Ezekieli 16:1-63

  • Upendo wa Mungu kwa Yerusalemu (1-63)

    • Apatikana kama mtoto aliyeachwa (1-7)

    • Mungu ampamba na kufanya agano la ndoa pamoja naye (8-14)

    • Akosa kuwa mwaminifu (15-34)

    • Aadhibiwa kama mwanamke mzinzi (35-43)

    • Alinganishwa na Samaria na Sodoma (44-58)

    • Mungu akumbuka agano lake (59-63)

16  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, lijulishe Yerusalemu mazoea yake yanayochukiza.+  Nawe utaliambia, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anakuambia hivi Yerusalemu: “Asili yako na kuzaliwa kwako ni katika nchi ya Mkanaani. Baba yako alikuwa Mwamori,+ na mama yako alikuwa Mhiti.+  Kuhusu kuzaliwa kwako, siku uliyozaliwa, kitovu chako hakikukatwa, hukuoshwa kwa maji uwe safi, hukusuguliwa kwa chumvi, wala hukufungwa kwa vitambaa.  Hakuna mtu aliyekusikitikia vya kutosha hivi kwamba akakufanyia lolote kati ya mambo hayo. Hakuna mtu aliyekuhurumia. Badala yake, ulitupwa uwanjani kwa sababu ulichukiwa* siku uliyozaliwa.  “‘“Nilipokuwa nikipita, nilikuona ukitupatupa mateke katika damu yako, nawe ulipokuwa umelala hapo katika damu yako, nikasema: ‘Endelea kuishi!’ Naam, nilikuambia ukiwa umelala hapo katika damu yako: ‘Endelea kuishi!’  Nilikufanya uwe umati mkubwa sana, kama mimea inayochipuka shambani, nawe ukakua, ukakomaa na kuvaa mapambo bora sana. Matiti yako yakakomaa, na nywele zako zikakua; lakini bado ulikuwa uchi, bila chochote.”’  “‘Nilipokuwa nikipita na kukuona, nilitambua kwamba ulikuwa na umri wa kutosha kuonyeshwa upendo. Basi nikatandaza vazi langu juu yako+ na kuufunika uchi wako, nami nikaapa na kufanya agano pamoja nawe,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nawe ukawa wangu.  Isitoshe, nilikuosha kwa maji na kuiondoa damu iliyokuwa juu yako na kukupaka mafuta.+ 10  Kisha nikakuvika vazi lililotariziwa na kukupa viatu vya ngozi bora* na kukufunika kwa kitani bora, nami nikakuvika mavazi ya bei ghali. 11  Nikakupamba kwa vito na kutia bangili kwenye mikono yako na mkufu shingoni mwako. 12  Pia nikatia pete ya puani kwenye pua yako na vipuli kwenye masikio yako na taji maridadi kwenye kichwa chako. 13  Ukaendelea kujipamba kwa dhahabu na fedha, na mavazi yako yalikuwa kitani bora, kitambaa cha bei ghali, na vazi lililotariziwa. Ulikula unga laini, asali, na mafuta, nawe ukawa mrembo kupindukia,+ ukastahili kuwa malkia.’”* 14  “‘Sifa zako zikaanza* kuenea kati ya mataifa+ kwa sababu ya urembo wako, kwa maana urembo wako ulikuwa kamili kwa sababu niliweka fahari yangu mwenyewe juu yako,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 15  “‘Lakini ulianza kuutumaini urembo wako,+ nawe ukawa kahaba kwa sababu ya sifa zako.+ Ulimmwagia kila mpita-njia matendo yako ya ukahaba,+ na urembo wako ukawa wake. 16  Ukachukua baadhi ya mavazi yako na kutengeneza mahali pa juu penye rangi mbalimbali ambapo ulifanyia ukahaba+—mambo hayo hayapaswi kufanywa, wala hayapaswi kutendeka kamwe. 17  Pia, ulichukua vito vyako maridadi vilivyotengenezwa* kwa dhahabu na fedha ambayo nilikupatia nawe ukajitengenezea sanamu za kiume na kufanya nazo ukahaba.+ 18  Nawe ukachukua mavazi yako yaliyotariziwa na kuzifunika,* nawe ukazitolea mafuta yangu na uvumba wangu.+ 19  Na mkate wangu niliokuwa nimekupa—uliotengenezwa kwa unga laini, mafuta, na asali niliyokupa ule—uliutoa pia kwa sanamu hizo ukiwa harufu inayopendeza.*+ Hivyo ndivyo ilivyokuwa,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 20  “‘Uliwachukua wana na mabinti wako uliokuwa umenizalia,+ nawe ukawatoa dhabihu kwa sanamu hizo ili waangamizwe+—je, matendo yako ya ukahaba hayajatosha? 21  Uliwachinja wanangu, nawe ukawatoa wawe dhabihu kwa kuwateketeza* motoni.