Ezekieli 23:1-49

  • Dada wawili ambao si waaminifu (1-49)

    • Ohola na Ashuru (5-10)

    • Oholiba na Babiloni na Misri (11-35)

    • Kuadhibiwa kwa dada wawili (36-49)

23  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, kulikuwa na wanawake wawili waliokuwa mabinti za mama mmoja.+  Wakawa makahaba huko Misri;+ tangu ujana wao walifanya ukahaba. Huko matiti yao yalitomaswa, na vifua vyao vya ubikira vilipapaswa-papaswa.  Yule mkubwa aliitwa Ohola,* na dada yake Oholiba.* Wakawa wangu nao wakazaa wana na mabinti. Kuhusu majina yao, Ohola ni Samaria,+ na Oholiba ni Yerusalemu.  “Ohola akaanza kufanya ukahaba+ alipokuwa wangu. Aliwatamani kwa uchu wapenzi wake,+ majirani zake Waashuru.+  Walikuwa magavana waliovaa mavazi ya bluu na watawala wasaidizi—wote walikuwa vijana wanaovutia waliopanda farasi wao.  Akaendelea kufanya ukahaba na wana wote bora wa Ashuru, naye akajichafua+ kwa sanamu zinazochukiza* za wale aliowatamani kwa uchu.  Hakuacha ukahaba aliofanya huko Misri, kwa maana walilala naye alipokuwa kijana, nao walipapasa-papasa kifua chake cha ubikira na kummwagia uchu wao.*+  Basi nikamtia mikononi mwa wapenzi wake, wana wa Ashuru,+ ambao aliwatamani kwa uchu. 10  Waliufunua uchi+ wake na kuwakamata wanawe na mabinti zake,+ naye wakamuua kwa upanga. Akawa na sifa mbaya kati ya wanawake, nao wakatekeleza hukumu dhidi yake. 11  “Dada yake Oholiba alipoona jambo hilo, akawa na uchu mbaya zaidi, na ukahaba wake ulikuwa mbaya kuliko wa dada yake.+ 12  Aliwatamani kwa uchu majirani zake wana wa Ashuru,+ magavana na watawala wasaidizi waliovaa mavazi ya kifahari na waliopanda farasi—wote walikuwa vijana wanaovutia. 13  Alipojichafua, niliona kwamba wote wawili walikuwa wamefuata njia ileile.+ 14  Lakini alizidisha matendo yake ya ukahaba. Aliwaona wanaume waliochongwa ukutani, sanamu za Wakaldayo zilizochongwa na kupakwa rangi nyekundu, 15  wakiwa wamevaa mishipi kiunoni, na vilemba vikubwa kwenye vichwa vyao, nao walikuwa na sura kama za mashujaa, wote walifanana na Wababiloni, waliozaliwa katika nchi ya Wakaldayo. 16  Akaanza kuwatamani kwa uchu mara tu alipowaona, naye akawatuma wajumbe kwao huko Ukaldayo.+ 17  Basi wana wa Babiloni wakaendelea kuja kwenye kitanda chake cha mapenzi, nao wakamchafua kwa uchu wao.* Baada ya kuchafuliwa nao, akawaacha akiwa amechukizwa. 18  “Alipoendelea kufanya ukahaba kwa ushupavu na kufunua uchi wake,+ nilimwacha nikiwa nimechukizwa, kama nilivyomwacha dada yake nikiwa nimechukizwa.+ 19  Naye akaendelea kuzidisha matendo yake ya ukahaba,+ akizikumbuka siku za ujana wake alipofanya ukahaba nchini Misri.+ 20  Aliwatamani kwa uchu kama masuria wa wanaume ambao kiungo chao cha kiume ni kama cha punda na ambao viungo vyao vya uzazi ni kama vya farasi. 21  Ulitamani mwenendo wako mchafu uliokuwa nao ulipokuwa kijana kule Misri+ walipopapasa-papasa kifua chako, matiti ya ujana wako.+ 22  “Kwa hiyo, ewe Oholiba, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Ninawachochea wale waliokupenda+ ambao uliwaacha ukiwa umechukizwa, nami nitawaleta ili wakushambulie kutoka kila upande,+ 23  wana wa Babiloni+ na Wakaldayo+ wote, wanaume wa Pekodi+ na Shoa na Koa, pamoja na wana wote wa Ashuru. Wote ni vijana wanaovutia, magavana na watawala wasaidizi, mashujaa waliochaguliwa moja kwa moja,* wote wakiwa wamepanda farasi. 24  Watakushambulia kwa magari ya vita na magurudumu yenye kelele pamoja na umati mkubwa wa wanajeshi, pamoja na ngao kubwa na ngao ndogo* na kofia. Watajipanga kukuzunguka, nami nitawapa mamlaka ya kuhukumu, nao lazima wakuhukumu wapendavyo.+ 25  Nitakumwagia ghadhabu yangu, nao watakutendea kwa hasira kali. Watakata pua yako na masikio yako, na watu wako waliobaki watauawa kwa upanga. Watawachukua wana na mabinti zako, na watu wako wanaobaki watateketezwa kabisa kwa moto.+ 26  Watakuvua mavazi yako+ na kuchukua vito vyako* maridadi.