Ezekieli 1:1-28

  • Ezekieli aona maono ya Mungu akiwa Babiloni (1-3)

  • Maono ya gari la kimbingu la Yehova (4-28)

    • Dhoruba, wingu, na moto (4)

    • Viumbe hai wanne (5-14)

    • Magurudumu manne (15-21)

    • Anga linalometameta kama barafu (22-24)

    • Kiti cha ufalme cha Yehova (25-28)

1  Katika mwaka wa 30, siku ya tano ya mwezi wa nne, nilipokuwa kando ya mto Kebari+ miongoni mwa watu waliohamishwa,+ mbingu zilifunguliwa nami nikaanza kuona maono ya Mungu.  Katika siku ya tano ya mwezi huo—yaani, katika mwaka wa tano wa uhamisho wa mfalme Yehoyakini+  neno la Yehova lilimjia Ezekieli* mwana wa Buzi kuhani akiwa kando ya mto Kebari katika nchi ya Wakaldayo.+ Na huko, mkono wa Yehova ukaja juu yake.+  Nilipokuwa nikitazama, nikaona tufani ya upepo+ ikija kutoka kaskazini, na kulikuwa na wingu kubwa na moto unaowakawaka*+ uliozungukwa na nuru nyangavu, na katikati ya ule moto kulikuwa na kitu kilichong’aa kama mchanganyiko wa dhahabu na fedha.+  Katikati yake kulikuwa na mfano wa viumbe hai wanne,+ na kila mmoja wao alifanana na mwanadamu.  Kila mmoja wao alikuwa na nyuso nne na mabawa manne.+  Miguu yao ilikuwa imenyooka, na nyayo za miguu yao zilikuwa kama nyayo za ndama, nayo ilikuwa iking’aa kama shaba iliyong’arishwa.+  Walikuwa na mikono ya mwanadamu chini ya mabawa yao pande zote nne, na wote wanne walikuwa na nyuso na mabawa.  Mabawa yao yaligusana. Hawakugeuka walipokuwa wakienda; kila mmoja wao alikuwa akienda mbele moja kwa moja.+ 10  Nyuso zao zilionekana hivi: Kila mmoja wa viumbe hao wanne alikuwa na uso wa mwanadamu na uso wa simba+ upande wa kulia, na uso wa ng’ombe dume+ upande wa kushoto, na kila mmoja wa viumbe hao wanne alikuwa na uso+ wa tai.+ 11  Hivyo ndivyo nyuso zao zilivyokuwa. Mabawa yao yalikuwa yamenyooshwa juu yao. Kila mmoja wao alikuwa na mabawa mawili yaliyogusana na mabawa mawili yaliyofunika miili yao.+ 12  Kila mmoja wao alikuwa akienda mbele moja kwa moja, walienda popote ambapo roho iliwaelekeza kwenda.+ Hawakugeuka walipokuwa wakienda. 13  Na wale viumbe hai walionekana kama makaa ya moto yanayowaka, na kitu kilichofanana na mienge ya moto mwangavu kilikuwa kikisonga mbele na nyuma katikati ya hao viumbe hai, na radi ilikuwa ikiwakawaka kutoka katika ule moto.+ 14  Na hao viumbe hai walipoenda na kurudi, mwendo wao ulionekana kama radi inayowakawaka. 15  Nilipoendelea kuwatazama hao viumbe hai, niliona gurudumu moja duniani kando ya kila mmoja wa hao viumbe hai wenye nyuso nne.+ 16  Magurudumu hayo na muundo wake yalionekana yaking’aa kama krisolito, na yote manne yalifanana. Na mwonekano wake na muundo wake ni kama gurudumu lililokuwa ndani ya gurudumu.* 17  Yaliposonga, yangeweza kwenda upande wowote kati ya zile pande nne bila kugeuka yalipokuwa yakienda. 18  Mizingo yake ilikuwa juu sana hivi kwamba iliogopesha, na mizingo ya magurudumu yote manne ilikuwa imejaa macho kuizunguka.+ 19  Wakati wowote viumbe hai waliposonga, yale magurudumu yalisonga pamoja nao, na wale viumbe hai walipoinuliwa kutoka duniani, yale magurudumu yaliinuliwa juu pia.+ 20  Walienda popote ambapo roho iliwaelekeza kwenda, popote roho ilipoenda. Magurudumu yaliinuliwa pamoja nao, kwa maana roho iliyokuwa ikitenda katika wale viumbe hai* ilikuwa pia katika yale magurudumu. 21  Waliposonga, magurudumu hayo yalisonga; na waliposimama tuli, nayo yalisimama tuli; na walipoinuliwa juu kutoka duniani, magurudumu yaliinuliwa juu pamoja nao, kwa maana roho iliyokuwa ikitenda katika wale viumbe hai ilikuwa pia katika yale magurudumu. 22  Juu ya vichwa vya wale viumbe hai kulikuwa na mfano wa anga lililometameta kama barafu inayotisha, lililotanda juu ya vichwa vyao.+ 23  Chini ya anga hilo mabawa yao yalikuwa yamenyooka,* moja kuelekea lingine. Kila mmoja alikuwa na mabawa mawili ya kufunika upande mmoja wa mwili wake na mawili ya kufunika upande mwingine. 24  Niliposikia sauti ya mabawa yao, ilikuwa kama sauti ya maji yenye kishindo, kama sauti ya Mweza-Yote.+ Waliposonga, ilikuwa kama sauti ya jeshi. Waliposimama tuli, waliyashusha mabawa yao. 25  Kulikuwa na sauti juu ya anga lililokuwa juu ya vichwa vyao. (Waliposimama tuli, waliyashusha mabawa yao.) 26  Juu ya anga lililokuwa juu ya vichwa vyao kulikuwa na kitu kilichoonekana kama jiwe la yakuti,+ na kilifanana na kiti cha ufalme.+ Kwenye kiti hicho cha ufalme aliketi mmoja aliyeonekana kama mwanadamu.+ 27  Nami nikaona kitu kinachong’aa kama mchanganyiko wa dhahabu na fedha,+ kilichokuwa kama moto unaong’aa kutoka kwenye kile kilichoonekana kuwa kiuno chake kwenda juu; na kutoka kwenye kiuno chake kwenda chini, nikaona kitu kilichofanana na moto.+ Kulikuwa na mwangaza mkali kumzunguka pande zote 28  kama wa upinde wa mvua+ katika mawingu siku ya mvua. Hivyo ndivyo mwangaza uliozunguka pande zote ulivyoonekana. Ulikuwa kama mwonekano wa utukufu wa Yehova.+ Nilipouona, nikaanguka chini kifudifudi na kuanza kusikia sauti ya mtu akizungumza.

Maelezo ya Chini

Maana yake “Mungu Huimarisha.”
Au “na radi.”
Labda yalikutana katikati kwenye mhimili mmoja katika pembe mraba.
Tnn., “roho ya yule kiumbe hai.”
Au labda, “yalinyooka moja kwa moja.”