Ezekieli 39:1-29

  • Kuangamizwa kwa Gogu na vikosi vyake (1-10)

  • Mazishi katika Bonde la Hamoni-Gogu (11-20)

  • Kurudishwa kwa Waisraeli (21-29)

    • Roho ya Mungu yamiminwa juu ya Waisraeli (29)

39  “Nawe, mwana wa binadamu, tabiri dhidi ya Gogu,+ umwambie, ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Niko dhidi yako, Gogu, kiongozi mkuu* wa Mesheki na Tubali.+  Nitakugeuza na kukuongoza na kukufanya uje kutoka sehemu za mbali zaidi za kaskazini+ na kukuleta kwenye milima ya Israeli.  Nitaupiga upinde wako utoke kwenye mkono wako wa kushoto na kufanya mishale yako ianguke kutoka kwenye mkono wako wa kulia.  Utaanguka kwenye milima ya Israeli,+ wewe na wanajeshi wako wote na mataifa yatakayokuwa pamoja nawe. Nitakufanya uwe chakula cha kila aina ya ndege wanaowinda na wanyama wa mwituni.”’+  “‘Utaanguka uwanjani,+ kwa maana mimi mwenyewe nimesema,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.  “‘Nami nitatuma moto dhidi ya Magogu na dhidi ya wale wanaokaa visiwani kwa usalama,+ nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.  Nitalifanya jina langu takatifu lijulikane miongoni mwa watu wangu Waisraeli, nami sitaruhusu jina langu takatifu lichafuliwe tena; na mataifa yatalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova,+ Mtakatifu katika Israeli.’+  “‘Naam, jambo hilo linakuja, nalo litatendeka,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. ‘Hiyo ndiyo siku ambayo nimesema kuihusu.  Kwa hakika wakaaji wa majiji ya Israeli watatoka nje na kuwasha moto kwa silaha—ngao ndogo* na ngao kubwa, pinde na mishale, rungu za vita* na mikuki. Nao watazitumia kuwasha moto+ kwa miaka saba. 10  Hawatahitaji kukusanya kuni shambani wala kuokota kuni misituni, kwa sababu watatumia silaha hizo kuwasha mioto.’ “‘Watawateka nyara wale waliowateka nyara na kuwapora wale waliokuwa wakiwapora,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 11  “‘Siku hiyo, nitampa Gogu+ kaburi katika Israeli, kwenye bonde la wale wanaosafiri upande wa mashariki wa bahari, nalo litazuia njia ya wale wanaopitia humo. Hapo ndipo watakapomzika Gogu na umati wake wote, nao wataliita Bonde la Hamon-Gogu.*+ 12  Kwa miezi saba watu wa nyumba ya Israeli watawazika ili kuitakasa nchi.+ 13  Watu wote wa nchi watafanya kazi ya kuwazika, na hilo litawaletea umaarufu siku nitakayojitukuza,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 14  Watu watapewa kazi ya kupitapita nchini daima na kuizika miili iliyobaki juu ya dunia, ili kuitakasa dunia. Wataendelea kutafuta kwa miezi hiyo saba. 15  Wale wanaopitapita nchini watakapoona mfupa wa mwanadamu, wataweka alama kando yake. Kisha wale waliopewa kazi ya kuzika watauzika mfupa huo katika Bonde la Hamon-Gogu.+ 16  Na huko pia kutakuwa na jiji linaloitwa Hamona.* Nao wataitakasa nchi.’+ 17  “Nawe, mwana wa binadamu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Waambie ndege wa kila aina na wanyama wote wa mwituni, “Kusanyikeni pamoja na mje. Kusanyikeni kuzunguka dhabihu yangu ninayowatayarishia, dhabihu kubwa kwenye milima ya Israeli.+ Mtakula nyama na kunywa damu.+ 18  Mtakula nyama ya wenye nguvu na kunywa damu ya viongozi wa dunia—kondoo dume, wanakondoo, mbuzi, na ng’ombe dume—wanyama wote waliononeshwa wa Bashani. 19  Mtakula mafuta kwa pupa mpaka mshibe na kunywa damu mpaka mlewe kutokana na dhabihu nitakayowatayarishia.”’ 20  “‘Mtashibishwa mezani pangu kwa farasi na waendeshaji wa magari, watu wenye nguvu na kila aina ya mashujaa,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova. 21  “‘Nitauonyesha wazi utukufu wangu kati ya mataifa, nayo mataifa yote yataona hukumu ambayo nimetekeleza na nguvu nilizoonyesha* kati yao.+ 22  Kuanzia siku hiyo, watu wa nyumba ya Israeli watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao. 23  Nayo mataifa yatalazimika kujua kwamba watu wa nyumba ya Israeli walipelekwa uhamishoni kwa sababu ya kosa lao, kwa sababu hawakuwa waaminifu kwangu.+ Basi niliwaficha uso wangu+ na kuwatia mikononi mwa maadui wao,+ na wote wakauawa kwa upanga. 24  Niliwatendea kulingana na uchafu wao na makosa yao, nami nikawaficha uso wangu.’ 25  “Kwa hiyo Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: ‘Nitawarudisha watu wa Yakobo waliotekwa+ na kuwaonyesha rehema watu wote wa nyumba ya Israeli;+ nami nitalitetea jina langu takatifu kwa bidii.*+ 26  Baada ya kufedheheshwa kwa sababu ya ukosefu wao wote wa uaminifu kunielekea,+ watakaa kwa usalama katika nchi yao, na hakuna mtu atakayewaogopesha.+ 27  Nitakapowarudisha kutoka katika mataifa na kuwakusanya pamoja kutoka katika nchi za maadui wao,+ mimi pia nitajitakasa miongoni mwao mbele ya macho ya mataifa mengi.’+ 28  “‘Watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao nitakapowapeleka uhamishoni miongoni mwa mataifa na kuwarudisha katika nchi yao, bila kumwacha yeyote kati yao huko.+ 29  Sitawaficha uso wangu tena,+ kwa maana nitawamiminia roho yangu watu wa nyumba ya Israeli,’+ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”

Maelezo ya Chini

Au “mkuu wa wakuu.”
Kwa kawaida ilibebwa na wapiga mishale.
Au labda, “silaha zenye ncha kali zilizovaliwa mkononi.”
Au “Bonde la Umati wa Gogu.”
Maana yake “Umati.”
Tnn., “mkono nilioonyesha.”
Tnn., “nitajitoa kikamili kwa ajili ya jina langu takatifu.”