+ 27  Nitaukomesha mwenendo wako mchafu na ukahaba wako+ ulioanza nchini Misri.+ Utaacha kuwatazama, na hutaikumbuka Misri tena.’ 28  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Niko karibu kukutia mikononi mwa wale unaowachukia, wale uliowaacha ukiwa umechukizwa.+ 29  Watakutendea kwa chuki na kuchukua kila kitu ulichofanyia kazi kwa jasho+ nao watakuacha ukiwa uchi, bila chochote. Uchi unaoaibisha wa uasherati wako na mwenendo wako mchafu na ukahaba wako utafunuliwa.+ 30  Utatendewa mambo hayo kwa sababu uliyafuata mbio mataifa kama kahaba,+ kwa sababu ulijichafua kwa sanamu zao zinazochukiza.+ 31  Umeifuata njia ileile aliyoifuata dada yako,+ nami nitakiweka kikombe chake mkononi mwako.’+ 32  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Utakunywa kikombe kipana na chenye kina cha dada yako,+ Nawe utakuwa kitu cha kuchekwa na kudhihakiwa, na kikombe hicho kina mambo hayo kwa wingi.+ 33  Utalemewa na* ulevi na huzuni, Kikombe cha hofu na ukiwa, Kikombe cha dada yako, Samaria. 34  Utalazimika kukinywa na kukimaliza kabisa+ na kuviguguna vigae vyake Kisha utayang’oa matiti yako. “Kwa maana mimi mwenyewe nimesema,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’ 35  “Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa kuwa umenisahau nawe umenipuuza kabisa,*+ utapata madhara ya mwenendo wako mchafu na matendo yako ya ukahaba.’” 36  Kisha Yehova akaniambia: “Mwana wa binadamu, je, utatangaza hukumu dhidi ya Ohola na Oholiba+ na kuwaonyesha waziwazi mazoea yao yanayochukiza? 37  Wamefanya uzinzi,*+ na mikono yao ina damu. Hawajafanya uzinzi tu na sanamu zao zinazochukiza, bali pia wamewateketeza* motoni wana wao walionizalia, kama chakula cha sanamu zao.+ 38  Isitoshe, hili ndilo wamenifanyia: Walipatia unajisi mahali pangu patakatifu siku hiyo, nao wakazitia unajisi sabato zangu. 39  Baada ya kuwachinja wana wao kama dhabihu kwa sanamu zao zinazochukiza,+ walikuja mahali pangu patakatifu ili kupatia unajisi+ siku hiyohiyo. Hivyo ndivyo walivyofanya ndani ya nyumba yangu mwenyewe. 40  Hata walimtuma mjumbe ili awaite wanaume waje kutoka mbali.+ Walipokuwa wakija, ulioga na kujipaka rangi machoni na kujipamba kwa mapambo.+ 41  Nawe ukaketi kwenye kochi la kifahari+ ambalo mbele yake kuna meza iliyoandaliwa,+ na juu yake uliweka uvumba wangu+ na mafuta yangu.+ 42  Sauti ya umati wa watu waliostarehe ilisikika huko, na miongoni mwao kulikuwa na walevi walioletwa kutoka nyikani. Waliwavisha wanawake bangili kwenye mikono na mataji maridadi kwenye vichwa vyao. 43  “Ndipo nikasema kumhusu yule aliyechakazwa na uzinzi: ‘Sasa ataendelea kufanya ukahaba wake.’ 44  Basi wakaendelea kuingia kwake, kama mtu anavyoenda kwa kahaba. Hivyo ndivyo walivyoenda kwa Ohola na kwa Oholiba, wanawake wenye mwenendo mchafu. 45  Lakini watu waadilifu watamhukumu kwa hukumu ambayo uzinzi+ na umwagaji wa damu unastahili;+ kwa maana wao ni wanawake wazinzi na mikono yao ina damu.+ 46  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Jeshi litaletwa liwashambulie na kuwafanya kuwa kitu cha kutisha na kitu cha kuporwa.+ 47  Jeshi hilo litawapiga mawe+ na kuwakatakata kwa panga zao. Watawaua wana wao na mabinti wao+ na kuziteketeza nyumba zao kwa moto.+ 48  Nitakomesha mwenendo wako mchafu nchini, na wanawake wote watajifunza somo nao hawataiga mwenendo wenu mchafu.+ 49  Watawaletea madhara ya mwenendo wenu mchafu na ya dhambi zenu kuhusiana na sanamu zenu zinazochukiza; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’”+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Hema Langu Limo Ndani Yake.”
Maana yake “Hema Lake.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Au “kufanya naye uasherati.”
Au “kwa uasherati wao.”
Tnn., “walioitwa.”
Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.
Au “mapambo yako.”
Au “Utajawa na.”
Tnn., “umenitupa nyuma ya mgongo wako.”
Tnn., “wamewapitisha.”
Yaani, uzinzi wa kiroho.