Ezekieli 13:1-23

  • Dhidi ya manabii wa uwongo (1-16)

    • Kuta zilizopakwa chokaa zitaanguka (10-12)

  • Dhidi ya manabii wa kike wa uwongo (17-23)

13  Na neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, tabiri dhidi ya manabii wa Israeli,+ nawe uwaambie hivi wale wanaotunga unabii wao wenyewe:*+ ‘Sikieni neno la Yehova.  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ole wao manabii wapumbavu, wanaofuata roho yao wenyewe, ingawa hawajaona chochote!+  Ewe Israeli, manabii wako wamekuwa kama mbweha katika magofu.  Hamtaenda mahali palipobomoka katika kuta za mawe ili kuzijenga upya kwa ajili ya watu wa nyumba ya Israeli,+ ili Waisraeli waendelee kusimama vitani katika siku ya Yehova.”+  “Wameona maono ya uwongo na kutabiri uwongo, wale wanaosema, ‘Neno la Yehova ni,’ wakati ambapo Yehova mwenyewe hajawatuma, nao wamengoja neno lao litimie.+  Je, ninyi hamkuona maono ya uwongo, na kutabiri uwongo, mnaposema, ‘Neno la Yehova ni,’ wakati ambapo sijasema lolote?”’  “‘Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “‘Kwa sababu mmesema uwongo na maono yenu ni ya uwongo, mimi niko dhidi yenu,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”+  Mkono wangu uko dhidi ya manabii ambao maono yao ni ya uwongo na wanaotabiri uwongo.+ Nao hawatakuwa miongoni mwa watu ninaowaambia siri zangu; wala hawataandikwa katika orodha ya watu wa nyumba ya Israeli; wala hawatarudi katika nchi ya Israeli; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.+ 10  Hayo yote ni kwa sababu wamewapotosha watu wangu wakisema, “Kuna amani!” wakati hakuna amani.+ Ukuta dhaifu unapojengwa, wanaupiga lipu kwa chokaa.’*+ 11  “Waambie wale wanaopiga lipu kwa chokaa kwamba ukuta huo utaanguka. Mvua kubwa ya mafuriko itakuja, mvua ya mawe itanyesha,* na dhoruba kali za upepo zitaubomoa.+ 12  Na ukuta huo utakapoanguka mtaulizwa, ‘Chokaa mliyopaka iko wapi?’+ 13  “Kwa hiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Nitasababisha dhoruba kali za upepo zilipuke kwa ghadhabu yangu, na mvua kubwa ya mafuriko kwa hasira yangu, na mvua ya mawe kwa ghadhabu inayoangamiza. 14  Nitaubomoa ukuta ambao mmeupiga lipu kwa chokaa na kuuangusha chini ardhini, na msingi wake utafunuliwa. Jiji litakapoanguka, mtaangamia ndani yake; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’ 15  “‘Nitakapoumwagia ukuta huo ghadhabu yangu yote na kuwamwagia wale walioupiga lipu kwa chokaa, nitawaambia ninyi: “Ukuta haupo tena, na wale wanaoupiga lipu hawapo tena.+ 16  Manabii wa Israeli hawapo tena, wale wanaowatabiria watu wa Yerusalemu na kuona maono ya amani kwa ajili yao, wakati hakuna amani,”’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 17  “Nawe, mwana wa binadamu, uelekeze uso wako dhidi ya mabinti wa watu wako wanaotunga unabii wao wenyewe, nawe utabiri dhidi yao. 18  Waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ole wao wanawake wanaoshona pamoja tepe kwa ajili ya mikono yote* na kutengeneza shela kwa ajili ya vichwa vya kila ukubwa ili kuwinda uhai wa* watu! Je, mnawinda uhai wa* watu wangu na kujaribu kuhifadhi uhai wenu* wenyewe? 19  Je, mtanitia unajisi miongoni mwa watu wangu kwa ajili ya makonzi ya shayiri na kwa ajili ya makombo ya mkate,+ mkiwaua watu wasiostahili kufa na kuwaacha hai watu wasiostahili kuishi, kwa kuwadanganya watu wangu, wanaosikiliza uwongo wenu?”’+ 20  “Kwa hiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Niko dhidi ya tepe zenu enyi wanawake, mnazotumia kuwinda watu* kana kwamba wao ni ndege, nami nitazirarua kutoka mikononi mwenu na kuwafungua watu mnaowawinda kama ndege. 21  Nitazirarua shela zenu na kuwaokoa watu wangu kutoka mikononi mwenu, nao hawatakuwa tena windo lenu; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.+ 22  Kwa sababu mmemvunja moyo aliye mwadilifu kwa uwongo wenu+ ingawa mimi mwenyewe sikuwa nimemsababishia taabu,* nanyi mmeiimarisha mikono ya mwovu+ ili asiiache njia yake ya uovu na kuendelea kuishi.+ 23  Kwa hiyo, ninyi wanawake hamtaona tena maono ya uwongo na kufanya uaguzi;*+ nami nitawaokoa watu wangu kutoka mikononi mwenu, nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”

Maelezo ya Chini

Au “wanaotabiri kutoka moyoni mwao wenyewe.”
Yaani, wanajenga ukuta wa ndani ulio dhaifu na kujaribu kuufanya uonekane imara kwa chokaa.
Tnn., “nanyi, enyi mawe ya mvua mtanyesha.”
Yaani, tepe za uchawi zinazovaliwa kwenye viwiko au mkononi.
Au “nafsi za.”
Au “nafsi za.”
Au “nafsi zenu.”
Au “nafsi.”
Au “maumivu.”
Au “ubashiri.”