Ezra 3:1-13

  • Madhabahu yajengwa upya na dhabihu zatolewa (1-7)

  • Kazi ya kujenga upya hekalu yaanza (8, 9)

  • Msingi wa hekalu wawekwa (10-13)

3  Mwezi wa saba+ ulipofika Waisraeli* walikuwa katika majiji yao; wakakusanyika Yerusalemu wakiwa na kusudi moja.  Yeshua+ mwana wa Yehosadaki na makuhani wenzake na Zerubabeli+ mwana wa Shealtieli+ na ndugu zake wakasimama na kujenga madhabahu ya Mungu wa Israeli, ili kutoa dhabihu za kuteketezwa juu yake, kama ilivyoandikwa katika Sheria ya Musa,+ mtu wa Mungu wa kweli.  Basi wakajenga madhabahu mahali ilipokuwa zamani, ingawa waliwaogopa watu wa nchi jirani,+ nao wakaanza kumtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa juu yake, asubuhi na jioni.+  Kisha wakafanya Sherehe ya Vibanda* kulingana na ilivyoandikwa,+ na siku baada ya siku walitoa idadi iliyohitajika ya dhabihu za kuteketezwa.+  Baadaye walitoa dhabihu za kuteketezwa zilizotolewa kwa ukawaida+ na matoleo kwa ajili ya miezi mipya+ na majira yote yaliyotakaswa+ ya sherehe za Yehova, na pia toleo la hiari la kila mtu aliyemtolea Yehova kwa kupenda.+  Tangu siku ya kwanza ya mwezi wa saba,+ walianza kumtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa, ingawa bado msingi wa hekalu la Yehova haukuwa umewekwa.  Wakawapa pesa wakataji wa mawe+ na mafundi,+ na kuwapa Wasidoni na Watiro vyakula na vinywaji na mafuta ili walete mbao za mierezi kupitia bahari kutoka Lebanoni mpaka Yopa,+ kwa ruhusa ya Mfalme Koreshi wa Uajemi.+  Katika mwaka wa pili tangu walipofika kwenye nyumba ya Mungu wa kweli huko Yerusalemu, katika mwezi wa pili, Zerubabeli mwana wa Shealtieli, Yeshua mwana wa Yehosadaki na ndugu zao wote, makuhani na Walawi, na wale wote waliorudi Yerusalemu kutoka utekwani+ wakaanza kazi; wakawaweka rasmi Walawi kuanzia umri wa miaka 20 na zaidi wawe wasimamizi wa kazi ya nyumba ya Yehova.  Basi Yeshua, wanawe na ndugu zake, na Kadmieli na wanawe, wana wa Yuda, wakaungana ili kuwasimamia wale waliokuwa wakifanya kazi katika nyumba ya Mungu wa kweli, pamoja na wana wa Henadadi,+ wana wao na ndugu zao Walawi. 10  Wajenzi walipoweka msingi wa hekalu la Yehova,+ makuhani waliovaa mavazi rasmi, wakiwa na tarumbeta,+ na Walawi, wana wa Asafu, wakiwa na matoazi, wakasimama ili kumsifu Yehova kulingana na maagizo ya Mfalme Daudi wa Israeli.+ 11  Nao wakaanza kuimba kwa kuitikia+ wakimsifu na kumshukuru Yehova “kwa maana yeye ni mwema; upendo wake mshikamanifu kwa Israeli unadumu milele.”+ Kisha watu wote wakapaza sauti wakimsifu Yehova kwa sababu msingi wa nyumba ya Yehova ulikuwa umewekwa. 12  Makuhani wengi, Walawi, na viongozi wa koo*—wazee ambao walikuwa wameona ile nyumba ya kwanza+—wakalia kwa sauti kubwa walipoona msingi wa nyumba hii ukiwekwa, na wengine wengi wakapaza sauti yao yote kwa shangwe.+ 13  Hivyo watu hawakuweza kutofautisha kati ya sauti ya kushangilia na ya kulia, kwa maana watu walikuwa wakipaza sauti kubwa hivi kwamba sauti hiyo ikasikika mbali sana.

Maelezo ya Chini

Tnn., “wana wa Israeli.”
Au “Vibanda vya Muda.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.