Ezekieli 21:1-32

  • Upanga wa hukumu wa Mungu wachomolewa (1-17)

  • Mfalme wa Babiloni kushambulia Yerusalemu (18-24)

  • Mkuu mwovu wa Israeli ataondolewa (25-27)

    • “Ulivue taji” (26)

    • “Mpaka yule aliye na haki ya kisheria atakapokuja” (27)

  • Upanga utawashambulia Waamoni (28-32)

21  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, uelekeze uso wako Yerusalemu, na utoe tangazo dhidi ya mahali patakatifu, na utabiri dhidi ya nchi ya Israeli.  Iambie nchi ya Israeli, ‘Yehova anasema hivi: “Niko dhidi yako, nami nitauchomoa upanga wangu kutoka katika ala yake+ na kumkatilia mbali mwadilifu na mwovu kutoka kati yako.  Kwa kuwa nitamkatilia mbali kutoka kati yako mwadilifu na mwovu, upanga wangu utachomolewa kutoka katika ala yake dhidi ya wote wenye mwili,* kutoka kusini mpaka kaskazini.  Watu wote watalazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimeuchomoa upanga wangu kutoka katika ala yake. Hautarudi tena kamwe.”’+  “Nawe, mwana wa binadamu, lia kwa maumivu huku ukitetemeka,* naam, lia kwa uchungu mbele yao.+  Na wakikuuliza, ‘Kwa nini unalia kwa maumivu?’ utasema, ‘Kwa sababu ya habari fulani.’ Kwa maana hakika itakuja, na kila moyo utayeyuka kwa woga na kila mkono utalegea na kila roho itahuzunika na kila goti litadondosha maji.*+ ‘Tazama! Hakika itakuja—itatokea,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, tabiri, ‘Yehova anasema hivi: “Sema, ‘Upanga! Upanga+ umenolewa, nao umesuguliwa. 10  Umenolewa kwa ajili ya uchinjaji mkubwa; umesuguliwa ili uwakewake kama radi.’”’” “Je, hatupaswi kushangilia?” “‘Je, utakataa* fimbo ya ufalme ya mwana wangu mwenyewe,+ kama unavyokataa kila mti? 11  “‘Umetolewa ili usuguliwe na kushikwa mkononi. Upanga huo umenolewa na kusuguliwa, ili utiwe mkononi mwa muuaji.+ 12  “‘Mwana wa binadamu, lia kwa sauti na uomboleze,+ kwa maana upanga umekuja dhidi ya watu wangu; uko dhidi ya wakuu wote wa Israeli.+ Na upanga huo utawaangamiza pamoja na watu wangu. Kwa hiyo piga paja lako kwa huzuni. 13  Kwa maana uchunguzi umefanywa,+ na itakuwaje ikiwa upanga utaikataa fimbo ya ufalme? Haitaendelea* kuwapo,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 14  “Nawe, mwana wa binadamu, tabiri na upige makofi na kusema mara tatu, ‘Upanga!’ Ni upanga wa wale waliouawa, upanga wa uchinjaji mkubwa, unaowazunguka.+ 15  Mioyo yao itayeyuka kwa woga+ na wengi wataanguka katika malango ya jiji lao; nitawachinja kwa upanga. Naam, unawakawaka kama radi na umesuguliwa ili kuchinja! 16  Kata kwa makali upande wa kulia! Geukia upande wa kushoto! Nenda popote ambapo makali yako yanaelekezwa! 17  Nami pia nitapiga makofi na kuiridhisha ghadhabu yangu.+ Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema.” 18  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 19  “Nawe, mwana wa binadamu, chora njia mbili ambazo upanga wa mfalme wa Babiloni utapitia. Zote mbili zitaanzia nchi ileile, na ishara iwekwe* mahali ambapo barabara inatengana ili kuingia katika yale majiji mawili. 20  Unapaswa kuchora njia moja ili upanga ushambulie jiji la Raba+ la Waamoni, na njia nyingine ili ushambulie jiji la Yerusalemu+ lenye ngome, nchini Yuda. 21  Kwa maana mfalme wa Babiloni amesimama ili kufanya uaguzi* kwenye njia panda, mahali ambapo zile barabara mbili zinatengana. Anaitikisa mishale. Anaomba ushauri kutoka kwa sanamu* zake; anachunguza ini. 22  Uaguzi* ulio katika mkono wake wa kulia umeelekezwa Yerusalemu, ili kuweka mitambo ya kubomolea, ili kutoa agizo la kuchinja, ili kupiga kelele za vita, kuweka kwenye malango mitambo ya kubomolea, kujenga boma la kuzingira, kujenga ukuta wa kuzingira.+ 23  Lakini utaonekana kama uaguzi* wa uwongo machoni pa wale* waliowaapia.+ Lakini anakumbuka hatia yao naye atawakamata.+ 24  “Kwa hiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Mmefanya hatia yenu wenyewe ikumbukwe kwa kuyafunua makosa yenu na kufanya dhambi zenu zionekane katika matendo yenu yote. Kwa kuwa sasa mmekumbukwa, mtachukuliwa kwa nguvu.’* 25  “Lakini siku yako imefika, ewe uliyejeruhiwa vibaya, mkuu mwovu wa Israeli,+ wakati wa adhabu yako ya mwisho. 26  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kiondoe kilemba, na ulivue taji.+ Hili halitabaki kama lilivyo.+ Mwinue aliye chini,+ na umshushe aliye juu.+ 27  Nitaliharibu, nitaliharibu, nitaliharibu. Nalo halitakuwa la mtu yeyote mpaka yule aliye na haki ya kisheria atakapokuja,+ nami nitampa yeye.’+ 28  “Nawe, mwana wa binadamu, tabiri, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi kuhusu Waamoni na kuhusu matusi yao.’ Sema, ‘Upanga! Upanga umechomolewa kwa ajili ya kuchinja; umesuguliwa ili kunyafua na kuwakawaka kama radi. 29  Licha ya maono ya uwongo na uaguzi* wa uwongo kuwahusu ninyi, mtarundikwa juu ya waliouawa,* watu waovu ambao siku yao imefika, wakati wa adhabu yao ya mwisho. 30  Urudishe upanga katika ala yake. Nitakuhukumia mahali ulipoumbwa, katika nchi uliyozaliwa. 31  Nitakumwagia ghadhabu yangu. Nitakupulizia moto wa hasira yangu, nami nitakutia mikononi mwa watu wakatili, mafundi wa maangamizi.+ 32  Utakuwa kuni kwa ajili ya moto;+ damu yako mwenyewe itamwagwa nchini, nawe hutakumbukwa tena, kwa maana mimi mwenyewe, Yehova, nimesema.’”

Maelezo ya Chini

Au “watu wote.”
Tnn., “kiuno chako kikitetemeka.”
Yaani, watajikojolea kwa sababu ya woga.
Yaani, upanga wa Yehova.
Au “Fimbo ya ufalme haitaendelea.”
Tnn., “mkono uwekwe.”
Au “ubashiri.”
Tnn., “terafimu.”
Au “Ubashiri.”
Au “ubashiri.”
Yaani, wakaaji wa Yerusalemu.
Tnn., “kwa mkono.”
Au “ubashiri.”
Tnn., “juu ya shingo za waliouawa.”