Ezekieli 28:1-26

  • Unabii dhidi ya mfalme wa Tiro (1-10)

    • “Mimi ni mungu” (2, 9)

  • Wimbo wa huzuni kuhusu mfalme wa Tiro (11-19)

    • “Ulikuwa katika Edeni” (13)

    • “Kerubi anayefunika aliyetiwa mafuta” (14)

    • ‘Uovu ulipatikana ndani yako’ (15)

  • Unabii dhidi ya Sidoni (20-24)

  • Israeli watarudishwa (25, 26)

28  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, mwambie kiongozi wa Tiro, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa sababu moyo wako umekuwa na majivuno,+ unaendelea kusema, ‘Mimi ni mungu. Ninaketi kwenye kiti cha ufalme cha mungu katikati ya bahari.’+ Lakini wewe ni mwanadamu tu, wewe si mungu, Ingawa moyoni mwako unahisi kwamba wewe ni mungu.   Tazama! Una hekima kuliko Danieli.+ Hujafichwa siri yoyote.   Umejitajirisha kwa hekima yako na utambuzi wako, Nawe unaendelea kukusanya dhahabu na fedha katika hazina zako.+   Ustadi wako katika biashara ulikuletea utajiri mwingi,+ Nao moyo wako ukawa na majivuno kwa sababu ya utajiri wako.”’  “‘Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa sababu katika moyo wako unahisi wewe ni mungu,   Ninawaleta wageni wakushambulie, walio wakatili zaidi kati ya mataifa,+ Nao watachomoa panga zao na kuuharibu uzuri wa hekima yako Na kuitia unajisi fahari yako yenye utukufu.+   Watakushusha shimoni,* Nawe utakufa kifo cha kikatili katikati ya bahari kuu.+   Je, bado utamwambia yule anayekuua, ‘Mimi ni mungu?’ Utakuwa mwanadamu tu, wala si mungu, mikononi mwa wale wanaokutia unajisi.”’ 10  “‘Kwa mkono wa wageni, utakufa kifo cha watu ambao hawajatahiriwa, Kwa maana mimi mwenyewe nimesema,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 11  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 12  “Mwana wa binadamu, mwimbie mfalme wa Tiro wimbo wa huzuni,* nawe umwambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ulikuwa mfano wa ukamilifu,* Ulijaa hekima+ nawe ulikuwa na urembo mkamilifu.+ 13  Ulikuwa katika Edeni, bustani ya Mungu. Ulipambwa kwa kila jiwe lenye thamani —Zabarijadi, topazi, na yaspi; krisolito, shohamu, na yashefi; yakuti, feruzi,+ na zumaridi; Na vifuko na vishikizi vyake vilikuwa vya dhahabu. Vilitayarishwa siku uliyoumbwa. 14  Nilikuweka kuwa kerubi anayefunika aliyetiwa mafuta. Ulikuwa kwenye mlima mtakatifu wa Mungu,+ nawe ulitembea-tembea kati ya mawe yenye moto. 15  Hukuwa na kosa katika njia zako tangu siku uliyoumbwa Mpaka uovu* ulipopatikana ndani yako.+ 16  Kwa sababu ya biashara zako nyingi,+ Ulijaa ukatili, nawe ukaanza kutenda dhambi.+ Basi nitakufukuza kutoka kwenye mlima wa Mungu kama kitu kilicho najisi na kukuangamiza,+ Mbali kutoka kwenye mawe ya moto, ewe kerubi unayefunika. 17  Moyo wako ulikuwa na majivuno kwa sababu ya urembo wako.+ Uliipotosha hekima yako kwa sababu ya fahari yako yenye utukufu.+ Nitakutupa chini duniani.+ Nitakufanya uwe kitu cha kutazamwa na wafalme. 18  Kwa sababu ya hatia yako kubwa na ukosefu wako wa unyoofu katika biashara, umepatia unajisi mahali pako patakatifu. Nitatokeza moto katikati yako, nao utakuteketeza kabisa.+ Nitakufanya uwe majivu juu ya dunia mbele ya wote wanaokutazama. 19  Wale wote waliokujua kati ya mataifa watakutazama kwa mshangao.+ Mwisho wako utafika ghafla nao utakuwa mbaya sana, Hutakuwapo tena kamwe.”’”+ 20  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 21  “Mwana wa binadamu, uelekeze uso wako Sidoni,+ nawe utabiri dhidi yake. 22  Nawe utasema, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Niko dhidi yako, Ee Sidoni, nami nitatukuzwa katikati yako; Na watu watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakapotekeleza hukumu dhidi yake na kutakaswa ndani yake. 23  Nitapeleka ugonjwa hatari humo na damu itatiririka kwenye barabara zake. Waliouawa wataanguka katikati yake upanga utakapokuja kumshambulia kutoka kila upande; Nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.+ 24  “‘“Na watu wa nyumba ya Israeli hawatazungukwa tena na michongoma inayodhuru na miiba mikali,+ wale wanaowadhihaki; na watu watalazimika kujua kwamba mimi ni Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”’ 25  “‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitakapowakusanya tena watu wa nyumba ya Israeli kutoka miongoni mwa mataifa walikotawanywa,+ nitatakaswa kati yao machoni pa mataifa.+ Nao watakaa katika nchi yao+ niliyompa mtumishi wangu Yakobo.+ 26  Wataishi huko kwa usalama+ na watajenga nyumba na kupanda mashamba ya mizabibu+ na watakaa kwa usalama nitakapotekeleza hukumu dhidi ya wote wanaowazunguka ambao wanawadhihaki;+ nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao.”’”

Maelezo ya Chini

Au “kaburini.”
Tnn., “Ulikuwa ukifunga kielelezo kwa muhuri.”
Au “wimbo wa maombolezo.”
Au “ukosefu wa uadilifu.”