Ezekieli 14:1-23

  • Wanaoabudu sanamu washutumiwa (1-11)

  • Hukumu dhidi ya Yerusalemu haiwezi kuepukika (12-23)

    • Noa, Danieli, na Ayubu waliokuwa waadilifu (14, 20)

14  Na baadhi ya wazee wa Israeli wakaja na kuketi mbele yangu.+  Kisha neno la Yehova likanijia likisema:  “Mwana wa binadamu, wanaume hawa wameazimia kufuata sanamu zao zinazochukiza,* nao wameweka kikwazo kinachowafanya watu watende dhambi. Je, niwaruhusu waniombe ushauri?+  Sasa zungumza nao uwaambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ikiwa Mwisraeli ameazimia kufuata sanamu zake zinazochukiza na kuweka kikwazo kinachowafanya watu watende dhambi kisha anaenda kuomba ushauri kutoka kwa nabii, mimi, Yehova, nitamjibu ipasavyo kulingana na sanamu zake nyingi zinazochukiza.  Kwa maana nitatia hofu katika mioyo ya watu wa nyumba ya Israeli* kwa sababu wote wameniacha na kuzifuata sanamu zao zinazochukiza.”’+  “Basi waambie watu wa nyumba ya Israeli, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Rudini na mziache sanamu zenu zinazochukiza na mgeuze nyuso zenu kutoka kwenye mazoea yenu yanayochukiza.+  Kwa maana ikiwa Mwisraeli yeyote au mgeni anayeishi Israeli anajitenga nami na kuazimia kufuata sanamu zake zinazochukiza na kuweka kikwazo kinachowafanya watu watende dhambi, kisha aje kuomba ushauri kutoka kwa nabii wangu,+ mimi, Yehova, nitamjibu mimi mwenyewe.  Nitamkataa* mtu huyo na kumfanya awe ishara ya kuonya na methali, nami nitamwangamiza kabisa kutoka kati ya watu wangu;+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”’  “‘Lakini nabii akipumbazwa naye atoe ushauri, ni mimi, Yehova, ambaye nimempumbaza nabii huyo.+ Ndipo nitakapounyoosha mkono wangu dhidi yake na kumwangamiza kutoka kwa watu wangu Waisraeli. 10  Nao lazima wataibeba hatia yao; hatia ya mwenye kuomba ushauri itakuwa sawa na hatia ya nabii, 11  ili watu wa nyumba ya Israeli waache kutangatanga mbali nami na kuacha kujichafua kwa makosa yao yote. Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 12  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 13  “Mwana wa binadamu, ikiwa nchi itanitendea dhambi kwa kukosa uaminifu, nitaunyoosha mkono wangu dhidi yake na kufanya chakula kisipatikane*+ na kuleta njaa kali nchini+ na kuwaangamiza kabisa wanadamu na wanyama kutoka humo.”+ 14  “‘Hata ikiwa watu hawa watatu—Noa,+ Danieli,+ na Ayubu+—wangekuwa humo, wangejiokoa wao wenyewe* tu kwa sababu ya uadilifu wao,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 15  “‘Au nikifanya wanyama hatari wa mwituni wapite kotekote nchini na kuwaua watu wengi* na kuifanya nchi iwe ukiwa hivi kwamba hakuna mtu atakayepita humo kwa sababu ya wanyama wa mwituni,+ 16  kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘hata ikiwa watu hao watatu wangekuwa humo, hawangewaokoa wana wao wala mabinti wao; wangejiokoa wao wenyewe tu, na nchi ingekuwa ukiwa.’” 17  “‘Au kama nikileta upanga dhidi ya nchi hiyo+ na kusema: “Upanga na upite kotekote nchini,” na kuwaangamiza wanadamu na wanyama kutoka humo,+ 18  hata ikiwa watu hao watatu wangekuwa humo, kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘hawangewaokoa wana wao wala mabinti wao; wangejiokoa wao wenyewe tu.’” 19  “‘Au nikileta ugonjwa hatari katika nchi hiyo+ na kuimwagia ghadhabu yangu kwa umwagaji wa damu ili kuwaangamiza wanadamu na wanyama kutoka humo, 20  hata ikiwa Noa,+ Danieli,+ na Ayubu+ wangekuwa humo, kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘hawangewaokoa wana wao wala mabinti wao; wangejiokoa wao wenyewe tu kwa sababu ya uadilifu wao.’”+ 21  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Ndivyo itakavyokuwa nitakapoleta adhabu zangu nne*+—upanga, njaa kali, wanyama hatari wa mwituni, na ugonjwa hatari+—dhidi ya jiji la Yerusalemu ili kuwaangamiza kabisa wanadamu na wanyama kutoka humo.+ 22  Lakini, baadhi ya watu waliobaki humo wataponyoka na kutolewa nje,+ wana na mabinti. Wanakuja kwenu, nanyi mtakapoona njia zao na matendo yao, kwa hakika mtafarijiwa kuhusiana na msiba ambao nilileta dhidi ya Yerusalemu, kuhusu kila jambo ambalo nilitenda dhidi ya jiji hilo.’” 23  “‘Watawafariji mtakapoona njia zao na matendo yao, nanyi mtajua kwamba sikutenda bila sababu yale niliyolazimika kulitendea jiji hilo,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Tnn., “nitawakamata watu wa nyumba ya Israeli katika moyo wao.”
Tnn., “Nitaukaza uso wangu dhidi ya.”
Tnn., “kuvunja fito zake za mikate.” Labda ni fito zilizotumiwa kuhifadhia mikate.
Au “wangeokoa nafsi zao.”
Au “na kuwaua watoto.”
Au “matendo yangu manne ya hukumu yanayodhuru.”