Ezekieli 31:1-18

  • Kuanguka kwa Misri, mwerezi mrefu (1-18)

31  Katika mwaka wa 11, mwezi wa tatu, siku ya kwanza ya mwezi huo, neno la Yehova lilinijia likisema:  “Mwana wa binadamu, mwambie mfalme Farao wa Misri na umati wake,+ ‘Unafanana na nani katika ukuu wako?   Kulikuwa na Mwashuru, mwerezi kule Lebanoni, Uliokuwa na matawi maridadi kama kichaka chenye kivuli, na uliokuwa mrefu, Kilele chake kilikuwa mawinguni.   Maji yaliufanya uwe mkubwa, chemchemi zenye maji mengi ziliufanya uwe mrefu. Vijito vilizunguka mahali ulipopandwa; Mifereji yake iliinywesha maji miti yote ya shambani.   Ndiyo sababu ulikuwa mrefu kuliko miti mingine yote ya shambani. Na vitawi vyake viliongezeka, na matawi yake yakawa marefu Kwa sababu ya maji mengi ya vijito vyake.   Ndege wote wa angani walitengeneza viota kwenye vitawi vyake, Wanyama wote wa mwituni walizaa chini ya matawi yake, Na mataifa yote yenye watu wengi yaliishi chini ya kivuli chake.   Ukapendeza katika uzuri na urefu wa matawi yake, Kwa maana mizizi yake ilipenya chini kwenye maji mengi.   Hakuna mwerezi mwingine katika bustani ya Mungu+ uliofanana nao. Hakuna mberoshi uliokuwa na vitawi kama vyake, Na hakuna mwaramoni uliokuwa na matawi yaliyofanana na yake. Hakuna mti mwingine katika bustani ya Mungu uliokaribia uzuri wake.   Niliufanya upendeze, kwa majani mengi, Na miti mingine yote ya Edeni, bustani ya Mungu wa kweli, iliuonea wivu.’ 10  “Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu ulikuwa* mrefu sana, ukainua kilele chake mawinguni, nao moyo wake ukawa na kiburi kwa sababu ya kimo chake, 11  nitautia mikononi mwa mtawala mwenye nguvu wa mataifa.+ Hakika atauadhibu, nami nitaukataa kwa sababu ya uovu wake. 12  Na wageni, wakatili zaidi kati ya mataifa, wataukata, nao watauacha milimani, nayo majani yake yataanguka katika mabonde yote, na matawi yake yatavunjika na kusambaa katika vijito vyote vya nchi.+ Mataifa yote ya dunia yataondoka kwenye kivuli chake na kuuacha. 13  Ndege wote wa angani wataishi kwenye shina lake lililoanguka, na wanyama wote wa mwituni kwenye matawi yake.+ 14  Itakuwa hivyo ili mti wowote ulio karibu na maji usiwe mrefu sana au usiinue kilele chake mawinguni na kusiwe na mti ulionyweshwa maji mengi utakaofikia kimo chao. Kwa maana miti yote itatiwa mikononi mwa kifo, kwenye nchi iliyo chini, pamoja na wana wa binadamu, wanaoshuka shimoni.’* 15  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Siku utakaposhuka kuingia Kaburini* nitasababisha maombolezo. Kwa hiyo, nitayafunika maji yenye kina na kuvizuia vijito vyake ili maji yake mengi yazuiwe. Nitatia giza Lebanoni kwa sababu yake, nayo miti yote ya shambani itanyauka. 16  Nitayafanya mataifa yatetemeke kwa sauti ya kuanguka kwake nitakapoushusha Kaburini* pamoja na wote wanaoshuka shimoni,* na miti yote ya Edeni,+ miti iliyo bora na iliyo mizuri kabisa ya Lebanoni, miti yote iliyonyweshwa maji mengi, itafarijiwa katika nchi iliyo chini. 17  Wameshuka Kaburini* pamoja naye, kwa wale waliouawa kwa upanga,+ pamoja na wale waliomsaidia* ambao waliishi katika kivuli chake kati ya mataifa.’+ 18  “‘Ni mti gani katika Edeni uliofanana nawe kwa utukufu na ukuu?+ Lakini kwa hakika utashushwa pamoja na miti ya Edeni katika nchi iliyo chini. Utalala kati ya wale ambao hawajatahiriwa, pamoja na wale waliouawa kwa upanga. Itakuwa hivyo kwa Farao na umati wake wote,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “wewe ulikuwa.”
Au “kaburini.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Au “kaburini.”
Au “Sheoli.” Angalia Kamusi.
Tnn., “mkono wake.”