Danieli 5:1-31

  • Sherehe ya mfalme Belshaza (1-4)

  • Maandishi ukutani (5-12)

  • Danieli aombwa aeleze maana ya maandishi (13-25)

  • Maana: Kuanguka kwa Babiloni (26-31)

5  Basi Mfalme Belshaza+ alifanya karamu kubwa kwa ajili ya wakuu wake elfu moja, naye alikuwa akinywa divai mbele yao.+  Alipokuwa amelewa, Belshaza akaagiza vyombo vya dhahabu na vya fedha ambavyo Nebukadneza baba yake alikuwa amevichukua kutoka katika hekalu la Yerusalemu viletwe,+ ili avitumie kunywea divai pamoja na wakuu wake, masuria wake, na wake zake wadogo.  Basi wakaleta vyombo vya dhahabu vilivyochukuliwa kutoka katika hekalu la Mungu kule Yerusalemu, na mfalme pamoja na wakuu wake, masuria wake na wake zake wadogo wakavitumia kunywea divai.  Wakanywa divai, nao wakaisifu miungu ya dhahabu na fedha, ya shaba, chuma, miti, na mawe.  Wakati huohuo, vidole vya mkono wa mwanadamu vikatokea na kuanza kuandika kwenye lipu ya ukuta wa jumba la mfalme unaoelekeana na kinara cha taa, na mfalme aliweza kuona sehemu ya nyuma ya mkono huo ulipokuwa ukiandika.  Ndipo uso wa mfalme ukabadilika rangi* na mawazo yake yakamwogopesha, kiuno chake kikalegea+ na magoti yake yakaanza kugongana.  Mfalme akawaita kwa sauti kubwa watu wanaofanya mazingaombwe, Wakaldayo,* na wanajimu.+ Mfalme akawaambia wanaume hao wenye hekima wa Babiloni: “Mtu yeyote atakayesoma maandishi haya na kuniambia maana yake atavishwa mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwake,+ naye atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+  Basi wanaume wote wenye hekima wa mfalme wakaja, lakini hawakuweza kusoma maandishi hayo wala kumwambia mfalme maana yake.+  Kwa hiyo Mfalme Belshaza akaogopa sana na uso wake ukazidi kubadilika rangi; na wakuu wake wakapigwa na bumbuazi.+ 10  Malkia aliposikia maneno ya mfalme na wakuu wake, akaingia kwenye ukumbi wa karamu. Malkia akasema: “Ee mfalme, uishi milele. Usiruhusu mawazo yako yakuogopeshe, wala usiruhusu uso wako ubadilike rangi. 11  Kuna mwanamume fulani* katika ufalme wako aliye na roho ya miungu mitakatifu. Katika siku za baba yako, mwanamume huyo alithibitika kuwa na ujuzi na ufahamu na hekima kama hekima ya miungu.+ Baba yako Mfalme Nebukadneza alimweka kuwa mkuu wa makuhani wachawi, watu wanaofanya mazingaombwe, Wakaldayo,* na wanajimu;+ hivyo ndivyo alivyofanya baba yako, Ee mfalme. 12  Kwa maana Danieli, ambaye mfalme alimwita Belteshaza,+ alikuwa na roho isiyo ya kawaida na ujuzi na ufahamu wa kueleza maana ya ndoto, kufumbua mafumbo, na kutatua matatizo magumu.*+ Basi agiza Danieli aitwe, atakwambia maana ya maandishi haya.” 13  Kwa hiyo Danieli akaletwa mbele ya mfalme. Mfalme akamuuliza Danieli: “Je, wewe ndiye Danieli, mmojawapo wa watu waliohamishwa na baba yangu mfalme kutoka Yuda?+ 14  Nimesikia kukuhusu kwamba roho ya miungu imo ndani yako+ na kwamba una ujuzi na ufahamu na hekima isiyo ya kawaida.