Ezekieli 47:1-23

  • Kijito kinachotiririka kutoka hekaluni (1-12)

    • Kina cha maji chaongezeka hatua kwa hatua (2-5)

    • Maji ya Bahari ya Chumvi yaponywa (8-10)

    • Sehemu zenye majimaji haziponywi (11)

    • Miti kwa ajili ya chakula na kuponya (12)

  • Mipaka ya nchi (13-23)

47  Kisha akanirudisha kwenye mlango wa hekalu,+ na hapo nikaona maji yakitiririka kuelekea mashariki kutoka chini ya kizingiti cha hekalu,+ kwa maana upande wa mbele wa hekalu ulitazama mashariki. Maji hayo yalikuwa yakitiririka kutoka chini upande wa kulia wa hekalu, upande wa kusini wa madhabahu.  Kisha akaniongoza nje kupitia lango la kaskazini+ na kunizungusha nje mpaka kwenye lango la nje linalotazama upande wa mashariki,+ nikaona maji yakitiririka kutoka upande wa kulia.  Mtu huyo alipotoka nje kuelekea mashariki akiwa na kamba ya kupimia mkononi mwake,+ alipima mikono 1,000* na kunipitisha katika maji; maji hayo yalifika kwenye vifundo vya miguu.  Kisha akapima mikono mingine 1,000 na kunipitisha katika maji, nayo yalifika mpaka kwenye magoti. Akapima mikono mingine 1,000 na kunipitisha humo, na maji hayo yalifika kiunoni.  Alipopima mikono mingine 1,000, maji yalikuwa mengi sana hivi kwamba singeweza kuvuka, kwa maana maji hayo yalikuwa na kina kirefu hivi kwamba mtu angelazimika kuogelea, maji mengi sana ambayo mtu hangeweza kuvuka kwa miguu.  Akaniuliza: “Mwana wa binadamu, je, umeona hili?” Kisha akanitembeza na kunirudisha kwenye ukingo wa kile kijito.  Niliporudi, nikaona miti mingi sana pande zote za ukingo wa kile kijito.+  Ndipo akaniambia: “Maji haya yanatiririka kuelekea eneo la mashariki na yanashuka kupitia Araba*+ na kuingia baharini. Yakiingia baharini,+ maji ya bahari yataponywa.  Kila mahali ambapo maji hayo yanapita, makundi makubwa ya viumbe walio* hai yataishi. Kutakuwa na samaki wengi, kwa sababu maji hayo yatatiririka* huko. Maji ya baharini yataponywa, na mahali ambapo kijito hicho kinapita, kila kitu kitaishi. 10  “Wavuvi watasimama kando yake kutoka En-gedi+ mpaka En-eglaimu ambako kutakuwa na uwanja wa kukaushia nyavu za kukokotwa. Kutakuwa na samaki wengi wa aina nyingi, kama samaki wa ile Bahari Kuu.*+ 11  “Kutakuwa na sehemu zenye majimaji na matope, nazo hazitaponywa. Zitabaki zikiwa sehemu za chumvi.+ 12  “Aina zote za miti ya chakula zitakua kwenye kingo zote mbili za hicho kijito. Majani yake hayatanyauka; wala miti hiyo haitakosa kuzaa matunda. Kila mwezi itazaa matunda mapya, kwa sababu maji yake yanatiririka kutoka patakatifu.+ Matunda yake yatakuwa chakula na majani yake yatatumiwa kuponya.”+ 13  Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova anasema hivi: “Hili ndilo eneo ambalo mtayagawia yale makabila 12 ya Israeli kuwa urithi wao wa ardhi, na Yosefu atapata sehemu mbili.+ 14  Nanyi mtairithi na kuigawa kwa usawa.* Niliapa kuwapatia mababu zenu nchi hii,+ na sasa mmegawiwa* ili iwe urithi wenu. 15  “Huu ndio mpaka wa kaskazini wa nchi: Unaanzia ile Bahari Kuu kupitia njia ya Hethloni+ kuelekea Sedadi,+ 16  Hamathi,+ Berotha,+ na Sibraimu, kati ya eneo la Damasko na eneo la Hamathi, hadi Haser-hatikoni, karibu na mpaka wa Haurani.+ 17  Basi mpaka utaanzia baharini hadi Hasar-enoni,+ kwenye mpaka wa Damasko kuelekea kaskazini, pamoja na mpaka wa Hamathi.+ Huo ndio mpaka wa kaskazini. 18  “Upande wa mashariki mpaka huo unapita kati ya Haurani na Damasko na kando ya Yordani kati ya Gileadi+ na nchi ya Israeli. Mnapaswa kupima kutoka mpakani hadi kwenye bahari ya mashariki.* Huo ndio mpaka wa mashariki. 19  “Mpaka wa kusini* utaanzia Tamari hadi kwenye maji ya Meribath-kadeshi,+ kisha utaelekea kwenye lile Korongo* hadi kwenye ile Bahari Kuu.+ Huo ndio mpaka wa kusini.* 20  “Bahari Kuu iko upande wa magharibi, kuanzia kwenye mpaka hadi kwenye eneo lililo ng’ambo ya Lebo-hamathi.*+ Huo ndio mpaka wa magharibi.” 21  “Mnapaswa kugawana nchi hii miongoni mwenu, miongoni mwa makabila 12 ya Israeli. 22  Mnapaswa kuigawa iwe urithi miongoni mwenu wenyewe na kuwagawia wageni wanaoishi pamoja nanyi ambao wamezaa watoto wakati wanaishi miongoni mwenu; nao watakuwa kwenu kama Waisraeli wenyeji. Watapokea urithi pamoja nanyi miongoni mwa makabila ya Israeli. 23  Mnapaswa kumpa mkaaji mgeni urithi katika eneo la kabila analoishi ndani yake,” asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.

Maelezo ya Chini

Hiki ni kipimo cha mikono mirefu. Angalia Nyongeza B14.
Au “jangwa tambarare.”
Au “nafsi zilizo.”
Tnn., “vijito hivyo viwili vitatiririka.”
Yaani, Bahari ya Mediterania.
Tnn., “mtairithi, kila mtu kama ndugu yake.”
Tnn., “inawaangukia.”
Yaani, Bahari ya Chumvi.
Tnn., “upande wa kusini kuelekea kusini.”
Yaani, Korongo la Misri.
Tnn., “upande wa kusini kuelekea kusini.”
Au “njia ya kuingia Hamathi.”