Ezekieli 11:1-25

  • Wakuu waovu washutumiwa (1-13)

    • Jiji lafananishwa na chungu cha kupikia (3-12)

  • Ahadi ya kurudishwa (14-21)

    • Wapewa “roho mpya” (19)

  • Utukufu wa Yehova waondoka Yerusalemu (22, 23)

  • Ezekieli arudi Ukaldayo katika maono (24, 25)

11  Na roho ikaniinua juu na kunileta kwenye lango la mashariki la nyumba ya Yehova, lango linalotazama mashariki.+ Hapo langoni niliona wanaume 25, na miongoni mwao kulikuwa na Yaazania mwana wa Azuri na Pelatia mwana wa Benaya, wakuu wa watu.+  Kisha Yeye akaniambia: “Mwana wa binadamu, hawa ndio wanaume wanaopanga uovu na kutoa ushauri wa uovu katika* jiji hili.  Wanasema, ‘Je, huu si wakati wa kujenga nyumba?+ Jiji* ni chungu cha kupikia,*+ na sisi ni nyama.’  “Basi tabiri dhidi yao. Tabiri, mwana wa binadamu.”+  Ndipo roho ya Yehova ikaja juu yangu,+ naye akaniambia: “Waambie, ‘Yehova anasema hivi: “Mambo mliyosema ni sahihi, enyi watu wa nyumba ya Israeli, nami ninajua mnachofikiria.*  Mmewafanya wengi wafe katika jiji hili, nanyi mmezijaza barabara zake watu waliokufa.”’”+  “Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Maiti mlizotawanya jijini ndizo nyama, nalo jiji ni chungu cha kupikia.+ Lakini ninyi wenyewe mtatolewa ndani yake.’”  “‘Mmeuogopa upanga,+ nami nitauleta upanga dhidi yenu,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.  ‘Nitawatoa ninyi ndani yake na kuwatia mikononi mwa watu wa nchi ya kigeni na kutekeleza hukumu dhidi yenu.+ 10  Mtauawa kwa upanga.+ Nitawahukumu kwenye mpaka wa Israeli,+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.+ 11  Jiji halitakuwa chungu chenu cha kupikia, nanyi hamtakuwa nyama iliyo ndani yake; nitawahukumu ninyi kwenye mpaka wa Israeli, 12  nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova. Kwa maana hamkutembea katika masharti yangu wala kutenda hukumu zangu,+ bali mmetenda kulingana na hukumu za mataifa yanayowazunguka.’”+ 13  Mara tu nilipotabiri, Pelatia mwana wa Benaya akafa, nami nikaanguka chini kifudifudi na kulia kwa sauti: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Je, utawaangamiza Waisraeli wanaobaki?”+ 14  Neno la Yehova likanijia tena likisema: 15  “Mwana wa binadamu, ndugu zako, ndugu zako walio na haki ya kukomboa, pamoja na watu wote wa nyumba ya Israeli, wameambiwa na wakaaji wa Yerusalemu, ‘Msimkaribie Yehova. Nchi ni yetu; tumepewa ili tuimiliki.’ 16  Kwa hiyo waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ingawa nimewapeleka mbali sana miongoni mwa mataifa, nami nimewatawanya katika nchi hizo,+ baada ya muda mfupi nitakuwa kwao mahali patakatifu katika nchi ambazo wameenda.”’+ 17  “Kwa hiyo waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Pia nitawakusanya ninyi kutoka kwa mataifa na kuwakusanya kutoka katika nchi ambazo mmetawanywa, nami nitawapa nchi ya Israeli.+ 18  Nao watarudi huko na kuondoa humo vitu vyote vinavyochukiza na mazoea yote yanayochukiza.+ 19  Nami nitawapa moyo wenye umoja,*+ nami nitatia roho mpya ndani yao;+ nami nitauondoa moyo wa jiwe katika miili yao+ na kuwapa moyo wa nyama,*+ 20  ili watembee katika sheria zangu na kushika hukumu zangu na kuzitii. Kisha watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao.”’ 21  “‘“Lakini kwa wale ambao mioyo yao imeazimia kuendelea kufanya mambo yao yanayochukiza na mazoea yao yanayochukiza, nitawaletea madhara ya njia yao juu ya kichwa chao,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’” 22  Sasa wale makerubi wakayainua juu mabawa yao, na yale magurudumu yalikuwa karibu nao,+ na utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa juu yao.+ 23  Kisha utukufu wa Yehova+ ukapanda kutoka jijini ukasimama juu ya mlima ulio upande wa mashariki wa jiji hilo.+ 24  Kisha roho ikaniinua juu—katika maono kupitia roho ya Mungu—na kunileta kwa watu walio uhamishoni huko Ukaldayo. Kisha maono niliyokuwa nimeyaona yakatoweka. 25  Nami nikaanza kuwaambia watu walio uhamishoni mambo yote ambayo Yehova alikuwa amenionyesha.

Maelezo ya Chini

Au “dhidi ya.”
Yaani, jiji la Yerusalemu, ambamo Wayahudi walidhani watalindwa.
Au “chungu cha kupikia chenye mdomo mpana.”
Au “mambo yanayokuja katika roho yenu.”
Yaani, moyo ulio mwepesi kutii mwongozo wa Mungu.
Tnn., “moyo mmoja.”