+ 22  Ulipokuwa ukitenda mambo yako yote yanayochukiza na matendo ya ukahaba, hukukumbuka siku za ujana wako ulipokuwa uchi, bila chochote, ukitupatupa mateke katika damu yako. 23  Baada ya uovu wako wote, ole, ole wako,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 24  ‘Ulijijengea kilima na kujitengenezea mahali pa juu katika kila kiwanja cha jiji. 25  Ulijenga mahali pako pa juu sehemu zinazoonekana zaidi za kila barabara, nawe ukaugeuza urembo wako kuwa kitu kinachochukiza kwa kuutoa mwili wako* kwa kila mpita-njia,+ nawe ukazidisha matendo yako ya ukahaba.+ 26  Ulifanya ukahaba na wana wa Misri,+ majirani wako wenye uchu,* nawe ulinikasirisha kwa matendo yako yasiyohesabika ya ukahaba. 27  Sasa nitauleta mkono wangu dhidi yako na kupunguza posho yako ya chakula+ na kukutia mikononi mwa mapenzi* ya wanawake wanaokuchukia,+ mabinti wa Wafilisti, wanawake walioshtushwa na mwenendo wako mchafu.+ 28  “‘Kwa kuwa hungeweza kutoshelezwa, ulifanya pia ukahaba na wana wa Ashuru,+ lakini baada ya kufanya nao ukahaba, bado hukutosheka. 29  Basi ukazidisha ukahaba wako kuelekea nchi ya wafanyabiashara* na kuelekea kwa Wakaldayo,+ lakini bado hukutosheka. 30  Jinsi moyo wako ulivyokuwa mgonjwa,’* asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘ulipofanya mambo hayo yote, ukitenda kama kahaba mwenye ushupavu!+ 31  Lakini ulipojenga kilima chako katika sehemu zinazoonekana zaidi za kila barabara na kutengeneza mahali pako pa juu katika kila kiwanja cha jiji, hukuwa kama kahaba, kwa sababu ulikataa malipo yoyote. 32  Wewe ni mke mzinzi anayewachukua wageni badala ya mume wake mwenyewe!+ 33  Watu huwapa zawadi makahaba wote,+ lakini wewe ndiye unayewapa zawadi wote walio na uchu kukuelekea,+ nawe unawapa rushwa ili waje kwako kutoka pande zote ili kufanya ukahaba.+ 34  Wewe ni tofauti kabisa na wanawake wengine wanaofanya ukahaba. Hakuna mtu anayefanya ukahaba kama wewe! Unawalipa watu, nao hawakulipi. Unatenda tofauti kabisa.’ 35  “Kwa hiyo, ewe kahaba,+ sikia neno la Yehova. 36  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu uchu wako umemwagwa na uchi wako umefunuliwa ulipokuwa ukifanya ukahaba na wapenzi wako na sanamu zako zote zinazoudhi na kuchukiza*+ ambazo hata ulizitolea dhabihu ya damu ya wanao,+ 37  kwa hiyo ninawakusanya pamoja wapenzi wote ambao umewapa raha, wote uliowapenda na wote uliowachukia. Nitawakusanya pamoja dhidi yako kutoka pande zote na kuwafunulia uchi wako, nao watakuona ukiwa uchi kabisa.+ 38  “‘Nami nitakuadhibu kwa hukumu wanayostahili wanawake wazinzi+ na wanawake wanaomwaga damu,+ na damu yako itamwagwa kwa ghadhabu na wivu.+ 39  Nitakutia mikononi mwao, nao watavibomoa vilima vyako, na mahali pako pa juu patabomolewa;+ nao watakuvua mavazi yako+ na kuchukua vito vyako* maridadi+ na kukuacha uchi, bila chochote. 40  Wataleta umati dhidi yako,+ nao watakupiga mawe+ na kukuchinja kwa panga zao.+ 41  Wataziteketeza nyumba zako kwa moto+ na kutekeleza hukumu dhidi yako mbele ya macho ya wanawake wengi; nami nitakomesha ukahaba wako,+ nawe utaacha kutoa malipo. 42  Nitaitosheleza ghadhabu yangu dhidi yako,+ na hasira yangu itakuacha;+ nami nitatulia na sitaendelea kukasirika.’ 43  “‘Kwa sababu hukuzikumbuka siku za ujana wako+ nawe umenikasirisha kwa kufanya mambo hayo yote, sasa nitakuletea madhara ya njia zako juu ya kichwa chako mwenyewe,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nawe hutaendelea tena na mwenendo wako mchafu na mazoea yako yote yanayochukiza. 44  “‘Tazama! Kila mtu anayetumia methali ataitumia methali hii kukuhusu: “Kama mama alivyo, ndivyo binti alivyo!”