Danieli 7:1-28

  • Maono ya wanyama wanne (1-8)

    • Pembe ndogo yenye majivuno yatokea (8)

  • Mzee wa Siku afanya kikao (9-14)

    • Mwana wa binadamu apewa ufalme (13, 14)

  • Danieli ajulishwa maana ya maono (15-28)

    • Wanyama wanne ni wafalme wanne (17)

    • Watakatifu kupokea ufalme (18)

    • Kusimama kwa pembe kumi, au wafalme (24)

7  Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Mfalme Belshaza+ wa Babiloni, Danieli aliota ndoto na kuona maono akiwa amelala kitandani mwake.+ Kisha akaandika ndoto hiyo;+ akaandika masimulizi kamili ya mambo hayo.  Danieli akasema: “Nilikuwa nikitazama katika maono yangu wakati wa usiku, na tazama! pepo nne za mbingu, zilikuwa zikivuruga bahari kubwa sana.+  Na wanyama wanne+ wakubwa sana wakatoka katika bahari hiyo, kila mmoja alikuwa tofauti na wenzake.  “Wa kwanza alikuwa kama simba,+ naye alikuwa na mabawa ya tai.+ Nikatazama mpaka mabawa yake yakang’olewa, akainuliwa kutoka duniani na kusimamishwa kwa miguu miwili kama mwanadamu, naye akapewa moyo wa mwanadamu.  “Na tazama! mnyama mwingine, wa pili, kama dubu.+ Aliinuliwa upande mmoja, na mbavu tatu zilikuwa kinywani mwake kati ya meno yake; naye akaambiwa, ‘Simama, kula nyama nyingi.’+  “Baada ya hayo nikaendelea kuangalia, na tazama! mnyama mwingine, kama chui,+ lakini mgongoni mwake alikuwa na mabawa manne kama ya ndege. Na mnyama huyo alikuwa na vichwa vinne,+ naye alipewa mamlaka ya kutawala.  “Baada ya hayo nikaendelea kutazama katika maono ya usiku, nikaona mnyama wa nne, mwenye kuogopesha na mwenye kutisha, na mwenye nguvu isivyo kawaida, naye alikuwa na meno makubwa ya chuma. Alikuwa akinyafua na kuvunjavunja, na kilichobaki alikikanyaga-kanyaga chini kwa miguu yake.+ Alikuwa tofauti na wanyama wote waliomtangulia, naye alikuwa na pembe kumi.  Nilipokuwa nikiangalia pembe hizo, tazama! pembe nyingine, ndogo,+ ikajitokeza miongoni mwa pembe hizo, na pembe tatu kati ya zile za kwanza zikang’olewa mbele yake. Na, tazama! pembe hiyo ilikuwa na macho kama ya mwanadamu, na ilikuwa na kinywa kinachozungumza kwa kiburi.*+  “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku+ akaketi.+ Mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji,+ na nywele za kichwa chake zilikuwa kama sufu safi. Kiti chake cha ufalme kilikuwa miali ya moto; magurudumu yake yalikuwa moto unaowaka.+ 10  Mto wa moto ulikuwa ukitiririka kutoka mbele zake.+ Elfu kwa maelfu waliendelea kumhudumia, na elfu kumi mara elfu kumi walisimama mbele zake.+ Mahakama+ ikaketi, na vitabu vikafunguliwa. 11  “Nikaendelea kutazama wakati huo kwa sababu ya mvumo wa maneno ya kiburi* yaliyokuwa yakisemwa na pembe hiyo;+ nilitazama mpaka mnyama huyo alipouawa na mwili wake ukaharibiwa na kutolewa ili uchomwe moto. 12  Lakini wale wanyama wengine+ walinyang’anywa tawala zao, na maisha yao yakarefushwa kwa wakati mmoja na majira. 13  “Nikaendelea kuangalia katika maono ya usiku, na tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu+ alikuwa akija na mawingu ya mbinguni; naye akaja mbele za Mzee wa Siku,+ nao wakamleta karibu Naye. 14  Naye akapewa utawala,+ heshima,+ na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie.+ Utawala wake ni utawala wa milele ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake hautaangamizwa.+ 15  “Basi, mimi Danieli, roho yangu ilifadhaika kwa sababu maono ya kichwa changu yaliniogopesha.+ 16  Nikamkaribia mmoja wa wale waliokuwa wamesimama pale ili nimuulize maana halisi ya mambo hayo. Basi akanijibu na kunieleza maana ya mambo hayo. 17  “‘Wanyama hawa wakubwa, wanne,+ ni wafalme wanne ambao watasimama kutoka duniani.+ 18  Lakini watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi+ watapokea ule ufalme,+ nao wataumiliki ufalme huo+ milele, naam, milele na milele.’ 19  “Kisha nikataka kujua mengi zaidi kuhusu yule mnyama wa nne, ambaye alikuwa tofauti na wale wengine; alikuwa mwenye kuogopesha isivyo kawaida; alikuwa na meno ya chuma na makucha ya shaba, naye alikuwa akinyafua na kuvunjavunja, na kukanyaga-kanyaga chini kwa miguu yake kilichobaki;+ 20  na pia kuhusu zile pembe kumi+ zilizokuwa kichwani mwake, na ile pembe nyingine iliyojitokeza na ambayo mbele yake pembe tatu zilianguka,+ pembe iliyokuwa na macho na kinywa kilichozungumza kwa kiburi* na ambayo umbo lake lilikuwa kubwa kuliko umbo la zile pembe nyingine. 21  “Nikaendelea kutazama pembe hiyo ilipokuwa ikiwapiga vita watakatifu, nayo ilikuwa ikiwashinda,+ 22  mpaka Mzee wa Siku+ alipokuja na kuhukumu kwa faida ya watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi,+ na wakati uliowekwa ukafika wa watakatifu kuumiliki ufalme.+ 23  “Alisema hivi: ‘Kuhusu yule mnyama wa nne, kuna ufalme wa nne utakaotokea duniani. Utakuwa tofauti na falme nyingine zote, nao utainyafua dunia yote na kuikanyaga-kanyaga chini na kuivunjavunja.+ 24  Kuhusu zile pembe kumi, wafalme kumi watainuka kutoka katika ufalme huo; na bado kuna mwingine atakayeinuka baada yao, atakuwa tofauti na wale wa kwanza, naye atawaaibisha wafalme watatu.+ 25  Atasema maneno dhidi ya Aliye Juu Zaidi,+ naye ataendelea kuwanyanyasa watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi. Atakusudia kubadili nyakati na sheria, nao watatiwa mikononi mwake kwa wakati, nyakati, na nusu wakati.*+ 26  Lakini ile Mahakama ikaketi, nao wakamnyang’anya utawala wake, ili wamwangamize na kumharibu kabisa.+ 27  “‘Na ufalme na utawala na utukufu wa falme chini ya mbingu zote ulikabidhiwa watu ambao ni watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.+ Ufalme wao ni ufalme wa milele,+ na tawala zote zitawatumikia na kuwatii wao.’ 28  “Huu ndio mwisho wa jambo hilo. Basi mimi, Danieli, mawazo yangu yaliniogopesha sana, hivi kwamba uso wangu ukabadilika* rangi; lakini niliweka jambo hilo katika moyo wangu mwenyewe.”

Maelezo ya Chini

Au “kujigamba.”
Au “kujigamba.”
Au “kwa kujigamba.”
Yaani, nyakati tatu na nusu.
Au “sura yangu ikabadilika.”