Ezekieli 20:1-49

  • Historia ya uasi wa Waisraeli (1-32)

  • Ahadi ya kurudishwa kwa Waisraeli (33-44)

  • Unabii dhidi ya kusini (45-49)

20  Katika mwaka wa saba, mwezi wa tano, siku ya kumi ya mwezi huo, baadhi ya wazee wa Israeli walikuja na kuketi mbele yangu ili kuniomba ushauri kutoka kwa Yehova.  Ndipo neno la Yehova likanijia likisema:  “Mwana wa binadamu, zungumza na wazee wa Israeli uwaambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Je, mnakuja kuniomba ushauri? ‘Kwa hakika kama ninavyoishi, sitawajibu,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”’  “Je, uko tayari kuwahukumu?* Mwana wa binadamu je, uko tayari kuwahukumu? Wajulishe mambo yanayochukiza ambayo mababu zao walifanya.+  Waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Siku nilipoichagua Israeli,+ pia niliuapia* uzao wa* nyumba ya Yakobo, na kujijulisha kwao nchini Misri.+ Naam, niliwaapia na kusema, ‘Mimi ni Yehova Mungu wenu.’  Siku hiyo niliapa kwamba nitawatoa nchini Misri na kuwapeleka katika nchi niliyokuwa nimeichunguza* kwa ajili yao, nchi inayotiririka maziwa na asali.+ Nchi hiyo ilikuwa nzuri sana kuliko* nchi zote.  Kisha nikawaambia, ‘Lazima kila mmoja wenu atupe vitu vinavyochukiza vilivyo mbele ya macho yake; msijitie unajisi kwa sanamu zinazochukiza* za Misri.+ Mimi ni Yehova Mungu wenu.’+  “‘“Lakini wakaniasi nao hawakutaka kunisikiliza. Hawakuvitupa vitu vinavyochukiza vilivyokuwa mbele yao, nao walikataa kuziacha sanamu zinazochukiza za Misri.+ Basi nikaahidi kuwamwagia ghadhabu yangu na kuwaletea hasira yangu yote nchini Misri.  Lakini nilichukua hatua kwa ajili ya jina langu ili lisichafuliwe mbele ya mataifa ambamo waliishi.+ Nilijijulisha kwao* mbele ya mataifa hayo nilipowatoa* nchini Misri.+ 10  Kwa hiyo nikawatoa nchini Misri na kuwaongoza kuingia nyikani.+ 11  “‘“Kisha nikawapa amri zangu na kuwajulisha sheria zangu,*+ ili mtu anayezifuata apate uzima kupitia hizo.+ 12  Pia nikawapa sabato zangu,+ ziwe ishara kati yangu nao,+ ili wajue kwamba mimi, Yehova, ndiye ninayewatakasa. 13  “‘“Lakini watu wa nyumba ya Israeli waliniasi nyikani.+ Hawakutembea katika amri zangu, nao wakakataa sheria zangu,* ambazo mtu akizifuata, atapata uzima kupitia hizo. Walizitia unajisi kabisa sabato zangu. Basi nikaahidi kuwamwagia ghadhabu yangu nyikani ili niwaangamize kabisa.+ 14  Nilichukua hatua kwa ajili ya jina langu mwenyewe ili lisichafuliwe mbele ya mataifa, walioona nikiwatoa* huko.+ 15  Pia nikawaapia wakiwa nyikani kwamba sitawapeleka katika nchi niliyowapa+—nchi inayotiririka maziwa na asali,+ nchi nzuri sana kuliko* nchi zote— 16  kwa sababu walizikataa sheria zangu* na hawakutembea katika amri zangu, nao wakazitia unajisi sabato zangu, kwa maana mioyo yao ilikuwa ikifuata sanamu zao zinazochukiza.+ 17  “‘“Lakini niliwasikitikia,* nami sikuwaharibu; sikuwaangamiza kabisa nyikani. 18  Niliwaambia wana wao nyikani,+ ‘Msitembee katika masharti ya mababu zenu+ wala kushika hukumu zao wala kujichafua kwa sanamu zao zinazochukiza. 19  Mimi ni Yehova Mungu wenu. Tembeeni katika amri zangu, na kuzishika sheria zangu,* na kuzifuata.