Ezekieli 36:1-38

  • Unabii kuhusu milima ya Israeli (1-15)

  • Kurudishwa kwa Waisraeli (16-38)

    • “Nitalitakasa jina langu kuu” (23)

    • “Kama bustani ya Edeni” (35)

36  “Nawe, mwana wa binadamu, tabiri kuhusu milima ya Israeli, nawe useme, ‘Enyi milima ya Israeli, lisikieni neno la Yehova.  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Adui amesema hivi dhidi yenu, ‘Aha! Hata mahali pa juu pa zamani pamekuwa mali yetu!’”’+  “Basi tabiri, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Kwa sababu wamekufanya uwe ukiwa na kukushambulia kutoka kila upande, ili uwe mali ya wale waliookoka* kutoka kati ya mataifa na watu wanaendelea kuzungumza kukuhusu na kukuchongea,+  kwa hiyo, enyi milima ya Israeli, sikieni neno la Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Hivi ndivyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anavyoiambia milima na vilima, vijito na mabonde, magofu yaliyofanywa ukiwa,+ na majiji yaliyoachwa ambayo yameporwa na kudhihakiwa na wale waliookoka kutoka katika mataifa yanayowazunguka;+  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anawaambia hivi: ‘Katika moto wa bidii yangu+ nitawakemea wale waliookoka kutoka katika mataifa na nchi yote ya Edomu, wale ambao kwa shangwe nyingi na kwa dharau kubwa*+ wamechukua nchi yangu na kuifanya kuwa mali yao, ili wachukue malisho yake na kuipora.’”’+  “Basi tabiri kuhusu nchi ya Israeli, nawe uiambie milima na vilima, vijito na mabonde, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Tazama! Nitazungumza kwa bidii yangu na kwa ghadhabu yangu, kwa sababu mmefedheheshwa na mataifa.”’+  “Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Mimi mwenyewe ninainua mkono wangu na kuapa kwamba mataifa yanayozunguka yatabeba aibu yao wenyewe.+  Lakini ninyi, enyi milima ya Israeli, mtachipusha matawi na kuzaa matunda yenu kwa ajili ya watu wangu Waisraeli,+ kwa maana watarudi hivi karibuni.  Kwa maana niko pamoja nanyi, nami nitawageukia, nanyi mtalimwa na kupandwa mbegu. 10  Nitazidisha idadi ya watu wako—nyumba yote ya Israeli, yote—nayo majiji yatakaliwa+ na magofu yatajengwa upya.+ 11  Naam, nitazidisha idadi ya watu wako na mifugo yako;+ wataongezeka na kuzaana. Nami nitafanya ukaliwe kama ilivyokuwa zamani,+ nami nitakufanya usitawi kuliko mwanzoni;+ nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.+ 12  Nitawafanya watu—watu wangu Waisraeli—watembee juu yako, nao watakumiliki.+ Utakuwa urithi wao, nawe hutawafanya wakose watoto tena kamwe.’”+ 13  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Kwa kuwa wanawaambia ninyi, “Wewe ni nchi inayowameza watu na kuwaua watoto wa mataifa yako,”’ 14  ‘kwa hiyo, hutawameza tena watu wala kuyafanya mataifa yako yakose watoto,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 15  ‘Sitaruhusu tena utukanwe na mataifa au udhihakiwe na watu,+ nawe hutafanya tena mataifa yako yakwazike,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 16  Na neno la Yehova likanijia tena likisema: 17  “Mwana wa binadamu, watu wa nyumba ya Israeli walipokuwa wakiishi katika nchi yao, waliichafua kwa njia zao na matendo yao.+ Njia zao zilikuwa kama uchafu wa hedhi kwangu.+ 18  Basi nikawamwagia ghadhabu yangu kwa sababu ya damu waliyoimwaga juu ya nchi+ na kwa sababu waliichafua nchi kwa sanamu zao zinazochukiza.*+ 19  Basi nikawatawanya miongoni mwa mataifa na kuwatawanya katika nchi mbalimbali.