Ezekieli 4:1-17

  • Aonyesha jinsi Yerusalemu litakavyozingirwa (1-17)

    • Abeba hatia kwa siku 390 na siku 40 (4-7)

4  “Na wewe, mwana wa binadamu, chukua tofali na uliweke mbele yako. Uchonge jiji juu yake—Yerusalemu.  Lizingire na ujenge ukuta wa kulizingira,+ utengeneze boma la kulizingira,+ upige kambi kulizunguka,+ na kulizungushia mitambo ya kubomolea.+  Chukua kiokeo cha chuma, na ukiweke kuwa ukuta wa chuma kati yako na jiji hilo. Kisha ukaze uso wako dhidi yake, nalo litazingirwa; nawe utalizingira. Hiyo ni ishara kwa watu wa nyumba ya Israeli.+  “Kisha ulalie upande wako wa kushoto na uweke hatia ya watu wa nyumba ya Israeli juu yako.*+ Utabeba hatia yao kwa idadi ya siku utakazolalia upande wako wa kushoto.  Na mimi nitakupa wewe siku 390, zinazolingana na miaka ya hatia yao,+ nawe utaibeba hatia ya watu wa nyumba ya Israeli.  Nawe lazima uzitimize. “Kisha kwa mara ya pili utalala chini, utalalia upande wako wa kulia, nawe utaibeba hatia ya watu wa nyumba ya Yuda+ kwa siku 40. Nimekupa wewe siku moja kwa mwaka mmoja, siku moja kwa mwaka mmoja.  Nawe utauelekeza uso wako kwa jiji la Yerusalemu lililozingirwa,+ mkono wako ukiwa wazi, nawe utatabiri dhidi ya jiji hilo.  “Tazama! Nitakufunga kwa kamba ili usiweze kugeuka kutoka upande mmoja kwenda upande mwingine, mpaka utakapotimiza siku zako za kulizingira.  “Na uchukue ngano, shayiri, maharagwe mapana, dengu, mtama, na kusemethi, nawe uvitie katika chombo kimoja na ujitengenezee mkate. Kwa idadi ya siku unazolalia upande wako, siku 390, utaula.+ 10  Utapima na kula shekeli 20* za chakula kwa siku. Utaula nyakati hususa. 11  “Na utakunywa maji kwa kipimo, sehemu ya sita ya hini.* Utayanywa nyakati hususa. 12  “Utaula kama ambavyo ungekula mkate wa mviringo wa shayiri; utauoka mbele ya macho yao, ukitumia mavi ya wanadamu yaliyokauka.” 13  Na Yehova akaendelea kusema: “Hivyo ndivyo Waisraeli watakavyoula mkate wao—usio safi—kati ya mataifa ambako nitawatawanya.”+ 14  Ndipo nikasema: “Isiwe hivyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tangu ujana wangu mpaka sasa sijatiwa* unajisi kwa kula nyama ya mnyama ambaye amepatikana amekufa wala mnyama aliyeraruliwa,+ na nyama isiyo safi* haijawahi kuingia kinywani mwangu.”+ 15  Basi akaniambia: “Sawa, nitakuruhusu utumie mavi ya ng’ombe badala ya mavi ya wanadamu, nawe utaoka mkate wako juu yake.” 16  Naye akaniambia: “Mwana wa binadamu, nitafanya chakula kikosekane* Yerusalemu,+ na kwa wasiwasi mwingi watakula mkate wao kwa kipimo,+ na kwa hofu nyingi watakunywa maji yao kwa kipimo.+ 17  Hili litatukia ili wakose mkate na maji, nao waangaliane kwa mshtuko na kudhoofika kwa sababu ya kosa lao.

Maelezo ya Chini

Tnn., “juu yake,” yaani, upande wa kushoto wa Ezekieli.
Karibu gramu 230. Angalia Nyongeza B14.
Karibu lita 0.6. Angalia Nyongeza B14.
Au “nafsi yangu haijatiwa.”
Au “mbaya.”
Tnn., “nitazivunja fito za mikate.” Labda ni fito zilizotumiwa kuhifadhia mikate.