina Belteshaza,+ akampa Hanania jina Shadraki, akampa Mishaeli jina Meshaki, na kumpa Azaria jina Abednego.+  Lakini Danieli aliazimia moyoni mwake kwamba hatajichafua kwa vyakula bora vya mfalme wala divai yake. Basi akamwomba ofisa mkuu wa makao ya mfalme ruhusa ya kutojichafua kwa njia hiyo.  Na Mungu wa kweli akamfanya ofisa mkuu wa makao ya mfalme amtendee Danieli kwa fadhili* na rehema.+ 10  Lakini ofisa mkuu wa makao ya mfalme akamwambia Danieli: “Ninamwogopa bwana wangu mfalme, ambaye ametoa maagizo kuhusu vyakula na vinywaji vyenu. Itakuwaje akiona kwamba afya yenu ni mbaya kuliko ya vijana* wengine wa rika lenu? Mtanifanya niwe na* hatia mbele ya mfalme.” 11  Lakini Danieli akamwambia mtu aliyeteuliwa na ofisa mkuu wa makao ya mfalme ili kumtunza yeye, Hanania, Mishaeli, na Azaria: 12  “Tafadhali, tujaribu sisi watumishi wako kwa siku kumi, tupe mboga za majani na maji ya kunywa; 13  kisha linganisha sura zetu na sura za vijana* wanaokula vyakula bora vya mfalme, halafu ututendee sisi watumishi wako kulingana na jinsi tunavyoonekana machoni pako.” 14  Basi akakubali pendekezo lao na kuwajaribu kwa siku kumi. 15  Baada ya siku kumi sura yao ilikuwa nzuri zaidi na yenye afya zaidi* kuliko ya vijana* wote waliokuwa wakila vyakula bora vya mfalme. 16  Kwa hiyo mtu aliyewatunza alikuwa akichukua vyakula vyao bora na divai yao na kuwapa mboga za majani. 17  Na Mungu wa kweli aliwapa vijana* hao wanne ujuzi na ufahamu wa kila aina ya maandishi na hekima; naye Danieli alipewa uwezo wa kuelewa maono na ndoto za kila aina.+ 18  Mwishoni mwa kipindi ambacho mfalme aliagiza vijana wote waletwe ndani,+ ofisa mkuu wa makao ya mfalme aliwaleta mbele ya Nebukadneza. 19  Mfalme alipozungumza nao, hakuna kijana yeyote katika kikundi chote aliyekuwa kama Danieli, Hanania, Mishaeli, na Azaria;+ nao wakaendelea kumtumikia mfalme. 20  Katika kila jambo lililohitaji hekima na uelewaji ambalo mfalme aliwauliza, aliona kwamba walikuwa bora mara kumi kuliko makuhani wote wachawi na watu waliofanya mazingaombwe+ katika milki yake yote. 21  Danieli alibaki huko mpaka mwaka wa kwanza wa Mfalme Koreshi.+

Maelezo ya Chini

Au “hekalu la.”
Yaani, Babilonia.
Au “hekalu la.”
Tnn., “wana wa Israeli.”
Tnn., “watoto.”
Au labda, “kulishwa.”
Maana yake “Yehova Amesaidia.”
Huenda jina hili linamaanisha “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Maana yake “Yehova Ameonyesha Kibali.”
Tnn., “wana wa.”
Maana yake “Mwamuzi Wangu Ni Mungu.”
Yaani, majina ya Kibabiloni.
Tnn., “amwonyeshe Danieli kibali.”
Tnn., “Mtakifanya kichwa changu kiwe na.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “miili yao ilinenepa.”
Tnn., “watoto.”
Tnn., “watoto.”