Ezekieli 17:1-24

  • Kitendawili cha tai wawili na mzabibu (1-21)

  • Chipukizi changa litakuwa mwerezi mkubwa (22-24)

17  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, tega kitendawili na useme methali kuhusu watu wa nyumba ya Israeli.+  Nawe utasema, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Tai mkubwa,+ mwenye mabawa makubwa, na manyoya marefu, na aliyejaa manyoya yenye rangi mbalimbali, alikuja Lebanoni+ na kuchukua sehemu ya juu ya mwerezi.+  Aliling’oa chipukizi lake lililo juu zaidi na kulileta kwenye nchi ya wafanyabiashara* na kuliweka katika jiji la wafanyabiashara.+  Kisha akachukua baadhi ya mbegu za nchi hiyo+ na kuziweka katika shamba lenye rutuba. Akaipanda mbegu moja kama mti wa mvinje kando ya maji mengi.  Basi ikachipuka na kuwa mzabibu mfupi, unaotambaa,+ wenye majani yanayotazama ndani na mizizi inayokua chini yake. Kwa hiyo ukawa mzabibu, ukatokeza machipukizi na kuota matawi.+  “‘“Akaja tai mwingine mkubwa,+ mwenye mabawa makubwa na manyoya makubwa.+ Kisha mzabibu huo ukasambaza mizizi yake kwa bidii kumwelekea, mbali na bustani mahali ambapo ulipandwa, nao ukaelekeza majani yake kwake ili aumwagilie maji.+  Ulikuwa tayari umepandwa katika shamba zuri karibu na maji mengi, ili utokeze matawi, uzae matunda, na uwe mzabibu mkubwa.”’+  “Sema, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Je, utasitawi? Je, mtu fulani hataing’oa mizizi yake+ na kufanya matunda yake yaoze na machipukizi yake yanyauke?+ Utakauka sana hivi kwamba hautahitaji mkono wenye nguvu wala watu wengi ili kuung’oa pamoja na mizizi yake. 10  Ingawa umepandikizwa, je, utasitawi? Je, hautakauka kabisa, utakapopigwa na upepo wa mashariki? Utakauka katika bustani ulikochipuka.”’” 11  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 12  “Tafadhali iambie nyumba ya uasi, ‘Je, hamtambui maana ya mambo haya?’ Sema, ‘Tazama! Mfalme wa Babiloni alikuja Yerusalemu, akamchukua mfalme wake na wakuu wake na kurudi pamoja nao Babiloni.+ 13  Isitoshe, alimchukua mmoja aliyekuwa wa uzao wa*+ kifalme, akafanya naye agano na kumwapisha.+ Kisha akawachukua watu mashuhuri wa nchi,+ 14  ili ufalme huo ushushwe, usiweze kuinuka, ili uendelee kuwapo ikiwa tu utashika agano lake.+ 15  Lakini mwishowe mfalme huyo alimwasi+ kwa kutuma wajumbe wake Misri ili apate farasi+ na jeshi kubwa kutoka huko.+ Je, atafanikiwa? Je, yule anayefanya mambo hayo ataponyoka adhabu? Je, anaweza kuvunja agano na bado aponyoke?’+ 16  “‘“Kwa hakika kama ninavyoishi,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, “atafia huko Babiloni, mahali ambapo anaishi mfalme* aliyemweka* kuwa mfalme, ambaye alikidharau kiapo chake na ambaye alilivunja agano lake.+ 17  Na lile jeshi kubwa na wanajeshi wengi wa Farao hawatamsaidia kamwe vitani,+ wakati boma la kuzingira litakapojengwa na kuta za kuzingira zitakapojengwa ili kuangamiza uhai wa* watu wengi. 18  Amedharau kiapo na kuvunja agano. Hata ingawa alitoa ahadi,* amefanya mambo hayo yote, naye hataponyoka.”’ 19  “‘Kwa hiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa hakika kama ninavyoishi, nitamletea juu ya kichwa chake madhara ya kudharau kiapo changu+ na kuvunja agano langu. 20  Nitautandaza wavu wangu juu yake, naye atakamatwa katika wavu wangu wa kuwindia.+ Nitamleta Babiloni na kumhukumu huko kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu alionitendea.+ 21  Wakimbizi wote kati ya wanajeshi wake watauawa kwa upanga, na wale wanaobaki watatawanyika kila upande.*+ Ndipo mtakapolazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimesema.”’+ 22  “‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitachukua chipukizi kutoka katika kilele cha mwerezi mkubwa+ na kulipanda, kutoka juu ya matawi yake nitakata chipukizi changa,+ nami mwenyewe nitalipanda juu ya mlima mrefu na ulio juu sana.+ 23  Nitalipanda juu ya mlima mrefu wa Israeli; na matawi yake yatakua, nalo litazaa matunda na kuwa mwerezi mkubwa. Na ndege wa kila aina wataishi chini yake na kukaa kwenye kivuli cha majani yake. 24  Na miti yote ya shambani italazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimeushusha ule mti mrefu na kuukweza ule mti mfupi;+ nimeukausha ule mti mbichi na kuufanya mti uliokauka usitawi.+ Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema nami nimefanya hivyo.”’”

Maelezo ya Chini

Tnn., “nchi ya Kanaani.”
Tnn., “mbegu ya.”
Yaani, Nebukadneza.
Yaani, Sedekia.
Au “nafsi za.”
Tnn., “aliutoa mkono wake.”
Tnn., “kwa kila upepo.”