Danieli 9:1-27

  • Danieli atoa sala ya toba (1-19)

    • Miaka sabini ya ukiwa (2)

  • Gabrieli amtembelea Danieli (20-23)

  • Majuma sabini ya kinabii yatabiriwa (24-27)

    • Kutokea kwa Masihi baada ya majuma 69 (25)

    • Kuuawa kwa Masihi (26)

    • Kuangamizwa kwa jiji na mahali patakatifu (26)

9  Katika mwaka wa kwanza wa utawala wa Dario+ mwana wa Ahasuero—mzao wa Wamedi aliyekuwa amewekwa kuwa mfalme wa ufalme wa Wakaldayo+  katika mwaka wa kwanza wa utawala wake, mimi, Danieli, nilitambua kutokana na vitabu* idadi ya miaka iliyokuwa imetajwa katika neno la Yehova kwa nabii Yeremia ili kutimiza ukiwa wa Yerusalemu,+ yaani, miaka 70.+  Basi nikageuza uso wangu kumwelekea Yehova Mungu wa kweli, nikimsihi katika sala, pamoja na kufunga+ na kuvaa nguo za magunia na kujimwagia majivu.  Nilisali kwa Yehova Mungu wangu, nikaungama na kusema: “Ee Yehova Mungu wa kweli, Mungu mkuu na Mwenye kuogopesha, unayeshika agano lako na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu+ wale wanaokupenda na kushika amri zako,+  tumetenda dhambi na tumekosea na tumetenda uovu na kuasi;+ nasi tumegeuka na kuacha amri zako na sheria* zako.  Hatujawasikiliza watumishi wako manabii,+ ambao kwa jina lako walizungumza na wafalme wetu, wakuu wetu, mababu zetu, na watu wote nchini.  Ee Yehova, uadilifu ni wako, lakini aibu ni yetu kama ilivyo leo, sisi watu wa Yuda, wakaaji wa Yerusalemu, na Waisraeli wote, wale walio karibu na walio mbali, katika nchi zote ambazo uliwatawanya kwa sababu hawakutenda kwa uaminifu kukuelekea.+  “Ee Yehova, aibu ni yetu, wafalme wetu, wakuu wetu, na mababu zetu, kwa sababu tumekutendea dhambi.  Rehema na msamaha ni zako Yehova Mungu wetu,+ kwa maana tumekuasi.+ 10  Hatujaitii sauti yako Yehova Mungu wetu kwa kufuata sheria zako ulizotupatia kupitia watumishi wako manabii.+ 11  Waisraeli wote wamekiuka Sheria yako na kukuacha kwa kutotii sauti yako, hivi kwamba ukatumwagia laana na kiapo kilichoandikwa katika Sheria ya Musa mtumishi wa Mungu wa kweli,+ kwa maana tumekutendea Wewe dhambi. 12  Umetimiza maneno uliyosema dhidi yetu+ na dhidi ya watawala wetu waliotutawala,* kwa kutuletea msiba mkubwa; hakuna jambo lililowahi kufanywa chini ya mbingu zote kama jambo lililofanywa Yerusalemu.+ 13  Kama tu ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa, msiba huu wote umetujia,+ lakini hatujakuomba kibali* Yehova Mungu wetu kwa kuacha uovu wetu+ na kwa kuonyesha ufahamu katika ukweli* wako. 14  “Basi Yehova ukakaa macho na kutuletea msiba, kwa maana wewe Yehova Mungu wetu ni mwadilifu katika kazi zote ambazo umefanya; hata hivyo sisi hatujaitii sauti yako.+ 15  “Sasa, Ee Yehova Mungu wetu, Wewe uliyewatoa watu wako nchini Misri kwa mkono wenye nguvu,+ na kujijengea jina hadi leo hii,+ tumefanya dhambi na kutenda uovu. 16  Ee Yehova, kulingana na matendo yako yote ya uadilifu,+ tafadhali, iondoe hasira na ghadhabu yako kutoka katika jiji lako Yerusalemu, mlima wako mtakatifu; kwa maana dhambi zetu na makosa ya mababu zetu yamefanya Yerusalemu na watu wako wawe kitu cha kushutumiwa na watu wote wanaotuzunguka.