Ezekieli 22:1-31

  • Yerusalemu, jiji lenye hatia ya damu (1-16)

  • Waisraeli ni kama takataka isiyo na thamani (17-22)

  • Viongozi na watu wa Israeli washutumiwa (23-31)

22  Na neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Nawe, mwana wa binadamu, je, uko tayari kulitangazia hukumu* jiji lenye hatia ya damu+ na kulijulisha mambo yake yote yanayochukiza?+  Nawe utasema, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ewe jiji linalomwaga damu+ ndani yake, ambalo wakati wake unakuja,+ linalotengeneza sanamu zinazochukiza* ili kujichafua,+  umwagaji wako wa damu umekufanya uwe na hatia,+ na sanamu zako zinazochukiza zimekufanya usiwe safi.+ Umeharakisha mwisho wa siku zako, na mwisho wa miaka yako umefika. Ndiyo sababu nitakufanya uwe kitu cha kushutumiwa na mataifa na kitu cha kudhihakiwa na nchi zote.+  Nchi zilizo karibu nawe na zile zilizo mbali nawe zitakudhihaki,+ wewe ambaye jina lako si safi na ambaye umejaa msukosuko.  Tazama! Kila mkuu wa Israeli aliye miongoni mwako anatumia mamlaka yake kumwaga damu.+  Ndani yako wanamdharau baba yao na mama yao.+ Wanampunja mkaaji mgeni, na kumtesa yatima na mjane.”’”+  “‘Unapadharau mahali pangu patakatifu, nawe unazitia unajisi sabato zangu.+  Ndani yako kuna wachongezi wanaokusudia kumwaga damu.+ Ndani yako wanakula dhabihu milimani na kuendeleza mwenendo mchafu ndani yako.+ 10  Ndani yako wanakidharau kitanda cha baba yao,*+ nao wanamnajisi mwanamke asiye safi aliye katika hedhi.+ 11  Ndani yako mwanamume mmoja anatenda kwa njia inayochukiza na mke wa jirani yake,+ mwingine anamnajisi binti mkwe wake mwenyewe kwa mwenendo mchafu,+ na mwingine anamnajisi dada yake, binti ya baba yake mwenyewe.+ 12  Ndani yako wanapokea rushwa ili kumwaga damu.+ Unakopesha kwa riba+ au kwa faida,* nawe unachukua pesa kwa nguvu kutoka kwa majirani zako.+ Naam, umenisahau kabisa,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 13  “‘Tazama! Ninapiga makofi kwa kuwa nimechukizwa na faida isiyo ya haki ambayo umepata na kwa sababu ya matendo yako ya kumwaga damu yaliyo ndani yako. 14  Je, ujasiri* wako utadumu na mikono yako itaendelea kuwa imara katika siku nitakapokuchukulia hatua?+ Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema, nami nitachukua hatua. 15  Nitakutawanya miongoni mwa mataifa na kukutawanya katika nchi hizo,+ nami nitakomesha uchafu wako.+ 16  Nawe utadharauliwa na mataifa, na utalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”+ 17  Na neno la Yehova likanijia tena likisema:⁠ 18  “Mwana wa binadamu, watu wa nyumba ya Israeli wamekuwa kama takataka isiyo na thamani kwangu. Wote ni shaba na bati na chuma na risasi katika tanuru. Wamekuwa takataka ya fedha.+ 19  “Kwa hiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa kama takataka isiyo na thamani,+ ninawakusanya pamoja ndani ya Yerusalemu. 20  Kama watu wanavyokusanya fedha na shaba na chuma na risasi na bati katika tanuru ili kuyapulizia moto madini hayo na kuyayeyusha, ndivyo nitakavyowakusanya ninyi kwa hasira yangu na kwa ghadhabu yangu, nami nitawapuliza na kuwayeyusha.+ 21  Nitawakusanya na kuwapuliza kwa moto wa ghadhabu yangu,+ nanyi mtayeyushwa ndani yake.+ 22  Kama fedha inavyoyeyushwa katika tanuru, ndivyo mtakavyoyeyushwa ndani yake; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimewamwagia ghadhabu yangu.’” 23  Na neno la Yehova likanijia tena likisema:⁠ 24  “Mwana wa binadamu, iambie hivi nchi hiyo: ‘Wewe ni nchi ambayo haitasafishwa au kunyeshewa mvua katika siku ya ghadhabu. 25  Ndani yake manabii wake wamepanga njama,+ kama simba anayenguruma akirarua mawindo.+ Wanawanyafua watu. Wanachukua hazina na vitu vyenye thamani. Wamewafanya wengi kuwa wajane ndani yake. 26  Makuhani wake wamevunja sheria yangu,+ nao wanaendelea kupatia unajisi mahali pangu patakatifu.+ Hawatofautishi kati ya kitu kitakatifu na cha kawaida,+ hawawajulishi watu kisicho safi na kilicho safi,+ na wanakataa kushika sabato zangu, nami nimechafuliwa kati yao. 27  Wakuu wake walio kati yake ni kama mbwamwitu wanaorarua mawindo; wanamwaga damu na kuua watu* ili wapate faida isiyo ya haki.+ 28  Lakini manabii wake wamepiga lipu matendo yao kwa kutumia chokaa. Wanaona maono ya uwongo na kufanya uaguzi* wa uwongo,+ nao wanasema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi,” wakati ambapo Yehova mwenyewe hajasema. 29  Watu wa nchi wamewapunja watu na kuwanyang’anya vitu vyao,+ wamewatesa wenye uhitaji na maskini, nao wamempunja mkaaji mgeni na kumnyima haki.’ 30  “‘Nilikuwa nikitafuta kati yao mtu ambaye angeurekebisha ukuta wa mawe au asimame mbele yangu katika shimo ukutani kwa ajili ya nchi, ili nisiiangamize,+ lakini sikumpata yeyote. 31  Basi nitawamwagia ghadhabu yangu na kuwaangamiza kabisa kwa moto wa ghadhabu yangu. Nitawaletea madhara ya njia yao juu ya kichwa chao wenyewe,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “je, utalihukumu, je, utalihukumu.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Tnn., “wanaufunua uchi wa baba yao.”
Au “kutoza riba ya juu sana.”
Tnn., “moyo.”
Au “nafsi.”
Au “ubashiri.”