Ezekieli 34:1-31

  • Unabii dhidi ya wachungaji wa Israeli (1-10)

  • Jinsi Yehova anavyowatunza kondoo wake (11-31)

    • “Mtumishi wangu Daudi” atawachunga (23)

    • “Agano la amani” (25)

34  Neno la Yehova likanijia tena likisema:  “Mwana wa binadamu, tabiri dhidi ya wachungaji wa Israeli. Tabiri, na uwaambie wachungaji hao, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Ole wao wachungaji wa Israeli,+ ambao wamekuwa wakijilisha wenyewe! Je, wachungaji hawapaswi kulilisha kundi?+  Mnakula mafuta, mnajivika wenyewe sufu, nanyi mnamchinja mnyama aliyenona zaidi,+ lakini hamlilishi kundi.+  Hamjawatia nguvu walio dhaifu au kuwaponya wagonjwa au kuwafunga waliojeruhiwa au kuwarudisha waliotangatanga au kuwatafuta waliopotea;+ badala yake, mmewatawala kwa ukali na kwa uonevu.+  Kwa hiyo walitawanyika kwa sababu hakukuwa na mchungaji;+ walitawanyika na kuwa chakula cha kila mnyama wa mwituni.  Kondoo wangu waliendelea kutangatanga kwenye milima yote na kwenye kila kilima kirefu; kondoo wangu walitawanyika kotekote duniani, na hakuna aliyewatafuta au kujitahidi kuwapata.  “‘“Kwa hiyo, ninyi wachungaji, lisikieni neno la Yehova:  ‘“Kwa hakika kama ninavyoishi,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, “kwa sababu kondoo wangu wamekuwa windo, chakula cha kila mnyama wa mwituni, kwa sababu hapakuwa na mchungaji, nao wachungaji wangu hawakuwatafuta kondoo wangu; badala yake waliendelea kujilisha wenyewe, nao hawakuwalisha kondoo wangu,”’  basi, ninyi wachungaji, lisikieni neno la Yehova.⁠ 10  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Niko dhidi ya wachungaji, nami nitafanya wawajibike kwa sababu ya kondoo wangu,* nami nitawafukuza ili wasiwalishe* kondoo wangu,+ nao wachungaji hawatajilisha tena. Nitawaokoa kondoo wangu kutoka kinywani mwao, nao hawatakuwa chakula chao tena.’” 11  “‘Kwa maana Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Mimi nipo hapa, na mimi mwenyewe nitawatafuta kondoo wangu na kuwatunza.+ 12  Nitawatunza kondoo wangu kama mchungaji ambaye amewapata kondoo wake waliotawanyika na kuwalisha.+ Nitawaokoa kutoka katika maeneo yote walikotawanyika siku ya mawingu na giza zito.+ 13  Nitawatoa katika mataifa na kuwakusanya pamoja kutoka katika nchi hizo na kuwaleta katika nchi yao na kuwalisha kwenye milima ya Israeli,+ kando ya vijito na kando ya makao yote nchini. 14  Nitawalisha kwenye malisho mazuri, na nchi ambamo watalisha itakuwa kwenye milima mirefu ya Israeli.+ Huko watalala katika nchi yenye malisho mazuri,+ nao watakula kwenye malisho bora juu ya milima ya Israeli.” 15  “‘“Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo wangu,+ na mimi mwenyewe nitawalaza,”+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 16  “Aliyepotea nitamtafuta,+ anayetangatanga nitamrudisha, aliyejeruhiwa nitamfunga, na aliye dhaifu nitamtia nguvu; lakini aliyenona na aliye na nguvu nitamwangamiza. Huyo nitamlisha hukumu.” 17  “‘Kuwahusu ninyi kondoo wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Niko karibu kuhukumu kati ya kondoo mmoja na kondoo mwingine, kati ya kondoo dume na mbuzi dume.+ 18  Je, hamtosheki kujilisha kwenye malisho yaliyo bora zaidi? Je, ni lazima myakanyage-kanyage kwa miguu yenu malisho yenu mengine? Na baada ya kunywa maji yaliyo safi zaidi, je, ni lazima myachafue kwa kuyakanyaga-kanyaga kwa miguu yenu? 19  Je, kondoo wangu wanapaswa kujilisha kwa malisho mliyoyakanyaga-kanyaga kwa miguu yenu na kunywa maji yaliyochafuliwa kwa kukanyagwa-kanyagwa kwa miguu yenu?” 20  “‘Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anawaambia hivi: “Mimi nipo hapa, na mimi mwenyewe nitahukumu kati ya kondoo aliyenona na kondoo aliyekonda, 21  kwa maana kwa ubavu wenu na kwa bega lenu mliendelea kuwasukuma, na kwa pembe zenu mliendelea kuwasukuma wote waliokuwa wagonjwa mpaka mkawatawanya maeneo ya mbali. 22  Nami nitawaokoa kondoo wangu, nao hawataendelea kuwa windo;+ nami nitahukumu kati ya kondoo mmoja na kondoo mwingine. 23  Nami nitamweka mchungaji mmoja juu yao,+ mtumishi wangu Daudi,+ naye atawalisha. Yeye mwenyewe atawalisha na kuwa mchungaji wao.+ 24  Na mimi, Yehova, nitakuwa Mungu wao,+ na mtumishi wangu Daudi atakuwa kiongozi wao. Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema.+ 25  “‘“Nitafanya agano la amani pamoja nao,+ na kuwaondoa kabisa nchini wanyama hatari wa mwituni,+ ili wakae kwa usalama nyikani na kulala misituni.+ 26  Nitawafanya wao na eneo linalozunguka kilima changu kuwa baraka,+ nami nitaifanya mvua inyeshe kwa wakati unaofaa. Baraka zitamwagika kama mvua.+ 27  Miti ya shambani itazaa matunda yake, na udongo utatoa mazao yake,+ nao wataishi kwa usalama nchini. Nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakapozivunja nira zao+ na kuwaokoa kutoka mikononi mwa wale waliowafanya kuwa watumwa. 28  Hawatakuwa windo la mataifa tena, na wanyama wa mwituni wa dunia hawatawanyafua, nao wataishi kwa usalama, na hakuna mtu atakayewaogopesha.+ 29  “‘“Nitawatayarishia shamba maarufu,* nao hawatakufa tena kwa njaa kali nchini,+ na hawatafedheheshwa tena na mataifa.+ 30  ‘Nao watalazimika kujua kwamba mimi, Yehova Mungu wao, niko pamoja nao na kwamba wao, watu wa nyumba ya Israeli, ni watu wangu,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”’ 31  “‘Nanyi kondoo wangu,+ kondoo ninaowatunza, ninyi ni wanadamu tu, nami ni Mungu wenu,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Au “nitadai kondoo wangu kutoka mikononi mwao.”
Au “wasiwachunge.”
Tnn., “ili wapate jina.”