Ezekieli 3:1-27

  • Ezekieli aambiwa ale kitabu cha kukunjwa alichopewa na Mungu (1-15)

  • Ezekieli atakuwa mlinzi (16-27)

    • Kupuuza kunasababisha hatia ya damu (18-21)

3  Kisha akaniambia: “Mwana wa binadamu, kula kilicho mbele yako.* Kula kitabu hiki cha kukunjwa, na uende ukazungumze na watu wa nyumba ya Israeli.”+  Kwa hiyo nikafungua kinywa changu, naye akanipa kitabu hicho nile.  Naye akaendelea kuniambia: “Mwana wa binadamu, kula kitabu hiki ninachokupa, ukijaze tumboni mwako.” Basi nikaanza kukila, nacho kilikuwa kitamu kama asali kinywani mwangu.+  Akaniambia: “Mwana wa binadamu, nenda miongoni mwa watu wa nyumba ya Israeli uwaambie maneno yangu.  Kwa maana hutumwi kwenda kwa watu wanaozungumza lugha isiyoeleweka au lugha isiyojulikana, bali kwa watu wa nyumba ya Israeli.  Hutumwi kwa watu wengi wanaozungumza lugha isiyoeleweka au lugha isiyojulikana, ambao maneno yao huwezi kuelewa. Ikiwa ningekutuma kwao, wangekusikiliza.+  Lakini watu wa nyumba ya Israeli watakataa kukusikiliza, kwa maana hawataki kunisikiliza mimi.+ Watu wote wa nyumba ya Israeli wana vichwa vigumu na mioyo migumu.+  Tazama! Nimeufanya uso wako uwe mgumu kama nyuso zao na paji la uso wako liwe gumu kama mapaji ya nyuso zao.+  Nimelifanya paji la uso wako kuwa kama almasi, gumu kuliko jiwe gumu.+ Usiwaogope, wala usitishwe na nyuso zao,+ kwa maana wao ni nyumba ya uasi.” 10  Naye akaendelea kuniambia: “Mwana wa binadamu, yatie moyoni mwako na kuyasikiliza maneno yangu yote nitakayokuambia. 11  Nenda miongoni mwa watu wako waliohamishwa*+ uzungumze nao. Waambie, ‘Hivi ndivyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anavyosema,’ iwe watasikiliza au watakataa kusikiliza.”+ 12  Ndipo roho ikanibeba+ nami nikasikia nyuma yangu sauti ya mngurumo mkubwa iliyosema: “Utukufu wa Yehova na usifiwe katika mahali pake.” 13  Nilisikia sauti ya mabawa ya wale viumbe hai yalipokuwa yakigusana,+ na sauti ya magurudumu kando yao,+ na sauti ya mngurumo mkubwa. 14  Nayo roho ikanibeba na kunichukua, nami nikaenda kwa uchungu na kwa ghadhabu ya roho yangu, na mkono wa Yehova ukatulia juu yangu kwa nguvu. 15  Basi nikaenda Tel-abibu kwa watu waliohamishwa, waliokuwa wakikaa kando ya mto Kebari,+ nami nikakaa huko walipokuwa wakikaa; nikakaa miongoni mwao kwa siku saba nikiwa nimepigwa na bumbuazi.+ 16  Mwishoni mwa siku saba neno la Yehova likanijia: 17  “Mwana wa binadamu, nimekuweka kuwa mlinzi wa watu wa nyumba ya Israeli;+ nawe unaposikia neno kutoka katika kinywa changu, lazima uwape onyo langu.+ 18  Ninapomwambia mtu mwovu, ‘Hakika utakufa,’ lakini wewe usimwonye, nawe ukatae kumwambia mtu huyo mwovu aiache njia yake ya uovu ili aendelee kuwa hai,+ yeye atakufa kwa sababu ya kosa lake kwa sababu yeye ni mwovu,+ lakini damu yake nitaidai kutoka kwako.*+ 19  Lakini ukimwonya mtu mwovu naye asiuache uovu wake na njia yake ya uovu, yeye atakufa kwa sababu ya kosa lake, lakini wewe kwa hakika utauokoa uhai wako.*+ 20  Lakini mtu mwadilifu anapoacha uadilifu wake na kutenda kosa,* nitaweka kikwazo mbele yake, naye atakufa.+ Ikiwa hukumwonya, atakufa kwa sababu ya dhambi yake na matendo yake ya uadilifu hayatakumbukwa, lakini damu yake nitaidai kutoka kwako.*+ 21  Lakini ikiwa umemwonya mtu mwadilifu asitende dhambi, naye asitende dhambi, kwa hakika ataendelea kuwa hai kwa sababu alionywa,+ na wewe utauokoa uhai wako.”* 22  Nikiwa huko mkono wa Yehova ukanijia, naye akaniambia: “Ondoka, nenda kwenye bonde tambarare, nami nitazungumza nawe huko.” 23  Basi nikaondoka na kwenda kwenye bonde tambarare, na tazama! utukufu wa Yehova ulikuwa huko,+ kama utukufu niliokuwa nimeuona kando ya mto Kebari,+ nami nikaanguka chini kifudifudi. 24  Kisha roho ikaingia ndani yangu na kunifanya nisimame kwa miguu yangu,+ naye akaniambia: “Nenda, jifungie ndani ya nyumba yako. 25  Lakini wewe mwana wa binadamu, wataweka kamba juu yako na kukufunga nazo ili usiweze kuondoka miongoni mwao. 26  Nami nitaufanya ulimi wako ushikamane na kaakaa la kinywa chako, nawe utakuwa bubu, usiweze kuwakaripia, kwa sababu wao ni nyumba ya uasi. 27  Lakini ninapozungumza nawe nitafungua kinywa chako, nawe lazima uwaambie,+ ‘Hivi ndivyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anavyosema.’ Anayesikiliza na asikilize,+ na anayekataa kusikiliza na akatae, kwa sababu wao ni nyumba ya uasi.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “kula utakachopata.”
Tnn., “wana wa watu wako.”
Au “nitakufanya uwajibike kwa sababu ya damu yake.”
Au “utaiokoa nafsi yako.”
Au “kutenda jambo lisilo la haki.”
Au “nitakufanya uwajibike kwa sababu ya damu yake.”
Au “utaiokoa nafsi yako.”