Ezekieli 37:1-28

  • Maono ya bonde la mifupa mikavu (1-14)

  • Vijiti viwili vitaunganishwa pamoja (15-28)

    • Taifa moja chini ya mfalme mmoja (22)

    • Agano la kudumu la amani (26)

37  Mkono wa Yehova ulikuwa juu yangu, naye Yehova akanichukua kwa roho yake na kuniweka chini katikati ya bonde tambarare,+ nalo lilikuwa limejaa mifupa.  Akanizungusha kwenye mifupa hiyo yote, nami nikaona kwamba kulikuwa na mifupa mingi sana katika bonde hilo tambarare, nayo ilikuwa mikavu sana.+  Akaniuliza: “Mwana wa binadamu, je, mifupa hii inaweza kuwa hai?” Nikajibu: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, wewe ndiye unayejua.”+  Basi akaniambia: “Itabirie mifupa hii, uiambie, ‘Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Yehova:  “‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ameiambia hivi mifupa hii: “Nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtakuwa hai.+  Nitaweka kano na nyama juu yenu, nami nitawafunika kwa ngozi na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtakuwa hai; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”’”  Kisha nikatabiri kama nilivyoamriwa. Mara tu nilipotabiri, nikasikia sauti, sauti ya vitu vinavyogongana, nayo mifupa ikaanza kukaribiana, mfupa kwa mfupa.  Kisha nikaona kano na nyama zikija juu yake, na ngozi ikazifunika. Lakini bado hakukuwa na pumzi ndani yake.  Kisha akaniambia: “Utabirie upepo. Tabiri, mwana wa binadamu, nawe uuambie upepo, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Njoo kutoka kwenye zile pepo nne, ewe upepo,* nawe uwapulizie watu waliouawa, ili wawe hai.”’” 10  Basi nikatabiri kama alivyoniamuru, nayo pumzi* ikaingia ndani yao, nao wakaanza kuishi na kusimama kwa miguu yao;+ walikuwa jeshi kubwa ajabu. 11  Kisha akaniambia: “Mwana wa binadamu, mifupa hii ni watu wote wa nyumba ya Israeli.+ Wanasema, ‘Mifupa yetu imekauka, nalo tumaini letu limepotea.+ Tumeangamizwa kabisa.’ 12  Basi tabiri uwaambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitayafungua makaburi yenu+ na kuwainua kutoka katika makaburi yenu, watu wangu, na kuwaleta katika nchi ya Israeli.+ 13  Nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova nitakapoyafungua makaburi yenu na nitakapowainua kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu.”’+ 14  ‘Nitaitia roho yangu ndani yenu,+ nanyi mtakuwa hai, nami nitawafanya mwishi katika nchi yenu; nanyi mtalazimika kujua kwamba mimi mwenyewe, Yehova, nimesema nami nimelitenda,’ asema Yehova.” 15  Neno la Yehova likanijia tena likisema: 16  “Nawe, mwana wa binadamu, chukua kijiti nawe uandike juu yake, ‘Kwa ajili ya Yuda na kwa ajili ya watu wa Israeli walio pamoja naye.’*+ Kisha uchukue kijiti kingine na kuandika juu yake, ‘Kwa ajili ya Yosefu, kijiti cha Efraimu, na watu wote wa nyumba ya Israeli walio pamoja naye.’*+ 17  Kisha viunganishe ili viwe kijiti kimoja tu mkononi mwako.+ 18  Watu wako* watakapokuuliza, ‘Je, hutatuambia mambo haya yanamaanisha nini?’ 19  waambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitakichukua kijiti cha Yosefu, kilicho mkononi mwa Efraimu, na makabila ya Israeli yaliyo pamoja naye, nami nitakiunganisha na kijiti cha Yuda; nami nitavifanya viwe kijiti kimoja,+ navyo vitakuwa kijiti kimoja mkononi mwangu.”’ 20  Vijiti utakavyoandika juu yake vinapaswa kuwa mkononi mwako ili wavione. 21  “Kisha uwaambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Nitawachukua Waisraeli kutoka katika mataifa ambako walienda, nami nitawakusanya pamoja kutoka kila upande na kuwaleta katika nchi yao.+ 22  Nitawafanya kuwa taifa moja katika nchi hiyo,+ kwenye milima ya Israeli, na mfalme mmoja atawatawala wote,+ nao hawatakuwa tena mataifa mawili; wala hawatagawanyika tena kuwa falme mbili.+ 23  Hawatajitia unajisi tena kwa sanamu zao zinazochukiza* na kwa matendo yao yanayochukiza na kwa makosa yao yote.+ Nitawaokoa kutoka katika ukosefu wao wote wa uaminifu ambao umewafanya watende dhambi, nami nitawatakasa. Watakuwa watu wangu, nami mwenyewe nitakuwa Mungu wao.+ 24  “‘“Mtumishi wangu Daudi atakuwa mfalme wao,+ na wote watakuwa na mchungaji mmoja.+ Watatembea katika sheria zangu* na kuzishika amri zangu kwa uangalifu.+ 25  Wataishi katika nchi niliyompa mtumishi wangu, Yakobo, ambamo mababu zenu waliishi,+ nao watakaa humo milele,+ wao na watoto* wao na watoto wa watoto wao;+ na mtumishi wangu Daudi atakuwa kiongozi* wao milele.+ 26  “‘“Nami nitafanya agano la amani pamoja nao;+ litakuwa agano la milele pamoja nao. Nitawaimarisha na kuwafanya wawe wengi+ na kupaweka mahali pangu patakatifu miongoni mwao milele. 27  Hema langu litakuwa* pamoja nao,* nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.+ 28  Na mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi, Yehova, ninawatakasa Waisraeli mahali pangu patakatifu patakapokuwa kati yao milele.”’”+

Maelezo ya Chini

Au “pumzi; roho.”
Au “roho.”
Au “wanaoshirikiana naye.”
Au “wanaoshirikiana naye.”
Tnn., “wana wa watu wako.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Au “mkuu.”
Tnn., “wana.”
Au “Makao yangu yatakuwa; Nyumba yangu itakuwa.”
Au “juu yao.”