Ezekieli 8:1-18

  • Ezekieli apelekwa Yerusalemu katika maono (1-4)

  • Vitu vinavyochukiza vyaonekana hekaluni (5-18)

    • Wanawake wakimlilia Tamuzi (14)

    • Wanaume wakiabudu jua (16)

8  Na katika mwaka wa sita, mwezi wa sita, siku ya tano ya mwezi huo, nilipokuwa nimeketi nyumbani mwangu na wazee wa Yuda walipokuwa wameketi mbele yangu, mkono wa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ulinishika nikiwa hapo.  Nilipokuwa nikitazama, niliona umbo lililoonekana kama moto; kulikuwa na moto chini ya kitu kilichoonekana kama kiuno chake,+ na kuanzia kiuno chake kwenda juu, mwonekano wake uling’aa kama mchanganyiko wa dhahabu na fedha.+  Kisha akanyoosha kitu kilichoonekana kama mkono na kuniinua kwa kishungi cha nywele za kichwa changu, na roho ikanibeba katikati ya dunia na mbingu na kunileta Yerusalemu kupitia maono kutoka kwa Mungu, kwenye njia inayoelekea kwenye lango la ndani+ linalotazama kaskazini, mahali ilipokuwa ishara ya* ibada ya sanamu inayochochea wivu.+  Na tazama! utukufu wa Mungu wa Israeli ulikuwa hapo,+ kama mwonekano niliokuwa nimeuona katika bonde tambarare.+  Kisha akaniambia: “Mwana wa binadamu, tafadhali inua macho yako kuelekea kaskazini.” Basi nikainua macho yangu kuelekea kaskazini, na huko, upande wa kaskazini wa lango la madhabahu kulikuwa na ishara hii ya* wivu langoni.  Naye akaniambia: “Mwana wa binadamu, je, unaona mambo mabaya sana na yenye kuchukiza ambayo watu wa nyumba ya Israeli wanafanya hapa,+ mambo yanayonifanya niende mbali sana na mahali pangu patakatifu?+ Lakini utaona mambo yanayochukiza yaliyo mabaya hata zaidi.”  Kisha akanileta kwenye mlango wa ua, nami nilipotazama, niliona tundu ukutani.  Akaniambia: “Mwana wa binadamu, tafadhali toboa ukuta.” Nami nikautoboa ukuta na kuona mlango.  Akaniambia: “Ingia ndani uone mambo maovu na yenye kuchukiza wanayofanya hapa.” 10  Basi nikaingia na kutazama, nikaona mifano mbalimbali ya viumbe wanaotambaa na wanyama wanaochukiza+ na sanamu zote zinazochukiza* za watu wa nyumba ya Israeli;+ zilikuwa zimechongwa ukutani kuzunguka pande zote. 11  Na wazee 70 wa nyumba ya Israeli walikuwa wamesimama mbele ya vitu hivyo, naye Yaazania mwana wa Shafani+ alikuwa amesimama miongoni mwao. Kila mmoja wao alikuwa na chetezo chake mkononi mwake, na wingu la uvumba lenye manukato lilikuwa likipanda juu.+ 12  Akaniambia: “Mwana wa binadamu, je, umeona mambo ambayo wazee wa nyumba ya Israeli wanafanya gizani, kila mmoja akiwa katika vyumba vya ndani ambamo sanamu zake za kuchongwa zimewekwa ili zionekane?* Kwa maana wanasema, ‘Yehova hatuoni. Yehova ameiacha nchi hii.’”+ 13  Naye akaendelea kuniambia: “Utaona mambo yanayochukiza yaliyo mabaya hata zaidi ambayo wanafanya.” 14  Basi akanileta kwenye njia inayoelekea kwenye lango la kaskazini la nyumba ya Yehova, na huko nikaona wanawake wameketi wakimlilia mungu Tamuzi. 15  Naye akaendelea kuniambia: “Je, unaona mambo haya, ewe mwana wa binadamu? Utaona mambo yanayochukiza ambayo ni mabaya hata zaidi kuliko haya.”+ 16  Basi akanileta katika ua wa ndani wa nyumba ya Yehova.+ Hapo kwenye mlango wa hekalu la Yehova, katikati ya ukumbi na madhabahu, kulikuwa na wanaume 25 hivi ambao migongo yao ilielekea hekalu la Yehova na nyuso zao zilitazama mashariki; nao walikuwa wakiliinamia jua kuelekea mashariki.+ 17  Akaniambia: “Mwana wa binadamu, je, unaona hili? Je, ni jambo dogo sana kwa watu wa nyumba ya Yuda kufanya mambo haya yanayochukiza, kuijaza nchi ukatili+ na kuendelea kunikasirisha? Tazama, wanaidunga pua yangu kwa lile tawi.* 18  Basi nitatenda kwa ghadhabu. Jicho langu halitasikitika; wala sitawahurumia.+ Hata wakilia kwa sauti kubwa masikioni mwangu, sitawasikia.”+

Maelezo ya Chini

Au “mfano wa.”
Au “mfano huu wa.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.
Au “katika vyumba vya ndani vya sanamu yake bora?”
Inaonekana ni tawi lililotumiwa katika ibada ya sanamu.