Ezekieli 12:1-28

  • Atabiri uhamisho kwa mifano (1-20)

    • Mizigo ya kwenda uhamishoni (1-7)

    • Mkuu ataondoka kukiwa na giza (8-16)

    • Mkate wa wasiwasi, maji ya hofu (17-20)

  • Msemo wa udanganyifu wathibitika kuwa uwongo (21-28)

    • “Hakuna neno langu lolote litakalokawia” (28)

12  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, unaishi katika nyumba ya uasi. Wana macho ya kuona, lakini hawaoni, na masikio ya kusikia, lakini hawasikii,+ kwa maana wao ni nyumba ya uasi.+  Nawe, mwana wa binadamu, jitayarishie mizigo ya kwenda uhamishoni. Kisha, mchana wakiwa wanatazama, unapaswa kwenda uhamishoni. Toka nyumbani kwako uende uhamishoni mahali pengine huku wakitazama. Labda wataona, ingawa wao ni nyumba ya uasi.  Wakati wa mchana toa mizigo yako iliyofungwa kwa ajili ya kwenda uhamishoni huku wakitazama, kisha jioni huku wakitazama, uondoke kama mtu anayepelekwa uhamishoni.+  “Toboa shimo ukutani huku wakitazama, nawe ubebe mizigo yako na kupitia humo.+  Beba mizigo yako begani huku wakikutazama, nawe uende nayo gizani. Ufunike uso wako ili usiweze kuona chini, kwa maana ninakufanya uwe ishara kwa watu wa nyumba ya Israeli.”+  Nikafanya kama nilivyoamriwa. Nikaitoa mizigo yangu nje mchana kama mizigo ya kwenda uhamishoni, na jioni nikatoboa shimo ukutani kwa mkono. Na kulipokuwa na giza, nikachukua mizigo yangu, nikaibeba begani mbele ya macho yao.  Asubuhi neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, je, watu wa nyumba ya Israeli, nyumba ya uasi, hawakukuuliza, ‘Unafanya nini?’ 10  Waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Tangazo hili linamhusu mkuu+ huko Yerusalemu na watu wote wa nyumba ya Israeli walio jijini.”’ 11  “Waambie, ‘Mimi ni ishara kwenu.+ Kama vile nilivyotenda, ndivyo watakavyotendewa. Watapelekwa uhamishoni, utekwani.+ 12  Mkuu aliye miongoni mwao atabeba mizigo yake begani na kuondoka kukiwa na giza. Atatoboa shimo ukutani na kuibeba mizigo yake kupitia humo.+ Ataufunika uso wake ili asione chini.’ 13  Nitautandaza wavu wangu juu yake, naye atakamatwa katika wavu wangu wa kuwindia.+ Kisha nitampeleka Babiloni, kwenye nchi ya Wakaldayo, lakini hataiona; naye atafia huko.+ 14  Na wote wanaomzunguka, wasaidizi wake na wanajeshi wake, nitawatawanya pande zote;+ nami nitauchomoa upanga ili kuwakimbiza.+ 15  Nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakapowatawanya miongoni mwa mataifa na kuwatawanya katika nchi hizo. 16  Lakini nitawalinda watu wachache kati yao wasife kwa upanga, njaa kali, na ugonjwa hatari, ili wasimulie kuhusu mazoea yao yote yanayochukiza miongoni mwa mataifa ambamo watapelekwa; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” 17  Nalo neno la Yehova likanijia tena likisema: 18  “Mwana wa binadamu, unapaswa kula mkate wako ukitetemeka na kunywa maji yako ukifadhaika na kuhangaika.+ 19  Waambie watu wa nchi, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anawaambia hivi wakaaji wa Yerusalemu katika nchi ya Israeli: “Watakula mkate wao kwa wasiwasi na kunywa maji yao kwa hofu, kwa maana nchi yao itakuwa ukiwa kabisa+ kwa sababu ya ukatili wa wale wote wanaokaa ndani yake.+ 20  Majiji yanayokaliwa yataharibiwa, na nchi itakuwa ukiwa;+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”’”+ 21  Nalo neno la Yehova likanijia tena likisema: 22  “Mwana wa binadamu, ni methali gani hii mliyo nayo katika Israeli, inayosema, ‘Siku zinapita, na maono yote hayatimii’?+ 23  Kwa hiyo waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitafanya msemo huo ukome, nao hawatautumia tena kama methali katika Israeli.”’ Lakini waambie, ‘Siku zimekaribia,+ na maono yote yatatimia.’ 24  Kwa maana hakutakuwa tena na maono ya uwongo au uaguzi* wa udanganyifu katika nyumba ya Israeli.+ 25  ‘“Kwa maana mimi, Yehova, nitasema. Neno lolote nitakalosema litafanywa bila kukawia zaidi.+ Katika siku zenu,+ enyi nyumba ya uasi, nitasema neno na kulitimiza,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’” 26  Neno la Yehova likanijia tena likisema: 27  “Mwana wa binadamu, hivi ndivyo watu wa* Israeli wanavyosema, ‘Maono anayoona ni ya muda mrefu kutoka sasa, naye anatabiri kuhusu wakati ujao ulio mbali.’+ 28  Kwa hiyo waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “‘Hakuna neno langu lolote litakalokawia; jambo lolote nitakalosema litafanywa,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”’”

Maelezo ya Chini

Au “ubashiri.”
Tnn., “nyumba ya.”