Ezekieli 26:1-21

  • Unabii dhidi ya Tiro (1-21)

    • “Uwanja wa kukaushia nyavu za kukokotwa” (5, 14)

    • Mawe na udongo vyatupwa ndani ya maji (12)

26  Katika mwaka wa 11, siku ya kwanza ya mwezi, neno la Yehova lilinijia likisema:  “Mwana wa binadamu, kwa sababu Tiro amesema kuhusu Yerusalemu,+ ‘Aha! Lango la mataifa limevunjwa!+ Kila kitu kitakuja kwangu, nami nitakuwa tajiri kwa sababu ameangamizwa’;  kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Niko dhidi yako, Ee Tiro, nami nitayainua mataifa mengi dhidi yako, kama vile bahari inavyoinua mawimbi yake.  Wataziharibu kuta za Tiro na kuibomoa minara yake,+ nami nitakwangua udongo na kumfanya awe mwamba ulio wazi, unaong’aa.  Atakuwa uwanja wa kukaushia nyavu za kukokotwa katikati ya bahari.’+ “‘Kwa maana mimi mwenyewe nimesema,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘naye ataporwa na mataifa.  Na vijiji vyake* vilivyo mashambani vitachinjwa kwa upanga, na watu watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Ninamleta Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni dhidi ya Tiro kutoka kaskazini;+ yeye ni mfalme wa wafalme,+ akiwa na farasi,+ magari ya vita,+ wapanda farasi, na jeshi lenye wanajeshi* wengi.  Ataviangamiza kwa upanga vijiji vyako vilivyo mashambani, naye atajenga ukuta wa kuzingira na kujenga dhidi yako boma la kuzingira na kuinua ngao kubwa dhidi yako.  Ataponda kuta zako kwa mtambo wake wa kubomolea,* na kubomoa minara yako kwa mashoka yake.* 10  Farasi wake watakuwa wengi sana hivi kwamba watakufunika kwa mavumbi, na sauti ya wapanda farasi, magurudumu, na magari ya vita itafanya kuta zako zitikisike anapoingia kwenye malango yako, kama wanaume wanaovamia jiji lenye kuta zilizobomolewa. 11  Kwato za farasi wake zitakanyaga-kanyaga barabara zako zote;+ atawaua watu wako kwa upanga, na nguzo zako kubwa zitaporomoka ardhini. 12  Wataiba mali zako, watapora bidhaa zako,+ watabomoa kuta zako, na kubomoa nyumba zako nzuri; kisha watayatupa mawe yako na mbao zako na udongo wako katika maji.’ 13  “‘Nitakomesha kelele za nyimbo zako, na sauti ya vinubi vyako haitasikika tena.+ 14  Nami nitakufanya uwe jiwe lililo wazi, linalong’aa, nawe utakuwa uwanja wa kukaushia nyavu za kukokotwa.+ Hutajengwa tena kamwe, kwa maana mimi mwenyewe, Yehova, nimesema,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 15  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anamwambia Tiro hivi: ‘Je, visiwa havitatetemeka vitakaposikia sauti ya kuanguka kwako, wanaokaribia kufa* watakapokuwa wakilia kwa maumivu makali, na uchinjaji utakapokuwa ukiendelea ndani yako?+ 16  Wakuu wote wa bahari hakika watashuka kutoka kwenye viti vyao vya ufalme na kuvua kanzu zao* na mavazi yao yaliyotariziwa, nao wataanza* kutetemeka. Wataketi chini na kuendelea kutetemeka na kukuangalia kwa mshangao.+ 17  Nao watakuimbia wimbo wa huzuni*+ na kukuambia: “Jinsi ulivyoangamia,+ wewe uliyekuwa na wakaaji kutoka baharini, jiji lililosifiwa; Wewe na wakaaji wako mlikuwa wenye nguvu baharini,+ Ukieneza hofu kwa wakaaji wote wa dunia! 18  Visiwa vitatetemeka siku utakapoanguka, Visiwa vya bahari vitakuwa na wasiwasi utakapoondoka.”’+ 19  “Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Nitakapokufanya ukiwa kama majiji yasiyokaliwa, nitakapokulemea kwa mawimbi makubwa nawe ufunikwe kwa maji mengi,+ 20  nitakushusha wewe pamoja na wale wanaoshuka shimoni,* kwa watu wa zamani za kale; nitakufanya ukae mahali pa chini zaidi, kama mahali pa zamani palipoachwa ukiwa, pamoja na wale wanaoshuka shimoni,+ ili usikaliwe. Kisha nitaitukuza* nchi ya walio hai. 21  “‘Nitakuletea hofu ya ghafla, nawe hutakuwapo tena.+ Watakutafuta, lakini hutapatikana tena kamwe,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “mabinti zake.”
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “watu.”
Au “mtambo wake wa kushambulia.”
Au “panga zake.”
Tnn., “waliouawa.”
Au “majoho yasiyo na mikono.”
Tnn., “watavikwa.”
Au “wimbo wa maombolezo.”
Au “kaburini.”
Au “nitaipamba.”