+ 15  Sasa wanaume wenye hekima na watu wanaofanya mazingaombwe waliletwa mbele yangu ili wasome maandishi haya na kuniambia maana yake, lakini wameshindwa kuniambia maana ya ujumbe huu.+ 16  Lakini nimesikia kukuhusu kwamba unaweza kueleza maana ya mafumbo+ na kutatua matatizo magumu.* Sasa, ukifaulu kusoma maandishi haya na kuniambia maana yake, utavishwa mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwako, nawe utakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.”+ 17  Ndipo Danieli akamwambia mfalme: “Si lazima unipe zawadi zako, unaweza kuwapa wengine zawadi hizo. Hata hivyo, nitakusomea maandishi haya na kukuambia maana yake. 18  Ee mfalme, Mungu Aliye Juu Zaidi alimpa baba yako Nebukadneza ufalme na ukuu na heshima na fahari.+ 19  Kwa sababu ya ukuu ambao Mungu alimpa, watu wa makabila yote, mataifa, na lugha walitetemeka kwa woga mbele yake.+ Yeyote ambaye mfalme alitaka kumuua, alimuua, yeyote aliyetaka kumwacha hai, alimwacha hai, yeyote aliyetaka kumkweza, alimkweza, na yeyote aliyetaka kumwaibisha, alimwaibisha.+ 20  Lakini moyo wake ulipokuwa na kiburi na roho yake kuwa ngumu hivi kwamba akatenda kwa kimbelembele,+ alishushwa chini kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, naye akanyang’anywa heshima yake. 21  Alifukuzwa mbali kutoka kati ya wanadamu, na moyo wake ukafanywa kuwa kama wa mnyama, akaishi na punda mwitu. Alipewa majani ale kama ng’ombe dume, na mwili wake ukalowa umande wa mbinguni, mpaka alipojua kwamba Mungu Aliye Juu Zaidi ni Mtawala katika ufalme wa wanadamu na kwamba yeye humweka yeyote amtakaye juu ya ufalme huo.+ 22  “Lakini wewe Belshaza, mwanawe, hujaunyenyekeza moyo wako, ingawa ulijua hayo yote. 23  Badala yake, ulijikweza mwenyewe dhidi ya Bwana wa mbinguni,+ ukawaamuru wakuletee vyombo vya nyumba yake.+ Kisha wewe pamoja na wakuu wako, masuria wako, na wake zako wadogo mkavitumia kunywea divai na kuisifu miungu ya fedha na ya dhahabu, ya shaba, chuma, miti, na mawe, miungu ambayo haioni chochote na haisikii chochote na haijui chochote.+ Lakini hujamtukuza Mungu ambaye pumzi yako na njia zako zote zimo mikononi mwake.+ 24  Kwa hiyo yeye ndiye aliyeutuma mkono huo, na maandishi haya yakaandikwa ukutani.+ 25  Na haya ndiyo maandishi yaliyoandikwa: MENE, MENE, TEKELI, na PARSINI. 26  “Hii ndiyo maana ya maneno hayo: MENE, Mungu amehesabu siku za ufalme wako na kuukomesha.+ 27  “TEKELI, umepimwa katika mizani na kuonekana umepungukiwa. 28  “PERESI, ufalme wako umegawanywa wakapewa Wamedi na Waajemi.”+ 29  Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvisha Danieli mavazi ya zambarau na mkufu wa dhahabu shingoni mwake; wakatangaza kwamba atakuwa mtawala wa tatu katika ufalme.+ 30  Usiku huohuo Belshaza mfalme wa Wakaldayo aliuawa.+ 31  Na Dario+ Mmedi akaupokea ufalme; alikuwa na umri wa miaka 62 hivi.

Maelezo ya Chini

Au “sura ya mfalme ikabadilika.”
Yaani, wabashiri na wanajimu hodari.
Au “mwanamume mwenye uwezo.”
Yaani, wabashiri na wanajimu hodari.
Tnn., “kufungua mafundo.”
Tnn., “kufungua mafundo.”