+ 20  Nanyi zitakaseni sabato zangu,+ nazo zitakuwa ishara kati yangu nanyi ili mjue kwamba mimi ni Yehova Mungu wenu.’+ 21  “‘“Lakini wana hao wakaanza kuniasi.+ Hawakutembea katika amri zangu, nao hawakushika wala kufuata sheria zangu,* ambazo mtu akizifuata, atapata uzima kupitia hizo. Walizitia unajisi sabato zangu. Basi nikaahidi kuwamwagia ghadhabu yangu, na kuwaletea hasira yangu yote nyikani.+ 22  Lakini nilijizuia+ na kuchukua hatua kwa ajili ya jina langu mwenyewe,+ ili lisichafuliwe mbele ya mataifa, walioona nikiwatoa* huko. 23  Pia, niliwaapia nyikani kwamba nitawatawanya miongoni mwa mataifa na kuwatawanya katika nchi mbalimbali,+ 24  kwa sababu hawakufuata sheria zangu* na walikataa amri zangu,+ walizitia unajisi sabato zangu, nao wakafuata* sanamu zinazochukiza za mababu zao.+ 25  Pia, niliwaruhusu wafuate masharti ambayo hayakuwa mazuri na sheria* ambazo hazingewasaidia kupata uzima.+ 26  Nami nikawaacha watiwe unajisi kwa dhabihu zao wenyewe—walipomteketeza* motoni kila mzaliwa wa kwanza+—ili kuwafanya wawe ukiwa, ili wajue kwamba mimi ni Yehova.”’ 27  “Basi zungumza na watu wa nyumba ya Israeli, ewe mwana wa binadamu, nawe uwaambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa njia hii pia, mababu zenu walinikufuru kwa kunitendea kwa ukosefu wa uaminifu. 28  Niliwaleta katika nchi niliyoapa kwamba ningewapatia.+ Walipoona vilima vyote virefu na miti yenye majani mengi,+ walianza kutoa dhabihu zao na matoleo yao yanayochukiza. Walitoa harufu inayopendeza* ya dhabihu zao na kumwaga matoleo yao ya vinywaji hapo. 29  Basi nikawauliza, ‘Mahali hapa pa juu mnapoenda panamaanisha nini? (Bado panaitwa Mahali pa Juu mpaka leo hii.)’”’+ 30  “Sasa waambie watu wa nyumba ya Israeli, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Je, mnajichafua kama mababu zenu walivyofanya kwa kuzifuata sanamu zao zinazochukiza ili kufanya nazo ukahaba wa kiroho?+ 31  Na je, bado mnajichafua mpaka leo hii kwa kuzitolea dhabihu sanamu zenu zote zinazochukiza, mkiwateketeza* motoni wana wenu?+ Je, wakati huohuo ninapaswa kujibu maombi yenu, enyi watu wa nyumba ya Israeli?”’+ “‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘Sitajibu maombi yenu.+ 32  Na jambo mnalofikiria mnaposema, “Na tuwe kama mataifa, kama familia za nchi nyingine, wanaoabudu* miti na mawe,”+ jambo hilo halitatimia kamwe.’” 33  “‘Kwa hakika kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘Nitawatawala nikiwa mfalme kwa mkono wenye nguvu, kwa mkono ulionyooshwa, na kwa ghadhabu kali.+ 34  Kwa mkono wenye nguvu, kwa mkono ulionyooshwa, na kwa ghadhabu kali nitawatoa kati ya mataifa na kuwakusanya pamoja kutoka katika nchi ambazo mmetawanywa.+ 35  Nitawapeleka katika nyika ya mataifa na huko nitawahukumu uso kwa uso.+ 36  “‘Kama nilivyowahukumu mababu zenu katika nyika ya nchi ya Misri, ndivyo nitakavyowahukumu ninyi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 37  ‘Nitawafanya mpite chini ya fimbo ya mchungaji+ na kuwaleta chini ya wajibu wa* agano. 38  Lakini nitawaondoa waasi kati yenu na wale wanaonitendea dhambi.