+ 17  Na sasa sikiliza, Ee Mungu wetu, sala yangu mimi mtumishi wako na maombi yangu, na ufanye uso wako uangaze juu ya mahali pako patakatifu+ palipo ukiwa,+ kwa ajili yako mwenyewe, Ee Yehova. 18  Tega sikio lako, Ee Mungu wangu, usikie! Fungua macho yako uone hali yetu ya ukiwa na jiji ambalo limeitwa kwa jina lako; kwa maana hatukuombi kwa sababu ya matendo yetu ya uadilifu bali kwa sababu ya rehema yako kuu.+ 19  Ee Yehova, sikia. Ee Yehova, samehe.+ Ee Yehova, sikiliza kwa makini na uchukue hatua. Usikawie, kwa ajili yako mwenyewe, Ee Mungu wangu, kwa maana jiji lako na watu wako wameitwa kwa jina lako mwenyewe.”+ 20  Nilipokuwa bado nikiongea na kusali na kuungama dhambi yangu na dhambi ya watu wangu Waisraeli na kuomba kibali mbele za Yehova Mungu wangu kuhusu mlima mtakatifu wa Mungu wangu,+ 21  naam, nilipokuwa bado nikisali, mwanamume Gabrieli,+ niliyekuwa nimemwona awali katika maono,+ alinijia nilipokuwa nimechoka kwelikweli karibu wakati ambao zawadi ya jioni hutolewa. 22  Naye akanipa uelewaji akisema: “Ee Danieli, sasa nimekuja kukupa ufahamu na uelewaji. 23  Ulipoanza kusali jibu lilitolewa, nami nimekuja kukujulisha jibu hilo, kwa sababu wewe ni mtu mwenye thamani sana.*+ Basi zingatia ujumbe huu na kuelewa maono haya. 24  “Kuna majuma 70* ambayo yameamuliwa kwa ajili ya watu wako na kwa ajili ya jiji lako takatifu,+ ili kukomesha uasi, kumaliza kabisa dhambi,+ kufunika makosa,+ kuleta uadilifu wa milele,+ kutia muhuri maono na unabii,*+ na kutia mafuta Patakatifu pa Patakatifu.* 25  Unapaswa kujua na kuelewa kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu+ mpaka atakapotokea Masihi*+ aliye Kiongozi,+ kutakuwa na majuma 7, na pia majuma 62.+ Yerusalemu litarudishwa na kujengwa upya, pamoja na uwanja wa jiji na handaki, lakini katika nyakati za taabu. 26  “Na baada ya hayo majuma 62, Masihi atauawa,*+ hatabaki na chochote.+ “Na watu wa kiongozi anayekuja wataliharibu jiji na mahali patakatifu.+ Na mwisho wake utakuwa kwa mafuriko. Na mpaka ule mwisho kutakuwa na vita; kilichoamuliwa ni ukiwa.+ 27  “Naye atalitendesha agano kwa ajili ya wengi kwa juma moja; na katika nusu ya juma hilo atakomesha dhabihu na toleo la zawadi.+ “Na juu ya bawa la vitu vyenye kuchukiza sana kutakuwa na yule anayesababisha ukiwa;+ na mpaka wakati wa maangamizi, kilichoamuliwa kitamwagwa pia juu ya yule anayekaa ukiwa.”

Maelezo ya Chini

Yaani, vitabu vitakatifu.
Au “hukumu.”
Tnn., “waamuzi wetu waliotuhukumu.”
Au “hatujautuliza uso wa.”
Au “uaminifu.”
Au “anayependwa sana; anayeheshimiwa sana.”
Yaani, majuma 70 ya miaka.
Au “Patakatifu Zaidi.”
Tnn., “nabii.”
Au “Mtiwa-Mafuta.”
Tnn., “atakatiliwa mbali.”