Ezekieli 27:1-36

  • Wimbo wa huzuni kuhusu meli inayozama ya Tiro (1-36)

27  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Nawe, mwana wa binadamu, mwimbie Tiro wimbo wa huzuni,*+  nawe umwambie Tiro, ‘Wewe unayekaa katika malango ya bahari, Mfanyabiashara wa mataifa ya visiwa vingi, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ee Tiro, wewe mwenyewe umesema, ‘Nina urembo mkamilifu.’+   Maeneo yako yamo katikati ya bahari, Na wajenzi wako wameukamilisha urembo wako.   Walitengeneza mbao zako zote kutokana na miberoshi ya Seniri,+ Nao waliuchukua mwerezi kutoka Lebanoni ili kukutengenezea mlingoti.   Walitengeneza makasia yako kutokana na mialoni ya Bashani, Na omo yako ilitengenezwa kwa mvinje na kupambwa ndani kwa pembe za tembo kutoka visiwa vya Kitimu.+   Kitani chenye rangi mbalimbali kutoka Misri ndicho kilichokuwa tanga lako, Na sitaha yako ilifunikwa kwa nyuzi za bluu na sufu ya zambarau kutoka visiwa vya Elisha.+   Wakaaji wa Sidoni na Arvadi+ walikuwa wapiga makasia wako. Watu wako mwenyewe wenye ustadi, Ee Tiro, walikuwa mabaharia wako.+   Wanaume wa Gebali+ wenye uzoefu* na ustadi waliziba nyufa zako kwa kalafati.+ Meli zote za baharini na wanamaji wake walikuja kwako kubadilishana bidhaa. 10  Wanaume wa Uajemi, Ludi, na Putu+ walikuwa katika jeshi lako, wanaume wako wa vita. Walitundika ngao na kofia zao ndani yako, nao walikuletea fahari. 11  Wanaume wa Arvadi katika jeshi lako walisimama juu ya kuta zako pande zote, Na wanaume jasiri walilinda minara yako. Walitundika ngao zao za mviringo kuzunguka kuta zako Nao wakaukamilisha urembo wako. 12  “‘“Watu wa Tarshishi+ walifanya biashara nawe kwa sababu ya utajiri wako mwingi.+ Walibadilisha fedha, chuma, bati, na risasi kwa ajili ya bidhaa zako.+ 13  Watu wa Yavani, Tubali,+ na Mesheki+ walifanya nawe biashara, wakibadilisha watumwa+ na vitu vya shaba kwa ajili ya bidhaa zako. 14  Watu wa nyumba ya Togarma+ walibadilisha farasi na farasi wa vita na nyumbu kwa ajili ya bidhaa zako. 15  Watu wa Dedani+ walifanya nawe biashara; uliwaajiri wafanyabiashara kwenye visiwa vingi; walitoa pembe za tembo+ na mbao za mpingo kama ushuru wako. 16  Watu wa Edomu walifanya biashara nawe kwa sababu ya wingi wa bidhaa zako. Walitoa feruzi, sufu ya zambarau, vitambaa vyenye rangi mbalimbali vilivyotariziwa, vitambaa bora, marijani, na zabarijadi ili kubadilishana na bidhaa zako. 17  “‘“Watu wa Yuda na wa nchi ya Israeli walifanya nawe biashara, wakitoa ngano ya Minithi,+ vyakula bora, asali,+ mafuta, na zeri+ ili kubadilishana na bidhaa zako.+ 18  “‘“Watu wa Damasko+ walifanya nawe biashara kwa sababu ya wingi wa bidhaa zako na utajiri wako wote, wakibadilishana divai ya Helboni na sufu ya Zahari.* 19  Watu wa Vedani na Yavani kutoka Uzali walitoa chuma kilichofuliwa, kida,* na kane* ili kubadilishana na bidhaa zako. 20  Watu wa Dedani+ walifanya nawe biashara kwa kukupa matandiko ya farasi.* 21  Uliwaajiri Waarabu na wakuu wote wa Kedari,+ waliokuwa wafanyabiashara wa wanakondoo na kondoo dume na mbuzi.+ 22  Wafanyabiashara wa Sheba na Raama+ walibadilishana nawe bidhaa; walitoa kila aina ya manukato bora, mawe yenye thamani, na dhahabu, ili kubadilishana na bidhaa zako.+ 23  Watu wa Harani,+ Kane, Edeni,+ wafanyabiashara wa Sheba,+ Asihuru,+ na Kilmadi walibadilishana nawe bidhaa. 24  Katika soko lako walibadilishana nawe mavazi maridadi, majoho yaliyotengenezwa kwa kitambaa cha bluu na vitambaa vyenye rangi mbalimbali vilivyotariziwa, na mazulia ya rangi mbalimbali, yote yakiwa yamefungwa kabisa kwa kamba. 25  Meli za Tarshishi+ zilisafirisha bidhaa zako katika misafara, Hivi kwamba ukajaa na kulemewa na mzigo* katikati ya bahari kuu. 26  Wapiga makasia wako wamekuleta katika bahari kuu; Upepo wa mashariki umekuvunjavunja katikati ya bahari kuu. 27  Utajiri wako, bidhaa zako, mali zako, wanamaji wako, na mabaharia wako, Wale wanaoziba nyufa zako kwa kalafati, wale wanaofanya biashara ya kubadilishana bidhaa zako,+ na wanaume wote wa vita+ —Umati wote ulio* ndani yako— Wote watazama katikati ya bahari kuu siku utakayoanguka.+ 28  Mabaharia wako watakapolia kwa sauti, maeneo ya pwani yatatetemeka. 29  Wapiga makasia wote, wanamaji, na mabaharia Watashuka kutoka kwenye meli zao na kusimama kwenye nchi kavu. 30  Watapaza sauti zao na kukulilia kwa uchungu+ Huku wakijirushia mavumbi vichwani na kugaagaa kwenye majivu. 31  Watajitia upara na kuvaa nguo za magunia; Watakulilia kwa uchungu* na kukuombolezea sana. 32  Katika maombolezo yao watakuimbia wimbo wa huzuni na kukuombolezea wakisema: ‘Ni nani aliye kama Tiro, ambaye sasa amenyamazishwa katikati ya bahari?+ 33  Bidhaa zako zilipofika kutoka kwenye bahari kuu, uliyashibisha mataifa mengi.+ Utajiri wako mwingi na bidhaa zako ziliwatajirisha wafalme wa dunia.+ 34  Sasa umevunjwavunjwa katika bahari kuu, katika vilindi vya bahari,+ Na bidhaa zako zote na watu wako wamezama pamoja nawe.+ 35  Wakaaji wote wa visiwani watakutazama kwa mshangao,+ Nao wafalme wao watatetemeka kwa hofu+—nyuso zao zitakuwa na wasiwasi. 36  Wafanyabiashara miongoni mwa mataifa watapiga mluzi kwa sababu ya yale yatakayokupata. Mwisho wako utafika ghafla nao utakuwa mbaya sana, Nawe hutakuwapo tena kamwe.’”’”+

Maelezo ya Chini

Au “wimbo wa maombolezo.”
Tnn., “wanaume wazee.”
Au “sufu ya rangi nyekundu na kijivu.”
Mti wa jamii ya mdalasini.
Utete wenye harufu nzuri.
Au “matandiko yaliyotengenezwa kwa vitambaa vilivyofumwa.”
Au labda, “na utukufu.”
Tnn., “Kutaniko lolote lililo.”
Au “kwa uchungu wa nafsi.”