Ezekieli 18:1-32

  • Kila mtu anawajibika kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe (1-32)

    • Nafsi inayotenda dhambi itakufa (4)

    • Mwana hatalipia dhambi ya baba yake (19, 20)

    • Sifurahishwi na kifo cha mtu mwovu (23)

    • Toba huhifadhi uhai (27, 28)

18  Na neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Methali hii mnayoisema katika nchi ya Israeli inamaanisha nini, ‘Akina baba wamekula zabibu chachu, lakini meno ya wana ndiyo yanayotiwa ukakasi’?+  “‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘hamtaendelea kuutaja msemo huo katika Israeli.  Tazama! Nafsi zote—ni zangu.* Kama nafsi ya baba ilivyo yangu ndivyo ilivyo nafsi ya mwana—ni zangu. Nafsi* inayotenda dhambi ndiyo itakayokufa.*  “‘Ikiwa mtu ni mwadilifu na anatenda haki na uadilifu,  naye hali dhabihu zinazotolewa kwa sanamu kwenye milima;+ hazitumaini sanamu zinazochukiza* za watu wa nyumba ya Israeli; hamnajisi mke wa jirani yake+ au kulala na mwanamke aliye katika hedhi;+  hamtesi mtu yeyote,+ bali hurudisha rehani aliyopewa na mtu mwenye deni lake;+ hamnyang’anyi yeyote,+ bali humpa mwenye njaa chakula chake+ na kumfunika kwa vazi aliye uchi;+  hatozi faida wala kutoza riba,+ lakini anajizuia asitende isivyo haki;+ anatekeleza haki ya kweli kati ya mtu na mwenzake;+  naye anaendelea kutembea katika amri zangu na kushika sheria zangu* ili atende kwa uaminifu. Mtu huyo ni mwadilifu na kwa hakika ataendelea kuishi,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 10  “‘Lakini ikiwa yeye ni baba ya mwana ambaye ni mnyang’anyi+ au muuaji*+ au anayefanya lolote kati ya mambo haya mengine 11  (ingawa baba yake hajafanya lolote kati ya mambo hayo)—anakula dhabihu zilizotolewa kwa sanamu kwenye milima, anamnajisi mke wa jirani yake, 12  anawatesa wenye uhitaji na maskini,+ anawanyang’anya watu vitu vyao, harudishi kitu kilichowekwa rehani; anatumaini sanamu zinazochukiza,+ anajihusisha na mazoea yanayochukiza,+ 13  ametoza riba na kutoza faida+—basi mwana huyo hataendelea kuishi. Kwa sababu ya mambo hayo yote yanayochukiza aliyofanya, kwa hakika atauawa. Damu yake mwenyewe itakuwa juu yake. 14  “‘Lakini ikiwa baba ana mwana anayeona dhambi zote anazofanya baba yake, na ingawa anaziona, hafanyi mambo kama hayo, 15  hali dhabihu zilizotolewa kwa sanamu kwenye milima; hazitumaini sanamu zinazochukiza za watu wa nyumba ya Israeli; hamnajisi mke wa jirani yake; 16  hamtesi mtu yeyote; habaki na kitu kilichowekwa rehani; hamnyang’anyi mtu kitu chochote; chakula chake mwenyewe anampa mwenye njaa na kumfunika kwa vazi aliye uchi; 17  anaepuka kuwakandamiza maskini; hatozi riba wala kutoza faida; naye anafuata sheria zangu;* ametembea katika amri zangu. Mtu huyo hatakufa kwa sababu ya kosa la baba yake. Kwa hakika ataendelea kuishi. 18  Lakini kwa kuwa baba yake alifanya ulaghai, akamnyang’anya ndugu yake, na kufanya mambo mabaya kati ya watu wake, atakufa kwa sababu ya kosa lake. 19  “‘Nanyi mtasema: “Kwa nini mwana hana hatia kwa sababu ya kosa la baba yake?” Kwa kuwa mwana ametenda mambo ya haki na ya uadilifu, amezishika amri zangu zote na kuzitenda, kwa hakika ataendelea kuishi.+ 20  Nafsi inayotenda dhambi ndiyo itakayokufa.*+ Mwana hatakuwa na hatia kwa sababu ya kosa la baba yake, na baba hatakuwa na hatia kwa sababu ya kosa la mwanawe. Mwadilifu atathawabishwa kwa sababu ya uadilifu wake mwenyewe, na mwovu ataadhibiwa kwa sababu ya uovu wake mwenyewe.+ 21  “‘Sasa mtu mwovu akiziacha dhambi zote alizofanya na kushika amri zangu na kutenda mambo ya haki na ya uadilifu, kwa hakika ataendelea kuishi. Hatakufa.+ 22  Hatahukumiwa kwa kosa lolote alilotenda.*+ Ataendelea kuishi kwa kutenda uadilifu.’+ 23  “‘Je, ninafurahia hata kidogo kifo cha mtu mwovu?’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Je, sipendelei kwamba aziache njia zake naye aendelee kuishi?’+ 24  “‘Lakini mtu mwadilifu akiacha uadilifu wake na kutenda kosa,* na kufanya mambo yote yanayochukiza wanayofanya waovu, je, ataishi? Hakuna jambo lolote litakalokumbukwa kati ya matendo ya uadilifu aliyotenda.+ Atakufa kwa sababu ya ukosefu wake wa uaminifu na dhambi aliyotenda.+ 25  “‘Lakini mtasema: “Njia ya Yehova si ya haki.”+ Tafadhali sikilizeni, enyi watu wa nyumba ya Israeli! Je, ni njia yangu isiyo ya haki?+ Je, si njia zenu ambazo si za haki?+ 26  “‘Mtu mwadilifu akiuacha uadilifu wake na kutenda kosa, naye afe kwa sababu ya kosa hilo, atakufa kwa sababu ya kosa lake mwenyewe. 27  “‘Na mtu mwovu akiacha uovu ambao ametenda na kuanza kutenda mambo ya haki na ya uadilifu, atauhifadhi uhai wake* mwenyewe.+ 28  Akitambua na kuacha makosa yote ambayo ametenda, kwa hakika ataendelea kuishi. Hatakufa. 29  “‘Lakini watu wa nyumba ya Israeli watasema: “Njia ya Yehova si ya haki.” Je, ni kweli kwamba ni njia zangu ambazo si za haki, enyi watu wa nyumba ya Israeli?+ Je, si njia zenu ambazo si za haki?’ 30  “‘Kwa hiyo, nitamhukumu kila mmoja wenu kulingana na njia zake,+ enyi watu wa nyumba ya Israeli,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Acheni, naam, acheni kabisa makosa yenu yote, ili yasiwe kikwazo kinachowaletea hatia. 31  Jiondoleeni makosa yenu yote mliyofanya+ na mjipatie* moyo mpya na roho mpya,+ kwa nini mfe,+ enyi watu wa nyumba ya Israeli?’ 32  “‘Mimi sifurahii kifo cha mtu yeyote,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Kwa hiyo geukeni na kuishi.’”+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Au “Mtu anayetenda dhambi ndiye atakayekufa.”
Au “Uhai wote—ni wangu.” Angalia Kamusi.
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Tnn., “mtu anayemwaga damu.”
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Au “Mtu anayetenda dhambi ndiye atakayekufa.”
Tnn., “Kosa lolote alilotenda halitakumbukwa.”
Au “kutenda jambo lisilo la haki.”
Au “ataihifadhi nafsi yake.” Angalia Kamusi.
Tnn., “mjitengenezee.”