+ Niliwahukumu kulingana na njia yao na kulingana na matendo yao. 20  Lakini walipoingia katika mataifa hayo, watu walilichafua jina langu takatifu+ kwa kusema hivi kuwahusu: ‘Hawa ndio watu wa Yehova, lakini walilazimika kutoka katika nchi yake.’ 21  Basi nitalihangaikia jina langu takatifu, ambalo watu wa nyumba ya Israeli walilichafua miongoni mwa mataifa ambako walienda.”+ 22  “Kwa hiyo, waambie watu wa nyumba ya Israeli, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Sifanyi jambo hili kwa ajili yenu, enyi watu wa nyumba ya Israeli, bali kwa ajili ya jina langu takatifu, ambalo ninyi mmelichafua miongoni mwa mataifa ambako mlienda.”’+ 23  ‘Kwa hakika nitalitakasa jina langu kuu,+ ambalo lilichafuliwa miongoni mwa mataifa, ambalo mlilichafua miongoni mwao; nayo mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, ‘nitakapotakaswa miongoni mwenu mbele ya macho yao. 24  Nitawatoa kutoka kwa mataifa na kuwakusanya kutoka katika nchi zote na kuwaleta katika nchi yenu.+ 25  Nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi;+ nami nitawatakasa kutokana na uchafu wenu+ wote na kutokana na sanamu zenu zote zinazochukiza.+ 26  Nitawapa moyo mpya+ na kutia roho mpya ndani yenu.+ Nitauondoa moyo wa jiwe+ kutoka mwilini mwenu na kuwapa moyo wa nyama.* 27  Nitaitia roho yangu ndani yenu, nami nitawafanya mtembee katika masharti yangu,+ nanyi mtashika na kufuata sheria zangu.* 28  Kisha mtakaa katika nchi niliyowapa mababu zenu, nanyi mtakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wenu.’+ 29  “‘Nitawaokoa kutokana na uchafu wenu wote na kuiita nafaka na kuifanya iwe tele, nami sitawaletea njaa kali.+ 30  Nitayafanya matunda ya mti na mazao ya shamba yawe tele, ili msipatwe tena na aibu ya njaa kali miongoni mwa mataifa.+ 31  Kisha mtakumbuka njia zenu ovu na matendo yenu mabaya, nanyi mtajichukia kwa sababu ya hatia yenu na matendo yenu yanayochukiza.+ 32  Lakini jueni jambo hili: Sifanyi hivyo kwa ajili yenu,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Badala yake, aibikeni na kufedheheka kwa sababu ya njia zenu, enyi watu wa nyumba ya Israeli.’ 33  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Siku nitakayowatakasa kutokana na hatia yenu yote, nitayafanya majiji yakaliwe+ na magofu yajengwe upya.+ 34  Nchi yenye ukiwa, iliyokuwa ukiwa ili kila mtu anayepita aione, italimwa. 35  Na watu watasema: “Nchi iliyokuwa ukiwa imekuwa kama bustani ya Edeni,+ na majiji yaliyokuwa magofu na yaliyokuwa ukiwa na kubomolewa sasa yana ngome na yanakaliwa na watu.”+ 36  Na mataifa yaliyobaki kukuzunguka yatalazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimejenga kilichobomolewa, nami nimepanda kilichofanywa ukiwa. Mimi mwenyewe, Yehova, nimesema, nami nimelitenda.’+ 37  “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Nitawaruhusu pia watu wa nyumba ya Israeli waniombe niwatendee jambo hili: Nitazidisha idadi ya watu wao kama kundi. 38  Kama kundi la watu watakatifu, kama kundi la Yerusalemu* wakati wa sherehe zake,+ majiji yaliyokuwa magofu yatajaa makundi ya watu;+ nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”

Maelezo ya Chini

Tnn., “waliobaki.”
Au “dharau katika nafsi.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Yaani, moyo ulio mwepesi kutii mwongozo wa Mungu.
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Au labda, “Kama makundi ya kondoo wa dhabihu huko Yerusalemu.”