Ezra 4:1-24

  • Kazi ya kujenga upya hekalu yapingwa (1-6)

  • Maadui watuma malalamishi kwa Mfalme Artashasta (7-16)

  • Artashasta ajibu (17-22)

  • Ujenzi wa hekalu wasimamishwa (23, 24)

4  Maadui wa Yuda na Benjamini+ waliposikia kwamba watu waliorudi kutoka uhamishoni+ walikuwa wakimjengea hekalu Yehova Mungu wa Israeli,  mara moja wakamfikia Zerubabeli na viongozi wa koo* na kuwaambia: “Acheni tujenge pamoja nanyi; kwa maana, sisi pia tunamwabudu* Mungu wenu+ na tumekuwa tukimtolea dhabihu tangu siku za Mfalme Esar-hadoni+ wa Ashuru, aliyetuleta hapa.”+  Hata hivyo, Zerubabeli na Yeshua na viongozi wa koo* za Israeli wakawaambia: “Hamna haki ya kujenga pamoja nasi nyumba ya Mungu wetu,+ kwa maana sisi wenyewe tutamjengea Yehova Mungu wa Israeli, kama alivyotuamuru Mfalme Koreshi, mfalme wa Uajemi.”+  Ndipo watu wa mataifa jirani wakazidi kuwavunja moyo* watu wa Yuda na kuwakatisha tamaa ili wasijenge.+  Waliwakodi washauri ili kuvuruga mipango yao ya kujenga,+ siku zote za Mfalme Koreshi wa Uajemi mpaka wakati wa utawala wa Mfalme Dario+ wa Uajemi.  Mwanzoni mwa utawala wa Ahasuero, waliandika mashtaka dhidi ya wakaaji wa Yuda na Yerusalemu.  Na katika siku za utawala wa Mfalme Artashasta wa Uajemi, Bishlamu, Mithredathi, Tabeeli, na wenzake walimwandikia Mfalme Artashasta; wakaitafsiri barua hiyo katika Kiaramu,+ na kuiandika kwa herufi za Kiaramu.*  * Rehumu ofisa mkuu wa serikali na mwandishi Shimshai, walimwandikia Mfalme Artashasta barua ifuatayo dhidi ya Yerusalemu:  (Ilitoka kwa Rehumu ofisa mkuu wa serikali na mwandishi Shimshai na wenzao, yaani, waamuzi na magavana wadogo, waandishi, watu wa Ereki,+ Wababiloni, wakaaji wa Susa,+ yaani, Waelamu,+ 10  na mataifa mengine yote ambayo Asenapari mkuu na mheshimiwa aliwahamisha na kuwapeleka katika majiji ya Samaria,+ na wengine walio Ng’ambo ya Mto,* basi sasa 11  hii ndiyo nakala ya barua waliyomtumia.) “Kwa Mfalme Artashasta kutoka kwa watumishi wako, watu walio Ng’ambo ya Mto: Sasa 12  tungependa kumjulisha mfalme kwamba Wayahudi waliokuja huku kutoka kwako wamefika Yerusalemu. Wanajenga upya lile jiji lenye uasi na uovu, nao wanamalizia kujenga kuta+ na kurekebisha misingi yake. 13  Sasa tungependa mfalme ajue kwamba ikiwa jiji hili litajengwa upya na kuta zake kukamilishwa, hawatalipa kodi, ushuru,+ wala ada, na jambo hilo litasababisha hasara kwa hazina za wafalme. 14  Na kwa kuwa sisi hula chumvi ya jumba la mfalme* na si vema kwetu kuona masilahi ya mfalme yakiathiriwa, ndiyo sababu tumetuma barua ili kumjulisha mfalme jambo hilo, 15  ili uchunguzi ufanywe katika kitabu cha kumbukumbu za mababu zako.+ Ndipo utakapoona katika kitabu hicho cha kumbukumbu kwamba hili ni jiji lenye uasi, linalowaletea hasara wafalme na mikoa,* na tangu zamani lilikuwa na wachochezi wa uasi. Ndiyo sababu jiji hili liliangamizwa.+ 16  Tunakujulisha mfalme kwamba jiji hili likijengwa upya na kuta zake kukamilishwa, hutaweza kutawala tena* eneo lililo Ng’ambo ya Mto.”+ 17  Mfalme akatuma ujumbe ufuatao kwa Rehumu ofisa mkuu wa serikali na mwandishi Shimshai na wenzao walioishi Samaria na katika eneo lote lililo Ng’ambo ya Mto: “Salamu! Na sasa 18  barua rasmi mliyotutumia imesomwa waziwazi* mbele yangu. 19  Niliagiza uchunguzi ufanywe na ikajulikana kwamba tangu zamani jiji hilo limewapinga wafalme, na limekuwa na uchochezi na uasi.+ 20  Kulikuwa na wafalme wenye nguvu juu ya Yerusalemu waliotawala eneo lote la Ng’ambo ya Mto, nao walikuwa wakilipwa kodi, ushuru, na ada. 21  Sasa toeni amri ili kusimamisha kazi ya wanaume hao, ili jiji hilo lisijengwe upya mpaka nitakapotoa agizo. 22  Hakikisheni amri hii inatekelezwa bila uzembe, ili masilahi ya mfalme yasiendelee kuathiriwa.”+ 23  Sasa baada ya nakala ya barua rasmi ya Mfalme Artashasta kusomwa mbele ya Rehumu na mwandishi Shimshai na wenzao, mara moja wakaenda Yerusalemu na kuwalazimisha Wayahudi waache kujenga. 24  Ndipo kazi ya kujenga nyumba ya Mungu, iliyokuwa Yerusalemu, iliposimamishwa; na haikuendelea mpaka mwaka wa pili wa utawala wa Mfalme Dario wa Uajemi.+

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “tunamtafuta.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “kuilegeza mikono ya.”
Au labda, “iliandikwa katika Kiaramu kisha ikatafsiriwa.”
Mwanzoni, maandishi ya Ezr 4:8 hadi 6:18 yaliandikwa katika Kiaramu.
Au “maeneo yaliyo magharibi ya Mto Efrati.”
Au “tunapokea mshahara wetu kutoka kwenye makao ya mfalme.”
Au “wilaya za utawala.”
Tnn., “hutakuwa na fungu katika.”
Au labda, “imetafsiriwa na kusomwa.”