Danieli 10:1-21

  • Danieli atembelewa na mjumbe wa Mungu (1-21)

    • Mikaeli amsaidia malaika (13)

10  Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Koreshi+ mfalme wa Uajemi, Danieli ambaye pia aliitwa Belteshaza+ alipewa ufunuo; na ujumbe wake ulikuwa wa kweli, nao ulihusu pambano kubwa. Naye alielewa ujumbe huo na kupewa uelewaji kuhusu mambo aliyokuwa ameona.  Siku hizo, mimi, Danieli, nilikuwa nikiomboleza+ kwa majuma matatu kamili.  Sikula kamwe chakula kizuri, sikula nyama wala kunywa divai, nami sikujipaka kamwe mafuta kwa majuma matatu kamili.  Katika siku ya 24 ya mwezi wa kwanza, nilipokuwa kwenye ukingo wa ule mto mkubwa, Mto Tigri,*+  niliinua macho yangu nikamwona mwanamume aliyevaa mavazi ya kitani,+ na kiunoni mwake alikuwa na mshipi wa dhahabu kutoka Ufazi.  Mwili wake ulikuwa kama krisolito,+ uso wake ulionekana kama radi, macho yake yalikuwa kama mienge inayowaka moto, mikono yake na miguu yake ilionekana kama shaba iliyong’arishwa,+ na mvumo wa maneno yake ulikuwa kama mvumo wa umati wa watu.  Ni mimi Danieli, peke yangu, niliyeona maono hayo; wanaume waliokuwa pamoja nami hawakuyaona.+ Hata hivyo, walishikwa na hofu kubwa, wakakimbia na kujificha.  Kisha nikabaki peke yangu, na nilipoona maono hayo makubwa nguvu ziliniishia na sura yangu ya heshima ikatoweka, nikapoteza nguvu zote.+  Kisha nikasikia sauti yake akizungumza; lakini nilipomsikia akizungumza, nikalala kifudifudi ardhini na kushikwa na usingizi mzito.+ 10  Lakini mkono ukanigusa,+ ukanitikisa ili niinuke kwa mikono na magoti yangu. 11  Kisha akaniambia: “Ee Danieli, wewe mtu mwenye thamani sana,*+ sikiliza kwa makini maneno ninayotaka kukwambia. Sasa simama mahali ulipo, kwa maana nimetumwa kwako.” Aliponiambia maneno hayo, nikasimama nikitetemeka. 12  Kisha akaniambia: “Usiogope,+ Ee Danieli. Maneno yako yamesikiwa tangu siku ya kwanza ulipoukaza moyo wako kupata uelewaji na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, nami nimekuja kwa sababu ya maneno yako.+ 13  Lakini mkuu+ wa ufalme wa Uajemi alinipinga kwa siku 21. Lakini Mikaeli,*+ mmoja wa wakuu wenye vyeo vya juu zaidi,* akaja kunisaidia; nami nikabaki huko kando ya wafalme wa Uajemi. 14  Nimekuja kukuelewesha mambo yatakayowapata watu wako katika kipindi cha mwisho cha zile siku,+ kwa maana ni maono yanayohusu siku zijazo.”+ 15  Sasa aliponiambia maneno hayo, niliuinamisha uso wangu chini nikashindwa kuongea. 16  Ndipo mmoja aliyeonekana kama mwanadamu akaigusa midomo yangu,+ nami nikafungua kinywa changu na kumwambia yule aliyesimama mbele yangu: “Bwana wangu ninaogopa kwa sababu ya maono hayo, nami sina nguvu.+ 17  Sasa bwana wangu, mimi mtumishi wako, ninawezaje kuzungumza nawe bwana wangu?+ Kwa maana sasa sina nguvu, na pumzi imeniishia.”+ 18  Yule aliyeonekana kama mwanadamu akanigusa tena na kunitia nguvu.+ 19  Kisha akasema: “Usiogope,+ Ee mtu mwenye thamani sana.*+ Uwe na amani.+ Uwe na nguvu, naam, uwe na nguvu.” Alipokuwa akizungumza nami nilitiwa nguvu na kusema: “Bwana wangu, sema, kwa maana umenitia nguvu.” 20  Ndipo akasema: “Je, unajua kwa nini nimekuja? Sasa nitarudi kupigana na mkuu wa Uajemi.+ Nitakapoondoka, mkuu wa Ugiriki atakuja. 21  Hata hivyo, nitakwambia mambo yaliyoandikwa katika kitabu cha kweli. Hakuna yeyote anayeniunga mkono kwa uthabiti katika mambo haya isipokuwa Mikaeli,+ mkuu wako.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Hidekeli.”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”
Au “mkuu wa cheo cha kwanza.”
Maana yake “Ni Nani Aliye Kama Mungu?”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”