Danieli 8:1-27

  • Maono ya kondoo na mbuzi (1-14)

    • Pembe ndogo yajitukuza (9-12)

    • Mpaka jioni na asubuhi 2,300 (14)

  • Gabrieli aeleza maana ya maono (15-27)

    • Ufafanuzi kuhusu kondoo na mbuzi (20, 21)

    • Kutokea kwa mfalme mkali (23-25)

8  Katika mwaka wa tatu wa utawala wa Mfalme Belshaza,+ mimi, Danieli, niliona maono, baada ya yale niliyoona mwanzoni.+  Niliona maono hayo, na nilipokuwa nikiyaona nilikuwa katika ngome ya* Shushani,*+ iliyo katika mkoa wa* Elamu;+ niliona maono hayo, nami nilikuwa kando ya mfereji wa maji wa Ulai.  Nilipoinua macho yangu, tazama! kulikuwa na kondoo dume+ aliyesimama mbele ya mfereji huo wa maji, naye alikuwa na pembe mbili.+ Pembe hizo mbili zilikuwa ndefu, lakini moja ilikuwa ndefu kuliko nyingine, na pembe hiyo ndefu ilitokea baadaye.+  Nikamwona huyo kondoo dume akisonga mbele kwa nguvu kuelekea magharibi, kaskazini, na kusini, na hakuna mnyama yeyote wa mwituni aliyeweza kusimama mbele yake, wala hakukuwa na yeyote aliyeweza kuokoa kutoka katika nguvu zake.*+ Alifanya apendavyo na kujikweza.  Nilipokuwa nikiendelea kuangalia, tazama! kulikuwa na mbuzi dume+ aliyekuwa akija kutoka magharibi* akivuka dunia yote bila kugusa ardhi. Na mbuzi huyo alikuwa na pembe iliyoonekana waziwazi kati ya macho yake.+  Alikuwa akija kumwelekea yule kondoo dume mwenye pembe mbili ambaye nilimwona amesimama mbele ya ule mfereji wa maji; alikuwa akikimbia kumwelekea kwa ghadhabu kubwa.  Nikamwona akimkaribia yule kondoo dume, naye alikuwa amejawa na uchungu mwingi kumwelekea. Akampiga na kumwangusha chini huyo kondoo dume na kuzivunja pembe zake mbili, na kondoo dume huyo hakuwa na nguvu za kustahimili. Basi akamwangusha ardhini kondoo dume huyo na kumkanyaga-kanyaga, na hakukuwa na yeyote wa kumwokoa kutoka katika nguvu zake.*  Kisha huyo mbuzi dume akajikweza kupita kiasi, lakini mara tu alipokuwa na nguvu, ile pembe kubwa ikavunjika; kisha mahali pake zikatokea pembe nne zilizokuwa zikionekana waziwazi, kuelekea zile pepo nne za mbingu.+  Pembe nyingine ndogo ilitokea katika mojawapo ya pembe hizo, nayo ikakua ikawa kubwa sana kuelekea kusini na kuelekea mashariki* na kuelekea lile Pambo.*+ 10  Ikawa kubwa sana hivi kwamba ikalifikia jeshi la mbinguni, nayo ikasababisha sehemu ya jeshi hilo na baadhi ya nyota zianguke duniani, nayo ikazikanyaga-kanyaga. 11  Ikajikweza hata dhidi ya Mkuu wa jeshi hilo, na ile dhabihu inayotolewa daima ikaondolewa* kutoka kwake, na mahali pake patakatifu palipo imara pakatupwa chini.+ 12  Na kwa sababu ya uasi, jeshi likatiwa mikononi mwa pembe hiyo, pamoja na ile dhabihu inayotolewa daima,* nayo iliendelea kuutupa ukweli duniani, ikatenda na kufanikiwa. 13  Nami nikamsikia mtakatifu akizungumza, na mtakatifu mwingine akamuuliza mtakatifu aliyekuwa akizungumza: “Maono ya dhabihu inayotolewa daima* na ya uasi unaosababisha ukiwa yataendelea kwa muda gani+ kufanya mahali patakatifu na lile jeshi kuwa vitu vya kukanyagwa-kanyagwa?” 