+ 45  Wewe ni binti ya mama yako, aliyemdharau mume wake na watoto wake. Nawe ni dada ya dada zako, waliowadharau waume zao na watoto wao. Mama yenu alikuwa Mhiti, na baba yenu alikuwa Mwamori.’”+ 46  “‘Dada yako mkubwa ni Samaria,+ anayekaa upande wako wa kaskazini* pamoja na mabinti zake,*+ na dada yako mdogo, anayekaa upande wako wa kusini,* ni Sodoma+ pamoja na mabinti zake.+ 47  Hukutembea tu katika njia zao na kufuata mazoea yao yanayochukiza, bali pia kwa muda mfupi mwenendo wako ulikuwa mpotovu hata zaidi kuliko mwenendo wao.+ 48  Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘Sodoma dada yako na mabinti zake hawajatenda yale ambayo wewe na mabinti zako mmetenda. 49  Tazama! Hili ndilo lililokuwa kosa la Sodoma dada yako: Yeye pamoja na mabinti zake+ walikuwa na kiburi,+ nao walikuwa na chakula kingi+ na utulivu mwingi;+ hata hivyo hawakuwasaidia walioteseka na maskini.+ 50  Waliendelea kuwa na majivuno+ na kuzidi kutenda mambo yanayochukiza machoni pangu,+ basi nikalazimika kuwaondoa.+ 51  “‘Samaria+ hata hakutenda nusu ya dhambi zako. Uliendelea kuzidisha mazoea yako yanayochukiza kuliko yao, hivi kwamba dada zako wakaonekana kuwa waadilifu kwa sababu ya mazoea yako yote yanayochukiza.+ 52  Lazima sasa ubebe fedheha yako kwa kuwa umetetea* tabia za dada zako. Kwa sababu ya dhambi yako ya kutenda mambo yanayochukiza kuliko wao, wao ni waadilifu kuliko wewe. Basi sasa, na uaibike na kubeba fedheha ya kuwafanya dada zako waonekane kuwa waadilifu.’ 53  “‘Nami nitawakusanya watu wao waliotekwa, watu waliotekwa wa Sodoma pamoja na mabinti zake na watu waliotekwa wa Samaria pamoja na mabinti zake; na pamoja nao nitawakusanya pia watu wako waliotekwa,+ 54  ili uibebe fedheha yako; nawe utafedheheka kwa sababu ya yale ambayo umefanya kwa kuwafariji. 55  Na dada zako wewe mwenyewe, Sodoma na mabinti zake, watarudia hali yao ya mwanzoni, na Samaria na mabinti zake watarudia hali yao ya mwanzoni, na wewe pamoja na mabinti zako mtarudia hali yenu ya mwanzoni.+ 56  Dada yako Sodoma hakustahili kutajwa nawe katika siku ya fahari yako, 57  kabla uovu wako mwenyewe haujafunuliwa.+ Sasa mabinti wa Siria na majirani zake wanakushutumu, na mabinti wa Wafilisti,+ wote wanaokuzunguka, wanakudharau. 58  Utayabeba madhara ya mwenendo wako mchafu na mazoea yako yanayochukiza,’ asema Yehova.” 59  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Sasa nitakutendea kama ulivyotenda,+ kwa maana ulikidharau kiapo kwa kuvunja agano langu.+ 60  Lakini mimi mwenyewe nitalikumbuka agano nililofanya pamoja nawe katika siku za ujana wako, nami nitafanya agano la kudumu pamoja nawe.+ 61  Utakumbuka tabia yako na kufedheheka+ utakapowakaribisha dada zako, waliokuzidi umri na pia walio na umri mdogo kuliko wako, nami nitakupa wawe mabinti zako, lakini si kwa sababu ya agano lako.’ 62  “‘Na mimi mwenyewe nitafanya agano langu pamoja nawe; nawe utalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova. 63  Kisha utakumbuka na kuaibika sana usiweze kuufungua mdomo wako kwa sababu ya kufedheheka,+ nitakapofunika dhambi zako licha ya mambo yote ambayo umefanya,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Au “nafsi yako ilichukiwa.”
Au “ngozi ya sili.”
Au “ukastahili cheo cha kifalme.”
Au “Jina lako likaanza.”
Au “mapambo yako maridadi yaliyotengenezwa.”
Yaani, sanamu za kiume.
Au “inayotuliza.”
Tnn., “kuwapitisha.”
Tnn., “kupanua miguu yako.”
Tnn., “majirani wako wenye mwili mkubwa.”
Au “nafsi.”
Tnn., “nchi ya Kanaani.”
Au “Jinsi moyo wako ulivyokuwa dhaifu.” Au labda, “Jinsi nilivyojawa na ghadhabu dhidi yako.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Au “mapambo yako.”
Labda ni miji ya jiji hilo.
Tnn., “upande wako wa kulia.”
Tnn., “upande wako wa kushoto.”
Au “umeunga mkono.”