+ Kwa maana nitawatoa katika nchi wanayokaa wakiwa wageni, lakini hawataingia katika nchi ya Israeli;+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’ 39  “Nanyi, enyi watu wa nyumba ya Israeli, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kila mmoja wenu na aende kuziabudu sanamu zake zinazochukiza.+ Lakini baadaye ikiwa hamtanisikiliza, hamtaweza tena kulichafua jina langu takatifu kwa dhabihu zenu na kwa sanamu zenu zinazochukiza.’+ 40  “‘Kwa maana katika mlima wangu mtakatifu, kwenye mlima mrefu wa Israeli,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘ndiko watu wote wa nyumba ya Israeli, wote, watanitumikia nchini.+ Nitafurahishwa nao huko, nami nitadai mnipe michango yenu na matunda ya kwanza ya matoleo yenu, vitu vyenu vyote vitakatifu.+ 41  Kwa sababu ya harufu inayopendeza,* nitafurahishwa nanyi nitakapowatoa kati ya mataifa na kuwakusanya pamoja kutoka katika nchi ambazo mmetawanywa;+ nami nitatakaswa kati yenu mbele ya macho ya mataifa.’+ 42  “‘Nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova+ nitakapowapeleka katika nchi ya Israeli,+ katika nchi ambayo niliapa kwamba nitawapa mababu zenu. 43  Na huko mtakumbuka mwenendo wenu na matendo yenu yote ambayo mlijichafua kupitia hayo,+ nanyi mtajichukia* kwa sababu ya mambo yote mabaya mliyotenda.+ 44  Ndipo mtakapolazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakaposhughulika nanyi kwa ajili ya jina langu,+ si kulingana na mwenendo wenu mwovu au kulingana na matendo yenu yaliyopotoka, enyi watu wa nyumba ya Israeli,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 45  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 46  “Mwana wa binadamu, uelekeze uso wako upande wa eneo la kusini na utangaze kuelekea kusini, na uutabirie msitu wa uwanja wa kusini. 47  Uambie msitu wa kusini, ‘Sikia neno la Yehova. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ninawasha moto dhidi yako,+ nao utateketeza kila mti mbichi na kila mti uliokauka ndani yako. Moto huo unaowaka hautazimwa,+ nao utachoma kila uso, kuanzia kusini mpaka kaskazini. 48  Na kila mwili utaona* kwamba Mimi mwenyewe, Yehova, nimeuwasha moto, ili usizimwe.”’”+ 49  Nami nikasema: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Wanasema kunihusu, ‘Je, hazungumzi kwa vitendawili?’”*

Maelezo ya Chini

Au “kuwatangazia hukumu.”
Tnn., “niliinua mkono wangu kwa.”
Tnn., “mbegu ya.”
Au “nimeipeleleza.”
Au “pambo la.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Yaani, Waisraeli.
Yaani, Waisraeli.
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Yaani, Waisraeli.
Au “pambo la.”
Tnn., “waliyakataa maamuzi yangu ya hukumu.”
Tnn., “jicho langu liliwasikitikia.”
Tnn., “kuyashika maamuzi yangu ya hukumu.”
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Yaani, Waisraeli.
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Tnn., “macho yao yakafuata.”
Tnn., “maamuzi ya hukumu.”
Tnn., “walipompitisha.”
Au “inayotuliza.”
Tnn., “mkiwapitisha.”
Au “wanaohudumia; wanaotumikia.”
Tnn., “katika kifungo cha.”
Au “inayotuliza.”
Tnn., “mtazichukia nyuso zenu.”
Au “watu wote wataona.”
Au “methali?”