14  Basi akaniambia: “Kwa muda wa jioni na asubuhi 2,300; na hakika mahali patakatifu patarudishwa katika hali yake inayofaa.” 15  Mimi, Danieli, nilipokuwa nikiona maono hayo na kujaribu kuyaelewa, kwa ghafla nikamwona mtu fulani aliyeonekana kama mwanamume amesimama mbele yangu. 16  Kisha nikasikia sauti ya mwanamume katikati ya mfereji wa Ulai,+ akaita kwa sauti kubwa: “Gabrieli,+ mweleweshe mtu huyo mambo aliyoona.”+ 17  Kwa hiyo akakaribia mahali nilipokuwa nimesimama, lakini alipokuja niliogopa sana hivi kwamba nikaanguka chini kifudifudi. Akaniambia: “Elewa, Ee mwana wa binadamu, kwamba maono hayo ni ya wakati wa mwisho.”+ 18  Lakini alipokuwa akizungumza nami, nilishikwa na usingizi mzito huku nikiwa nimeanguka chini kifudifudi. Basi akanigusa na kunisimamisha mahali nilipokuwa nimesimama mwanzoni.+ 19  Kisha akasema: “Ninakujulisha yatakayotokea katika sehemu ya mwisho ya shutuma, kwa sababu maono hayo yanahusu wakati uliowekwa wa mwisho.+ 20  “Yule kondoo dume mwenye pembe mbili uliyemwona anafananisha wafalme wa Umedi na Uajemi.+ 21  Yule mbuzi dume mwenye manyoya anafananisha mfalme wa Ugiriki;+ na ile pembe kubwa iliyokuwa kati ya macho yake, inafananisha mfalme wa kwanza.+ 22  Kuhusu ile pembe iliyovunjika, kisha pembe nne zikatokea badala yake,+ kuna falme nne kutoka katika taifa lake zitakazosimama, lakini hazitakuwa na nguvu kama zake. 23  “Na katika kipindi cha mwisho cha ufalme wao, waasi watakapofikia kilele cha kutenda maovu, mfalme mwenye uso mkali anayeelewa mafumbo* atatokea. 24  Atakuwa na nguvu nyingi, lakini si kwa uwezo wake mwenyewe. Ataleta uharibifu kwa njia isiyo ya kawaida,* naye atafanikiwa katika kila analotenda. Atawaangamiza wenye nguvu, na pia watu watakatifu.+ 25  Na kwa ujanja wake atatumia udanganyifu kufanikiwa; na katika moyo wake atajikweza; na atawaangamiza watu wengi wakati wa usalama.* Hata atasimama dhidi ya Mkuu wa wakuu, lakini atavunjwa si kwa mkono wa mwanadamu. 26  “Mambo yaliyosemwa katika maono kuhusu jioni na asubuhi hizo ni ya kweli, lakini ni lazima uyaweke siri maono hayo, kwa sababu yanahusu kipindi cha siku nyingi kutoka sasa.”*+ 27  Basi mimi, Danieli, nilichoka sana nikawa mgonjwa kwa siku kadhaa.+ Kisha nikaamka na kufanya kazi ya mfalme;+ lakini mambo niliyokuwa nimeona yalifanya nife ganzi, na hakuna yeyote aliyeweza kuelewa maono hayo.+

Maelezo ya Chini

Au “jumba la mfalme la.”
Au “Susa.”
Au “wilaya ya utawala ya.”
Tnn., “mkono wake.”
Au “machweo ya jua.”
Tnn., “mkono wake.”
Au “mawio ya jua.”
Au “ule Urembo.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku kikaondolewa.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “kile kitu kinachotolewa kila siku.”
Au “aliye stadi wa hila.”
Au “Ataleta uharibifu wa kutisha.”
Au labda, “bila onyo.”
Au “wakati ujao ulio mbali.”